Quantcast
Channel: Zanzibar Daima – Zanzibar Daima
Viewing all articles
Browse latest Browse all 854

Nguzo ya pili ya mitaji ya mafanikio ni fikra

$
0
0

Katika makala ya juma lililopita niliweka bayana kwamba nguzo ya kwanza ya mitaji ya mafanikio ni Afya Njema ya Mwili. Mwili wenye afya njema ndicho chombo cha kutekelezea mawazo yako endapo ni mazuri, murua na ikiwa yamechujwa na kupimwa. Kila uamkapo asubuhi, kichwani kwako unafikiria cha kufanya, mahali kwa kwenda na namna ya kwenda huko. Mwili wenye afya njema unakuwezesha kuwaza cha kutenda. Na kwahiyo, nguzo ya pili ya mitaji ya mafanikio ni “Fikra” au “Mawazo.”

Kila kitu kinachofanyika kwa vitendo huanzia kichwani – kinatokana na fikra au mawazo (ideas) ya vichwani mwetu. Wengine huenda mbali zaidi na kusema vitu vyote vinavyotuzunguka na kuonekana kwa macho, kugusika au kushikika (tangibles), chimbuko lake ni vitu visivyoonekana (intangibles), yaani fikra au mawazo. Amini usiamini, hata kuwepo kwa sayari ya dunia na zinginezo, pamoja na ulimwengu mzima, wa vitu hai na visivyo hai, kulitokana na mawazo! Uumbaji huanzia kwenye mawazo, na hadi sasa tunaendelea kuumba au kutengeneza vitu kwa kuanza navyo kichwani.

Na kwa kusema hivyo, lazima niweke wazi kuwa zipo fikra mbovu au potofu na fikra pevu. Zote ni fikra au mawazo, lakini tutajikita zaidi katika fikra pevu – zilizopikwa kichwani na kuiva, zenye faida ya kutuletea maendeleo ya mtu binafsi, jamii na ulimwengu kwa ujumla. Bila fikra, tunabakia watupu kama makopo au mapipa yaliyowazi. Fikra ni mwanga wa giza na zinaweza kubadili chochote kutoka kutokuwa na faida kwenda kwenye mafanikio. Ilimradi una afya njema ya mwili na akili, tayari una nguzo muhimu za kukupatia mafanikio katika maisha.

Fikra ni ubunifu alionao mtu kichwani au akilini mwake. Hata fedha ulizonazo mkononi, mfukoni, kwenye pochi yako au benki, ni sarafu au makaratasi tu yanayochapishwa na kutupwa au kubadilishwa baada ya kutumika. Lakini fikra au mawazo yaliyosababisha upate hayo makaratasi unayoyaita fedha taslimu ndio msingi au nguzo muhimu ya mafanikio yako. Hakuna anayepinga ukweli huu, na kwahiyo nami napata fursa nzuri ya kujadili kwa kina kuthibitisha kuwa fikra au mawazo ni mtaji tosha.

Mchango wa fikra na mawazo katika maendeleo ya watu

Angalia maandishi mbalimbali yenye maelezo (information), maelekezo (instructions) na miongozo (guidelines) mbalimbali. Sikiliza sauti kwenye vyombo mbalimbali vya kutunzia na/au kunasia sauti. Ni kama mchanga wa bahari ya mawazo kutoka vichwani mwetu. Hata mtu akifa bado ataendelea kuishi nasi kupitia mawazo yake yaliyoandikwa au kurekodiwa (audio), na pengine hata picha zake mnyato (video) tutaendelea kuishi nazo daima.

Aidha, fikra ni ndoto au maono ya mtu anayoyafanyia kazi yeye mwenyewe au wengine ili yatimie. Kuna watu wengi wametupa maono pevu na kuleta mafanikio makubwa sana katika jamii. Dkt Martin Luther King alikuwa na ndoto ya jamii inayojali utu, haki na usawa nchini Marekani.

Ndoto alizoota na kutamka Dkt King, ziliandikwa, zikarekodiwa na kutimia kwa mtu mwenye asili ya Afrika, Barack Hussein Onyango Obama, alipokuja kuapishwa rasmi mnamo Januari 20, 2009 kuwa rais wa Marekani. Ilipita miaka zaidi ya 40 baada ya Dkt King kufariki. Mwili wake ulikufa lakini mawazo yake yaliendelea na yanaendelea kuishi nasi – yuko hai pamoja na Wamarekani na wapenda haki duniani kote kupitia fikra zake za ukombozi.

Nelson Mandela alikuwa jela, lakini fikra zake za ukombozi zilirindima duniani kote na zikaja kufungua milango ya gereza na hatimaye akawa rais wa kwanza mweusi Afrika Kusini.

Fikra alizokuwa nazo Dkt Martin Luther King zimesaidia sana kuibadilisha Marekani

Fikra za ukombozi za Nelson Mandela zilisaidia kwa kiasi kikubwa kuondoa ukaburu Afrika Kusini

Nisisitize kuwa tuliumbwa kwanza ili tufikiri na ndipo tuishi, hatukuumbwa kuishi ndipo tufikiri. Tuko hivi tulivyo kutokana na jinsi tunavyofikiri. Bila kufikiri tunakuwa si watu, tunabaki kama vyombo vya kutumika na kutumiwa na wengine. Kama kuna utumwa mbaya na jela mbaya kuliko zote, basi ni kubinywa kufikiri. Naamini kabisa kikwazo kikubwa cha maendeleo yetu si kukosa rasilimali, bali kukosa fikra za jinsi ya kuzitumia rasilimali zetu kwa faida yetu. Ufukara mbaya kabisa na adui mkubwa kuliko maradhi na umaskini ni kukosa fikra.

Tukikosa ubunifu kichwani tunakosa kila kitu – hata kilicho chetu! Na kamwe tusiruhusu watu wengine au mataifa mengine yawaze kwa niaba yetu, kwa kuwa watakuwa wanawaza kwa faida yao. Tuwe makini sana katika kila tunachowaza ili kiwe na faida kwetu na jamii tuliyomo. Kama kuna urithi bora na udumuo kwa familia na jamii yetu basi ni fikra. Ni muhimu sana kuziandika au kuzirekodi ili tusije kufukiwa nazo kaburini.

Ulimwengu mzima unaendeshwa na kuendelezwa na mawazo. Watu wanatafakari na kukuna vichwa vyao kila siku. Hata Mungu katika misahafu hakutupa fedha au vitu, bali mawazo ya kutusaidia namna bora ya kuishi kistaarabu katika maisha haya na yajayo.

Magari, ndege, maghorofa, simu, umeme, kompyuta, viwanda, nk.; vilianza na wazo na kisha kuendelezwa. Jaribu kufikiria dunia ya wakati wa bila simu wala umeme, kisha angalia mafanikio yake sasa. Msingi wa jambo lolote lile, katika kila nyanja na fani kutoka siasa hadi teknolojia, ni fikra.

Baba wa sayansi ya kileo Galileo Galilei (1564-1642) alikuna kichwa na kugundua anga lilivyojaa sayari mbalimbali na namna zinavyovutana na/au kuzungukana. Alexander Graham Bell alikuna kichwa namna rahisi ya kuwasiliana kwa sauti tukiwa mbali, akagundua simu. Michael Faraday na wengineo, waliwaza na kugundua nguvu za sumaku na elektroni tukapata umeme na mkondo wake wa hasi na chanya.

Tukumbuke ugunduzi wa Archimedes na Isaac Newton unavyotusaidia katika ufundi makenika wa vyombo vya ardhini, majini na angani. Tunastaajabu kila wakati akina Grace Hooper, Charles Babbage, Ada Lovelace, Steve Jobs, Bill Gates (aliyehai hadi sasa) nk.; walivyokuna vichwa katika ugunduzi wa kompyuta na simu za mkononi.

Tumkumbuke Albert Einstein aliyegundua ukweli muhimu sana katika atomi na molekuli na kutuletea kanuni muhimu ya E = mc2. Fikiria aliyekuna kichwa chake na kugundua dizeli na petroli. Mnaoishi sehemu za joto kaali, fikiria waliokuna vichwa vyao na kugundua jokofu na kiyoyozi. Fikiria tunavyofaidika na waliogundua madawa mbalimbali, ya asilia na ya kisasa, pamoja na vifaatiba. Orodha ni ndefu sana!

Nasi tukune vichwa kwa kuwa hakuna ukomo wa ugunduzi madhali Mungu alituumba kufikiri. Kamwe tusijidharau maana inasadikika kuwa kuna mambo mengi sana hayajagunduliwa, ikiwa pamoja na jinsi ya kutibu mwili bila kunywa vidonge au kudungwa sindano. Unatibu tu kwa kutamka maneno yanayomfanya mtu apone. Kwa taarifa tu, zaidi ya asilimia 70 ya tiba bora ya mwili ni maneno yenye faraja, si vidonge wala sindano!

Tunasema haiwezekani. Ni sawa, lakini mbona pia tunasema haiwezekani kutembea kwa miguu juu ya maji? Tayari kuna mtu alishatembea juu ya maji zaidi ya miaka 2000 iliyopita! Tusikate tamaa, tuendelee kukuna vichwa kisha tutagundua jinsi ya kutembea juu ya maji, na kwahiyo tutaacha kujenga madaraja au kuvuka kwa mitumbwi.

Bila mawazo au fikra hakuna maendeleo, hakuna mabadiliko, na hapawezi kuwepo mafanikio yoyote yale popote pale. Nihitimishe kwa kusema kila unapotaka kufanya jambo lolote, tulia, tafakari kwa makini, yapime vizuri mawazo yako ndiposa ufanye maamuzi. Usikurupuke!


Filed under: JAMII Tagged: fikra, mafanikio, martin luther king, mawazo, nelson mandela

Viewing all articles
Browse latest Browse all 854

Trending Articles