Wakati hali ya wasiwasi ikizidi kuendelea kwenye wilaya za Kilwa, Mkuranga, Kibiti na Rufiji, ambako mauaji ya kunyemelea yameshaangamiza maisha ya watu wapatao 30, wakiwemo wenyeviti 20 wa serikali za vijiji na mitaa, Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe, ametoa wito wa kutumwa kwa Kamati ya Usalama ya Bunge kuchunguza mauaji hayo.
Akiandika kwenye ukurasa wake wa Facebook hivi leo, mbunge huyo ambaye pia ni kiongozi mkuu wa chama cha ACT-Wazalendo, amesema sasa “ni wakati mwafaka kwa Kamati ya Bunge ya Usalama iende MKIRU (Mkuranga, Kibiti na Rufiji) kuonana na wananchi na askari pia.”
Zitto amesema hayo, baada ya kusoma mfululizo wa makala za kile kinachojiri kwenye wilaya hizo kupitia vyombo binafsi vya habari, hasa magazeti ya Mwananchi na The Citizen, ambayo ameyapongeza kwa “kufanya kazi nzuri ya uchunguzi” na kutoka na taarifa za kina ambazo huwezi kuzipata “kutoka taarifa rasmi za serikali.”
Miongoni mwa taarifa hizo ni ile aliyosema ilichapishwa na gazeti la Mwananchi ikilitaja “jeshi la polisi linaua raia wasio na hatia akiwemo kijana Sultani Mpingi ambaye alikutwa anafua nguo nyumbani kwao na kukamatwa na kuteswa mpaka kufa. Baba yake aitwaye Mussa Mpingi aliikuta maiti ya mwanae huko Muhimbili. Hii ni Habari ya kustusha mno na chombo pekee cha kufuatilia na kuchukua hatua ni Bunge.”
“Kuna haja kubwa sana Bunge kutoa taarifa maalumu kuhusu eneo la MKIRU”, ameongeza Mbunge Zitto.
Filed under: HABARI Tagged: Kibiti, mkuranga, rufiji, zitto kabwe
