Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, leo amekutana na mkuu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Mchungaji Josephat Gwajima, katika kile walichokielezea kuwa kikao cha kuujadili mgogoro wa kiuongozi ndani ya CUF.
Baada ya mazungumzo yao yaliyochukuwa masaa yapatayo matatu, viongozi hao walizungumza na waandishi wa habari, ambapo Mchungaji Gwajima alisema amefurahi kupata nafasi ya “kukijuwa kinachoendelea ndani ya CUF kwa sasa” na kwamba atatafakari kile ambacho anaweza kusaidia.
“Nilikuwa nasikia tu kuwa kuna mambo yanaendelea ndani ya CUF, nikasikia Profesa Lipumba (mwenyekiti wa zamani wa chama hicho) anafanya hivi mara vile. Lakini sasa nimesikia kutoka kwa rafiki yangu (Maalim Seif),” amesema Mchungaji Gwajima.
Kwa upande wake, Maalim Seif alisema kuwa wamekaa na Mchungaji Gwajima na kila mmoja kumuelezea mwenzake anachokielewa na “sasa Mchungaji Gwajima atapata muda wa ku-digest (kufikiria) na kuona anachoweza kukifanya.”
Tangu mwaka jana, CUF imekumbwa na mzozo mkubwa wa kiuongozi baada ya mwenyekiti aliyejiuzulu wadhifa wake karibuni na uchaguzi mkuu wa 2015, Profesa Ibrahim Lipumba, kuamua kujirejesha kwenye nafasi hiyo kwa njia ambazo CUF inasema ni kinyume na sheria na katiba ya Chama chao, lakini akiwa anaungwa mkono na Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, na vyombo vya dola.
Filed under: HABARI Tagged: cuf, Gwajima, Lipumba, maalim seif
