Quantcast
Channel: Zanzibar Daima – Zanzibar Daima
Viewing all 854 articles
Browse latest View live

Lissu wa dhahabu

$
0
0

Mkononi mwangu nina kitabu kiitwacho ‘A Golden Opportunity? Justice & Respect in Mining’ (Fursa ya Dhahabu? Haki na Heshima kwenye Madini) cha mwaka 2008. Waandishi wake ni wawili – Mark Curtis na Tundu Lissu.

Ni matokeo ya utafiti uliofanywa na wawili hao wakiwa chini ya Baraza la Wakristo Tanzania (CCT) na Baraza la Waislamu Tanzania (BAKWATA) na uchapishaji wake kufadhiliwa na Shirika la Misaada la Kikristo la Norway.

Ndani ya kitabu hiki, namuona Lissu mpambanaji na mtaalamu akipigania rasilimali za nchi yake kwenye eneo la madini, akitetea haki za wananchi wanyonge wa kawaida, na akiipa changamoto serikali pamoja na wawekezaji kuacha ukatili, dhuluma na unyanyasaji dhidi ya wakaazi wanaozunguka au waishio katika maeneo zilipo rasilimali hizo za madini.

Simuoni Lissu msaliti wala Lissu mkurupukaji wala Lissu mpinga maendeleo kama, kwa bahati mbaya sana, wanavyotaka kutuaminisha maadui zake. Bali ndani yake, namuona Lissu mzalendo aliyetulia, mwenye maarifa na uwelewa wa anachokisimamia na anayeiona Tanzania inayopaswa kuwa na haki na usawa na neema na maendeleo.

Na Mohammed Ghassani

Naacha ripoti hii hata sijaimaliza kufika kwenye mapendekezo, nageukia mitandao ya kijamii – Facebook, Instagram, Twitter, Facebook, YouTube na blogu za Tanzania. Mote nakutana na sura na habari kuhusu Lissu. Asilimia 99 ni maelezo, ufafanuzi, ushuhuda na maombi ya kumtakia apone haraka.

Namo humo simuoni Lissu aliyetengwa na watu, bali namuona Lissu aliyezungukwa na umma unaompenda na kumuhusudu. Hata wale ambao kisiasa ni mahasimu wake, nawaona japo hivyo kwenye maandishi ya mitandaoni, wakisimama naye. Wanamtakia afya ya haraka. Wanalaani janga alilokutanishwa nalo – risasi zaidi ya tano mwilini kati ya risasi zikaribiazo 40 alizorushiwa.

Nafungua televisheni za kimataifa – CNN, Al Jazeera, BBC, ABC. Nasoma magazeti ya kimataifa pia kuanzia majirani zetu wa Afrika Mashariki hadi Amerika na Ulaya. Hali ni sawa kwenye redio za ndani na za kimataifa. Habari ni Lissu.

Sifikirii kuwa hao watu waliopachikwa jina la ‘wasiojuilikana’ na au waliowatuma walifahamu awali namna ambavyo mashambulizi haya ya aibu yangeliweza kumyanyua zaidi mtu ambaye tangu hapo alishanyanyuka juu katika medani za mapambano ya haki, sheria na demokrasia.

Kiwango cha risasi zilizotumika, hapana shaka, kilikusudiwa hasa kiumalize uhai wa Lissu papo hapo na kuizika hadithi nzima ya mwanaharakati huyu mwenye kipawa cha ajabu. Lakini ukweli ni kuwa, hata kama zingefanikiwa kuyakatisha maisha yake siku ile (Mungu apishe mbali), basi zingeshindwa – kama ambavyo zimeshashindwa sasa – kumlaza chini Lissu.

Matokeo ya ‘upuuzi’ huu uliotendwa na yeyote aliyeutenda ni kuwa kile walichotaka kukizamisha, ndicho sasa wamekiibua. Kwa mfano, hadi risasi zinamiminwa kwenye gari la Lissu mnamo Alhamis ya tarehe 7 Septemba, wengi wetu – mimi nikiwa mmoja wao – hatukuwa tumesoma kazi za Lissu alizozifanya kabla ya kuingia kwenye ubunge.

Ni baada ya jaribio hili la kuuondoa uhai wake, ndipo tukaanza kusaka na kuchakuwa makabrasha ya kutaka kumfahamu zaidi Lissu anayepigania roho yake kwenye chumba cha wagonjwa mahututi, Nairobi. Ndipo hapo tunakutana na maandiko kadhaa yanayoelezea alama alizowacha mwahala mote alimokanyaga shujaa huyu. Mojawapo ni hiki kitabu cha Golden Opportunity.

Wengine kwa kuona kuwa Lissu anawatoka mbele ya macho yao, wakageukia kuperuzi mtandao wa YouTube kumuangalia na kumsikiliza tena na tena yale ambayo aliyasema kipindi cha huko nyuma na hata cha karibuni zaidi.

Ukweli ni kuwa Google imepata sana matangazo ya bidhaa za wateja wake kupitia vidio za Lissu ndani ya kipindi hiki cha juma moja kuliko wakati mwengine wowote huko nyuma.

Mwandishi mmoja wa kujitegemea anayeendesha chaneli yake mwenyewe ya YouTube tangu mwaka 2014, ameniambia kuwa kwa mara ya kwanza alifikisha watazamaji 100,000 kwa vidio moja ndani ya masaa matano, baada ya kuweka vidio ya Lissu siku ya tarehe 8 Septemba, siku moja baada ya mashambulizi.

Binafsi nilikutana na Lissu kwa mara ya kwanza mwaka 2006 katika Hoteli ya Peacock jijini Dar es Salaam, ambapo vuguvugu la Katiba Mpya lilikuwa limeanza kupitia muungano wa vyama vya CUF, TLP, CHADEMA na NCCR-Mageuzi. Siku hiyo, Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, alikuwa anazindua vuguvugu la kudai katiba mpya, na miongoni mwa waliohudhuria alikuwa ni yeye, Lissu.

Nakumbuka kuwa mchango wake siku hiyo uliwavutia wengi, hasa kwenye suala la Muungano na nafasi ya Zanzibar. Msimamo ulikuwa – na mara kadhaa baada ya hapo amekuwa akiurejea – kwamba Tanganyika inautumia Muungano kuikalia Zanzibar bila ridhaa ya Wazanzibari.

Ushauri wake ulikuwa lazima Wazanzibari wadai mabadiliko ya katiba ili kuubadilisha muundo wa Muungano kutoka ukaliwaji wa sasa na kuwa ushirikiano wa heshima baina ya majirani wawili wenye udugu wa damu na kihistoria. Nikiwa muumini wa Uzanzibari, nilimuamini hapo hapo, maana alikuwa anakisema kile ambacho nimekuwa nikikiamini siku nyingi.

Mara nyengine ilikuwa mwaka 2014 kisiwani Pemba, baada ya kuvunjika kwa Bunge Maalum la Katiba. Vuguvugu la Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) wakati huo lilikuwa kwenye upya wake. Viongozi wa UKAWA walikuwa kisiwani Pemba kama sehemu ya kampeni yao kuwahamasisha wananchi kupinga kuandikiwa katiba mpya isiyokuwa na matakwa yao, mimi nilikuwa huko kwa mapumziko.

Kwa mara nyengine, alipewa jukumu la kuuzungumzia Muungano wa Tanzania, naye kwa mara nyengine akauita jina lake halisi – ukaliaji. Kwenye mkutano huo uliofanyika viwanja vya Gombani Kongwe, niliwashuhudia wazee wa Kipemba wakilia machozi kwa namna Lissu alivyokuwa akiwachoma kwa maneno yake.

Baada ya mara hizo mbili, mara nyengine kadhaa nimewasiliana naye kwa njia ya simu kikazi, nikimuomba kufanya mahojiano naye au kuwa mshiriki wa vipindi ninavyoandaa redioni. Na mote, ni nadra sana kunikatalia, labda awe na dharura kubwa sana.

Katika mazingira hayo yote niliyobahatika kukaribiana naye, Lissu aliniondolea shaka juu ya uwezo, uweledi na uzalendo wake. Alikuwa akikisema anachokiamini na kukisimamia. Na huyu ndiye Lissu anayejiuguza sasa, baada ya wabaya wake kutaka kuutoa uhai wake!

Kule visiwani Zanzibar wakati wa utawala wa Dk. Salmin Amour Juma aliyekuwa akijiita Kamando, wapinzani walikuwa wakimtania: “N’lidhani kamando wa chuma, kumbe kamando wa udongo. Tutamtoa ikulu, tukampeleke Kidombo!” Walikuwa wakikusudia kumdogosha Rais Salmin.

Lakini hata kwa maadui wa Lissu, sasa wanajuwa kuwa huyu sio tu ni wa chuma asiyevunjika, bali pia ni wa dhahabu asiyeshushika hadhi yake.

Kwa umadhubuti aliosimama nao kabla ya risasi za Alhamis, kwa mahaba aliyomiminiwa na umma wa Watanzania baada ya risasi hizo, na kwa dhamira aliyoisimamia maishani mwake mote, yote haya, yanamfanya mwanasheria, mwanasiasa na mwanaharakati huyu kuwa wa dhahabu.

Na hivyo ndivyo atakavyobakia ama awe hai au amekufa – Lissu wa dhahabu!

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHALISI la tarehe 18 Septemba 2017.


Filed under: KALAMU YA GHASSANI Tagged: CHADEMA, demokrasia, golden opportunity, haki, madini, Tanzania, Tundu Lissu

Nguvu ya Lissu ni kubwa kuliko ya risasi

$
0
0

Sisi wengine tangu siku ya mwanzo akina Nape Nnauye walipokuwa wakitetea uamuzi wa serikali ya awamu ya tano kuzuia matangazo ya moja kwa moja ya bunge kupitia televisheni ya taifa kwa madai ya kubana matumizi, tulijuwa wameshachelewa.

Si katika zama hizi za mawasiliano ya mitandao ya kijamii, ambapo nguvu hasa za mawasiliano zimo viganjani mwa watu! Kwamba huu si wakati tena wa kuwapangia watu cha kusikia, kuona, kusoma na kusikiliza, hata kama una sheria kali kama ya Uhalifu wa Mitandaoni iliyokimbizwa mbio mbio kupitishwa bungeni na utawala wa awamu ya nne wa Jakaya Kikwete kuuwahi uchaguzi wa 2015! Huwezi.

Wengine tulishasema kuwa ukilizima ‘Bunge Live’ kupitia televisheni ya TBC, utakuja kukumbana na ‘Bunge la Wananchi’ kupitia televisheni nyingi zaidi za mitandaoni. Ki vipi? Likawa ndilo swali.

Nimetaja neno ‘nguvu’ hapo juu na hapa nitalifafanuwa. Watu wenye nguvu – na sio wenye maguvu – huwa wana mambo matatu yanayofanana. Kwanza, huwa wako wazi, hawajifichi na sio wale watu wasiojulikana; pili, huwa hawafi hata wakiuliwa na hubaki milele na, tatu, wanawafanya wengine kunena ama kutenda kwa niaba yao, wawepo ama wasiwepo. Na hao ni pamoja  na hata maadui zao.

Na Mohammed Ghassani

Sababu ni kuwa maana ya nguvu halisi ni ushawishi. Ule uwezo wa kumuathiri mtu nafsini na akilini mwake. Akawaza kama utakavyo wewe awaze na, hatimaye, akatenda kama utakavyo wewe atende – ama kinyume chake. Wanafalsafa husema: “Niwazavyo ndivyo nilivyo!”

Wakati naandika makala hii, bado mbunge wa Singida Mashariki na Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika, Tundu Lissu, anaendelea kupigania maisha yake kwenye chumba cha wagonjwa mahututi jijini Nairobi, Kenya – umbali wa kilomita 682, mwendo wa masaa 10 na dakika 16 kwa gari itembeayo kilomita 112 kwa saa kutoka mjini Dodoma, Tanzania, alikoshambuliwa Alhamis ya tarehe 7 Septemba.

Lissu yuko mbali kwelikweli kifizikia na kidhahania, maana hata huko Nairobi aliko, nako ananing’inia baina ya uhai na umauti. Lakini kiuhalisia, mwanasiasa na mwanaharakati huyu yupo ndani ya ardhi ya Tanzania, nchi anayoipigania ambayo kwayo akamwagwa damu yake.

Mwangwi wa sauti yake unaakisika kwenye miji yote mikubwa na midogo, vyombo vyote vya habari vilivyo rasmi na visivyo rasmi, vikao vilivyo rasmi na visivyo rasmi vya wanasiasa, wanaharakati, na raia wa kawaida. Mote ni Lissu, Lissu, Lissu!

Nguvu ya Lissu ni kubwa kuliko inavyotazamwa

Ndio ujuwe namna msomi huyu wa sheria alivyo na nguvu za kweli. Hana mabavu ya kulazimisha watu kusema na kutenda, lakini ana ushawishi wa kuwafanya wengine wamuone shujaa wao. Bali hata kwa maadui zake, nguvu yake inawafanya waitikie mdundo wa ngoma inayopigwa naye.

Maana yake ni kusema kuwa kumbe zile risasi zaidi ya 32 alizomiminiwa nyumbani kwake Dodoma, hazikuweza kuzivunja nguvu za Lissu, bali kinyume chake ni kuwa zimeziongeza mno kufikia umbali wa kuwapatia Watanzania kile kitu adimu ambacho walikuwa wanakililia tangu utawala wa awamu ya tano uanze. Matangazo ya moja kwa moja ya bunge – ‘Bunge Live’.

Ukisikia namna ambavyo uongozi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, hasa kupitia Spika Job Ndugai, unavyojitahidi kupapatua na kujibizana na wabunge wa upinzani kuhusu kadhia hii ya Lissu, unaweza kukiona ninachokusudia hapa.

Kwanza alianza Mbunge Saeed Kubenea wa Ubungo, ambaye alizungumza kwenye ibada ya Jumapili ya Kanisa la Uzima na Ufufuo la Mchungaji Josephat Gwajima, akitaja mkasa mzima wa tukio la kushambuliwa Lissu na kutaja idadi tafauti ya risasi na zile alizozitaja Spika Ndugai hapo kabla. Matangazo ya ibada hiyo yalikuwa yakirushwa moja kwa moja na mitandao ya YouTube na Facebook.

Muda mchache, Spika Ndugai akaamuru Kubenea aitwe mbele za Kamati ya Maadili na Usalama za Bunge kuhojiwa eti kwa kukikashifu kiti kuwa kimesema uongo kwenye tukio la kushambuliwa Lissu.

Kisha akaja Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, ambaye vidio yake ilisambaa pia mitandaoni akiwa Nairobi anakomuuguza Lissu akimkosoa Spika Ndugai kwa kutumia muda mwingi kupambana na Kubenea badala ya kushughulika na hali ya Lissu aliye kitandani.

Siku ya pili asubuhi, Spika Ndugai akasimama tena bungeni kutumia kiti cha uspika kumjibu Lema, akienda mbali zaidi ‘kusumbulia’ kuwa serikali na wabunge wa Chama chake cha Mapinduzi (CCM) ndio waliochangia kumsafirisha Lissu hadi Nairobi.

Dakika chache tu baada ya Spika Ndugai kuyasema hayo akiwa kwenye kiti cha enzi cha uspika makao makuu ya nchi, Dodoma, Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, anapanda hewani kupitia ukurasa wa Facebook na mtandao wa YouTube akimsuta Ndugai juu ya anachokisema.

Mchana wake, Mbunge wa Mpendae, Salim Turki, ambaye ndiye aliyetajwa na Spika Ndugai kuwa alilipia ndege ya kumpeleka Lissu jijini Nairobi kwa matibabu, akakanusha kuwa hakulipa, isipokuwa alidhamini na kwamba malipo yalifanywa na CHADEMA yenyewe. Vidio yake ikasambazwa mitandaoni – Facebook na YouTube.

Kufikia jioni, ofisi ya bunge ikaonekana kusalimu amri kwa kutoa taarifa ya kimaandishi kuweka sawa kauli ya Spika Ndugai juu ya utata huo wa malipo ya ndege ya Lissu. Tena nayo ikasambazwa kupitia ukurasa wa Facebook.

Kwa hivyo, unapouangalia huu mtiririko wa mawasiliano ya moja kwa moja (mubashara) kati ya wabunge wa upinzani na kiti cha spika ndani ya kipindi hiki cha kushambuliwa Lissu, unapata picha kwamba kumbe bunge lilikuwa ‘live’.

Kwamba kumbe Lissu akiwa kitandani jijini Nairobi amelifanya bunge la Tanzania liruke moja kwa moja kupitia mitandao ya kijamii. Kubenea anasema kanisani, YouTube inarusha; Ndugai anaipata Dodoma, anajibu kwenye kiti cha spika.

Lema anaingilia kati kupitia Facebook na YouTube akiwa Nairobi hospitali; Spika Ndugai anarudi tena kitini pake kujibu.

Msigwa anayaona majibu ya Spika hayafai, anashuka tena kwenye YouTube na Facebook; Ofisi ya Bunge inatoa waraka wa kimaandishi inausambaza mitandaoni kuweka mambo sawa.

Yote hayo, mote humo, kila kitu tunakipata mubashara, bila chenga, moja kwa moja kutoka Nairobi na Dodoma. Hata tunaoishi maelfu ya maili kutoka Dodoma, tunajuwa mapigo ya moyo ya bunge yanadundaje. Tunaweza kusoma kupitia uso wa Spika Ndugai, ile fadhaa iliyolikumba bunge  na, hapana shaka, nchi nzima kwa sababu ya mtu mmoja tu – Tundu Lissu.

Hivi ndivyo nguvu hasa inavyofanya kazi. Ndipo unapojuwa kuwa, kama ilivyosemwa awali, kumbe pana tafauti baina ya kuwa na nguvu na kutumia mabavu. Wakati waliotaka kumuua Lissu walitumia mabavu kuizima nguvu yake, yeye anatumia nguvu yake kuyazima mabavu yao.

Walidhani kwamba kama jaribio la tarehe 7 Septemba lingefanikiwa, hivi sasa Lissu angelikuwa ameshalala pima sita chini ya ardhi. Wamemzima na kumnyamazisha. Kama alivyosema mwenyewe: “Tutanyamaza tukiwa makaburini mwetu!”

Lakini uhalisia wa nguvu umenena vyengine. Sio tu kwamba risasi hazikuweza hapo hapo kuondoka na roho yake, bali pia akiwa anapigania uhai wake huko Nairobi aliko, Lissu amekuwa kama kwamba yumo ndani ya viunga vya – kama si kwenye ukumbi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano – Dodoma.

Hakuna siku ilipita bila kutajwa. Hakuna gazeti limewahi kuchapishwa bila habari yake ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja. Hakuna televisheni wala redio imewahi kumaliza matangazo yake bila kuonesha picha yake. Hakuna mtandao wa kijamii hata mmoja – iwe Facebook, Twitter, YouTube, Instagram ama hata makundi ya WhatsApp – unaweza kupitisha siku bila Lissu kuwamo ndani yake.

Katika uzima wake na katika ugonjwa wake, nguvu za Lissu ni kubwa mno kuweza kuzuilika kwa mabavu yoyote yawayo. Ndiyo thamani ya kuwa upande wa ukweli. Unakuwa huzami chini. Wakupendao watakuhusudu, wakuchukiao watakuhishimu!

Ndio maana hata akiwa katikati ya uhai na umauti, Lissu amesimama imara na kuwapatia Watanzania kile wakitakacho. Ukweli na ujasiri na uthubutu.

Baadhi ya wakati, kheri yaweza kuzaliwa kutoka matumboni mwa shari na hakuna kipindi ambacho hayo yamedhihirika wazi kuliko juma hili moja tangu Lissu apigwe risasi!

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa mara ya kwanza na gazeti la Mwelekeo la tarehe 19 Septemba 2017 chini ya kichwa cha habari “Lissu katupa Bunge Live”.


Filed under: KALAMU YA GHASSANI Tagged: bunge, CCM, CHADEMA, Kubenea, Lema, Lissu, msigwa, Ndugai

Si nchi istahiliyo kuongozwa kihuni

$
0
0

NILIPOMSIKIA Mohamed Aboud Mohamed, mwanasiasa ndani ya CCM anayeitwa waziri katika serikali anayoiongoza Dk. Ali Mohamed Shein, akitaka Jeshi la Polisi Tanzania kuwa makini na baadhi ya viongozi wa siasa wanaotumia mwamvuli wa siasa au dini kinyume na taratibu kutaka kuharibu amani na utulivu, kwa kweli nilijua kitakachofuata.

Huyu waziri katika serikali iliyojiweka madarakani, alifanya ziara kwenye vyombo vya ulinzi na usalama mjini Zanzibar. Ziara yenyewe ilinijenga imani kuwa inapalilia jambo kubwa na zito, na litadhihirika muda si mrefu.

Mohamed Aboud ambaye wanaompamba wanamuita Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais, akiwa ofisi za makao makuu ya Jeshi la Polisi Zanzibar, akasema kwa kuwa nchi imetulia sasa, mambo yanakwenda vizuri, na vyombo vya ulinzi na usalama vinafanya kazi zake vizuri, wadhibitiwe watu wachache wenye nia mbaya na nchi na dhamira mbovu kwa maslahi yao binafsi wanaokusudia kuharibu amani na utulivu kwa ujanja wanaoufanya.

Na Jabir Idrissa

Kwa hivyo, anataka jeshi hilo kutilia maanani hali hiyo kwa kuizungumza mara kwa mara ili kuwahi kudhibiti tatizo kabla halijawa kubwa. Akasema jambo la msingi ni lazima watu hao wajulikane na wapelekwe kwenye vyombo vya sheria ili sheria ichukuwe mkondo wake.

Nikarudi nyuma kidogo. Wiki mbili hivi, baada tu ya wahalifu kumshambulia kwa nia ya kutaka kumtoa roho Tundu Anthipas Lissu, Mbunge wa Singida Mashariki, Mnadhimu Mkuu wa Upinzani Bungeni, Mwanasheria Mkuu wa Chadema na Rais wa Wanasheria Tanganyika, mwanasiasa asiyefanana kwa mengi na Mohamed Aboud naye alisema makubwa.

Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi au The Civic United Front (CUF), Maalim Seif Shariff Hamad akionesha hisia kali dhidi ya shambulio lililolengwa kumuua Lissu kwa risasi za moto, alimtaka Rais John Magufuli kuitisha kikao cha dharura kujadili hali mbaya ya usalama katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Maalim Seif alisema tukio alilotendewa Lissu limemshtua na kumfadhaisha na kufikia hatua ya kuamini usalama wa raia na mali zao umo kwenye mtihani mkubwa; na kuwa ipo haja kwake Rais kuitisha kikao cha dharura kitakachojumuisha viongozi wa kisiasa na wa kidini kujadili mustakbali wa taifa kipindi hiki.

Hawa wawili ni wanasiasa. Maalim Seif ni mwanasiasa wa enzi na aliyebobea. Amesomea hasa sayansi ya siasa na kuikhitimu kwa daraja la juu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam tangu miaka ya mwanzo ya 1970. Mohamed Aboud naye mwanasiasa, ila mchanga au wa kuja. Baada ya kufanya biashara kwa muda fulani, aliamua kuingia katika siasa ilipokaribia miaka ya 1990.

Maneno yake ni ya fitna. Yale ya Maalim Seif yanasihi kiongozi mkuu katika jamhuri si tu kutafakari, bali kuchukua hatua ya dharura. Huyu gwiji ameona kushambuliwa mbunge na wakili maarufu nchini, kunaashiria kuvunjwa kwa misingi ya amani na utawala wa kidemokrasia nchini. Hoja nzito kiuongozi na kimaono.

Hujaelewa sio? Angalia tukio la kushambuliwa Lissu lilivyoiteka dunia, achilia mbali Tanzania. Hujaona namna vyama vya mawakili Marekani (ALA), Afrika Kusini (SAL), Kenya (KLS), Zanzibar (ZLS), Uganda (ULS), Uingereza na Wales vilivyoibana serikali ya Rais Magufuli kutaka uchunguzi makini ufanywe kubaini wahusika wa kutaka kumuua Lissu na wakipatikana washitakiwe na ushahidi imara kutolewa mahakamani? Na katika muktadha huohuo, wametaka Marekani kama taifa na Umoja wa Ulaya (EU).

Maalim Seif, kama walivyopata picha mawakili wa mataifa hayo, amegundua kuwa utawala umeingia doa na uzito wake unampita hata kiongozi mwenyewe. Panahitajika mjadala mpana kuidhibiti hali iliyokwishavurugika. Anayaona matukio mabaya yanayozidi kuiharibu sifa ya jamhuri, ya kuitwa kisiwa cha amani na utulivu.

Maalim Seif, tofauti na Mohamed Aboud ambaye anaendekeza fitna ya kisiasa kwa kuwa yu miongoni mwa walaji nchi kwa ushindi uliotokana na kupindua maamuzi ya haki ya wananchi waliyoyafanya tarehe 25 Oktoba 2015, anajua kasi ya uharibifu wa amani isipoangaliwa, taifa laweza kusambaratika.

Maalim Seif ndiye anayeshika uongozi wa kupigania kurudishwa kwa haki ya wananchi iliyonyongwa kutokana na tamko haramu la Jecha Salim Jecha la tarehe 28 Oktoba 2015 ambalo alilitoa mafichoni, nje na mbali kabisa na majukumu yake kama mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC).

Jecha, kada mashuhuri CCM, katika siku hiyo, alikimbia makamishna wenzake waliokuwa na kazi muhimu ya kuuchunga mustakbali wa Zanzibar, na kutumika kutimiza matakwa ya mabwana zake CCM waliokuwa wameangushwa chini na wananchi kupitia sanduku la kura. CCM walikuwa wameshindwa kura halali.

Sasa wakati kosa hilo halijasahihishwa itakiwavyo, na Zanzibar yenye historia refu na iliyo hazina maishani, ikiwa na utulivu wa juujuu kwa vile umma mkubwa unaamini umedhulumiwa na haki yao ingali imeshikwa na hao madhalimu, anatokea Mohamed Aboud na maneno ya kutaka Polisi ikaze kamba katika kuwabana wananchi wanaotaka haki yao ya kikatiba.

Ni kwa sababu anajua vifua vya viongozi wa CCM na shingo zao vinazidi kuandamwa na dhambi ya dhuluma, anaingia, akibeba utumwa wa wakubwa zake wanaoumia naye pamoja, anashinikiza Polisi waumize wadaihaki.

Wanachokitaka kwa maneno aliyoyatoa na yakanukuliwa na vyombo vya habari vingi, ni Polisi kukamata viongozi wa CUF, chama kilichojijenga kuwa nguzo madhubuti ya kubeba matakwa ya Wazanzibari walio wengi Unguja na Pemba, na walioko ughaibuni, mpaka yatakapothibitishwa yameingia kwenye mikono salama.

Mohamed Aboud katu kwa maneno yake yale hakulenga kuiambia Polisi iwashike wapuuzi wanaobeba silaha za moto na za jadi na kupita mitaani wakishambulia wananchi katika maeneo ngome ya upinzani. Asilani abadani.

Mwanasiasa wa kuja huyu ambaye ndo katika wale wasiowakilisha hasa maslahi ya Wazanzibari wa asili ya Pemba, ingawa mwenyewe anatokea, anakula raha, anashiba yeye na familia yake, bali anahofia nguvu ya kudai haki ya wananchi inaongezeka na kama vile inahatarisha maslahi yao binafsi.

Yeye kama kweli anastahili kutambuliwa ni waziri msaidizi mkuu wa makamo wa pili wa rais, mbona hajasikika akiiambia Polisi tangu ikiwa chini ya Hamdani Omar kwamba iwadhibiti askari wa vikosi vya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar wanaohujumu wananchi kila wakati mitaani usiku na mchana? Hajapata kusema na hawezi kusema hayo.

Sasa usiku wa siku ya pili baada ya maneno yake kwa Polisi, hao wanaoitwa askari wa vikosi vya SMZ ambao wananchi wamewapachika jina la “mazombi” waliingia mitaani kama kawaida yao, na kushambulia wananchi kwenye barza zao kuanzia magharibi. Udhalimu ulioje unaotendwa na kupaliliwa na viongozi wa CCM?

Naam, ni udhalimu tu. Unapoona askari wamebeba bunduki za moto na marungu ya miti na mapande ya nondo, na kushambulia raia huku serikali ikichekelea – hakika inachekelea kwa sababu siku zote wahalifu hao wamebaki kuwa ni watu wasiodhibitiwa kama vile watu wasiojulikana – ujue utawala umekuwa asi na kwa kujua haukubaliki kwa wananchi, hauna isipokuwa kutumia staili ya ufashisti kuendeleza madaraka.

Leo matukio ya mashambulizi dhidi ya raia yanayozidi kushuhudiwa, yameshalaza watu kadhaa hospitali, baadhi wakiwa wamevunjwa miguu na mikono. Hapo damu imemwagwa kipuuzi tu. Ni ili kufurahisha wakubwa. Sasa utasemaje nchi inaongozwa kwa sheria na wanaoongoza wanahishimu katiba na sheria? Zanzibar ni nchi ya watu wema, sio madhalimu, na kwa hivyo haiwezi kudumu kuendelea kuongozwa kihuni na wahuni. Hapana.


Filed under: NDIO NASEMA Tagged: sheria, SMZ, Tundu Lissu, Umoja wa Ulaya, usalama, Zanzibar. haki

Kama vile Dk. King, hata kifo kisingemuua Lissu

$
0
0

Nimefuatilia kwa makini mazungumzo yanayoendelea katika mitandao ya kijamii, magazeti ya nchini pamoja na vyombo vyenginevyo vyenye kutoa taarifa tangu siku ya tarehe 7 Septemba mwaka huu, baada ya Mbunge wa Singida Mashariki na Rais wa Chama cha Wanasheria cha Tanganyika (TLS), Tundu Antipas Lissu, kupigwa risasi nje ya nyumba yake mjini Dodoma.

Kitendo hicho cha Lissu kupigwa risasi mchana kweupe, ndicho kilichoibua hisia kali za Watanzania. Hata kwa ambao kabla ya tukio hilo hawakuwa hata wakimtaja Lissu, baada ya kitendo hicho ndio wamekuwa wafuatiliaji wakubwa wa kutaka kujua Lissu ni nani, anafanya nini na kwa nini yakamkuta hayo yaliyomkuta.

Kwa wingi wa risasi zilizomiminwa katika shambulio hilo na kwa jumla ya risasi tano zilizothibitishwa kuzama mwilini mwa Lissu kwa mujibu madaktari wa Tanzania, kwa mtu mwepesi mwepesi aliye na wingi wa hofu na uchache wa ujasiri, hakukuwa na sababu ya kubakia hata kwa kutapia roho, bali angekufa kwa ule mlio wa risasi moja tu baada ya kufyatuliwa kutoka bunduki za hao wanaoitwa ‘Watu wasiojulikana’.

Na Ali Mohammed

Lakini kwa Lissu haikuwa hivyo. Alijihami kwa kufuata maelekezo ya dereva wake na hatimaye akatoka mzima ingawa si salama.

Sitaki niungane na watu wengine wanaotoa hukumu juu ya tukio hilo, lakini kwa hali inavyokwenda nchini tangu Lissu apigwe risasi mpaka leo, hakuna siku ipitayo kama Lissu hajatajwa. Wengi wao humtaja Lissu kutumia nafasi yake katika ulingo wa mapambano ya siasa.

Umaarufu wa Lissu baada ya kushambuliwa

Wengine hutumia kumtaja kupitia taaluma na ubobezi wake katika fani yake ya sheria na wengine humtaja na kumuita ni mtetezi wa haki za wanyonge wakihusisha mifano mbali mbali baada ya kusoma maandiko mbali mbali yanayoelezea kwamba kumbe mbali na yote hayo, Lissu pia ni mtetezi wa raia wote wa Tanzania kwa kupitia sekta ya madini.

Yote haya yamekuja mara tu baada ya Lissu kumiminiwa risasi. Kwamba baada ya tukio hilo, sio kwamba watu walisikitika kidogo na baadaye yakesha, lakini walisikitika na kisha wakataka kujuwa kwa nini Lissu apigwe risasi. Licha ya upelelezi wa kipolisi tunaoaminishwa kuwa unaendelea hadi leo bila ya taarifa za kina za matokeo na maendeleo ya upelelezi huo, lakini raia nao wanatumia nafasi zao kutaka kumjua Lissu kutoka utandu hadi ukoko. Hapo ndipo mambo mengi yanayomuhusu Lissu yakaenea kwa kasi kubwa sana katika jamii ya Tanzania.

Miongoni mwa hayo, ni kile kitabu chake kitabu kiitwacho ‘A Golden Opportunity? Justice & Respect in Mining’ cha mwaka 2008, alichoandika kwa ushirikiano na Mark Curtis. Kitabu hichi kinaonesha jinsi Tundu Lissu aliye mahututi kitandani hospitalini huko Nairobi, akiuguzwa na kutibiwa majeraha ya risasi za bunduki ya SMG, anavyoinuka na kusimama barabara na kupambana kitaalamu kupigania wananchi wa Tanzania juu ya suala zima la madini.

Huyo ndiye Lissu aliyejitoa muhanga, licha ya vitisho alivyovipata mara kadhaa kutoka kwa watu wasiojulikana na wanaojulikana si kwa maslahi binafsi yake binafsi, bali ni kwa kutetea haki za wananchi wanyonge wa kawaida, sambamba changamoto kedekede alizoipa serikali pamoja na wawekezaji wa madini kuacha ukatili, dhuluma na unyanyasaji dhidi ya wakaazi wanaozunguka au waishio katika maeneo zilipo rasilimali hizo za madini.

Je, kifo kingelizika jina la Lissu?

Kihistoria, duniani Lissu si mtu wa kwanza kuanzisha mapambano kuitetea na kuisimamia jamii yake katika kupata haki fulani au kulinda kitu fulani. Yako mataifa kadhaa yalikuwa na watu mfano wa Lissu. Kinyume chake pia, Lissu hatakuwa wa mwisho kwa Tanzania kujitolea kufanya hivyo. Watakuja wengi mfano wa Lissu na zaidi ya Lissu watakaosimama kuitetea Tanzania ndani na hadi nje yake.

Kama ninavyoamini mimi na wengine kwamba Lissu amejitoa kuitetea jamii ya Tanzani, pia duniani wapo wengi wamepita kuzitetea jamii zao. Wapo waliofanikiwa kuzipata haki walizokuwa wakizipigania wakiwa katika hali ya uzima bila hata kovu moja, licha ya madhila mengi waliyoyapata kutoka kwa wapinga haki hizo. Lakini pia wapo waliozipata haki hizo wakiwa walemavu, wagonjwa na waliodhoofika kutokana na madhila kama hayo ya kupigwa risasi na mateso mengineyo.

Na pia wako waliozikosa haki hizo kwa kuuwawa kikatili na wapinga haki waliokuwa wakipambana nao, lakini pamoja na kuuwawa kwao, bado harakati zao ziliendelea hadi kupatikana haki hizo walizokuwa wakizidai. Wengine hadi leo bado wanaendelea kupambana na kudai haki hizo huko huko makaburini walipo, mfano wa hao ni Dkt. Martin Luther King Jr. Huyu ni mfano wa wanaharakati waliokufa ambao hadi hii leo bado wako hai kupigania haki za jamii zao.

Sitaki nieleweke labda wamekufa kimazingara kama vile tuaminivyo kwamba watu hufa kwa kutolewa kikoa lakini wanatumika uchawini Bumbwini, Kwanyanya na Ukutini – Chambani Pemba. La hasha! Ninachokusudia ni kuwa ingawa bwana huyu na wengine mfano wake walipigwa risasi na kuuawa wakiwa katika mapambano ya kuzitetea jamii zao, fikra zao bado kila uchao zinaonekana kama zimetolewa leo, na jamii inatumia fikra zao kama ndio dira ya kuongozea mambo na nchi zao.

Ikumbukwe kwamba mwaka 2008 wakati wa kampeni za kugombania urais wa Marekani, taifa lililo kubwa zaidi duniani lakini likiwa pia na kiwango cha juu cha ubaguzi wa rangi dhidi ya weusi, waliingia katika historia mpya ya uongozi wa nchi hiyo ikiwa ni kwa kumuingiza rais mweusi madarakani, Barack Hussein Onyango Obama. Mtoto huyo wa raia wa Kenya alifanikiwa kwa kutumia kumbukumbu za harakati zile zile za Hayati Dk. King, ambapo hata katika baadhi ya majimbo ambayo Obama alihisi yana kiwango cha juu cha ubaguzi, alitumia msamiati wa ‘I have a Dream……..’ (Nina ndoto……), msamiati ambao ulitumiwa na Dk. King katika hutuba yake maarufu ya tarehe 28 Agosti 1963, miaka mitano kabla ya kupigwa risasi kadhaa katika taya na uti wa mgongo.

Basi kwa mfano huo wa wanaharakati waliouwawa kwa kutetea maslahi na haki za raia wa nchi zao, hususan Dk. Martin Luther King Jr, yatosha kuamini kwamba hata zile risasi zilizomiminwa kutoka kwenye bunduki aina ya SMG mbele ya ‘kadamnasi’, mchana kweupe, na baadaye moja kwa moja zikaingia katika tumbo, mguu, kiuno na bega la Lissu, sambamba na Watanzania wanyvyomzungumza baada ya tukio lile kuanzia siku ile hadi leo, nashawashika kuamini kwamba hata kama risasi zile zingempeleka kwenye umauti, bado Lissu angaeendelea kuzungumzwa, kutajwa, kupendwa na hata kuheshimiwa na Watanzania wanaoheshimu na kufahamu maana na malengo ya harakati za kusimamia na kuetea haki na maslahi ya raia. Kwa hivyo, hata kifo kisingelilizika jina la Lissu.


Filed under: SAUTI Tagged: Lissu, martin luther king

Mayatima na wajane wa kisiasa hadi lini Zanzibar?

$
0
0

Ali Juma Suleiman alivamiwa na kikosi kikubwa cha watu usiku wa tarehe 26 Septemba mwaka huu nyumbani kwake Mtoni, Unguja.

Mke wake, Bi Rehema Nassor Juma, anasema alishuhudia askari wenye sare za vikosi vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) wakiwa na mitutu ya bunduki, marungu na mapanga.

Watoto wake wanasema askari hao walikuwa na magari matatu na kuzunguka eneo lote la nyumba yao na za majirani zao usiku huo ukaribiao saa sita.

Ali Juma alipigwa ndani ya nyumba yake, kisha akatiwa pingu kwa nyuma na kufungwa kitambaa cha macho, kabla ya kutupwa kwenye gari, ambalo mwenyewe aliwasikia watekaji wake wakizungumzia habari za Masingini.

Masingini ni eneo lisilo mbali sana na kitovu cha mji mkuu wa Zanzibar, upande wa magharibi muelekeo wa kaskazini mashariki. Huko kuna msitu mkubwa.

Na Mohammed Ghassani

Aliposhushwa hapo, alipigwa na watekaji wake kwa vyuma na vitu vyenye ncha kali, ambavyo vilimpasua misuli ya miguu yote miwili, miongoni mwa majeraha na maumivu mengine mengi.

Watekaji hao walikuwa wakimpiga huku wakimuambia wanamtia adabu kwa kuwa anataka “kuipindua serikali”. Walimshushia kipigo kwa muda mrefu mpaka waliporidhika kuwa kwa namna alivyo, basi asingeliinuka tena.

Walihakikisha amepoteza damu nyingi sana na kwa mahala walipomuwacha – katikati ya msitu na usiku huo mkubwa – waliamini asingeliweza kupata msaada wowote hadi tone lake la mwisho la damu lingekauka mwilini na huo ukawa mwisho wake.

Lakini kumbe siku yake ya kuondoka duniani, Allah hakuwa ameiandika iwe Jumanne hiyo, wala malaika wa mauti hakuwa ametumwa kuitwaa roho ya Ali Juma katikati ya msitu wa Masingini.

Badala yake, Mungu alimpa nguvu za kujikongoja hadi kijiji cha karibu na msitu huo, ambako baada ya jitihada kubwa na kwanza kukataliwa msaada na wenyeji yumkini kwa woga wao, wakatokea vijana wawili kumsaidia. Ni hao walioiwezesha hadithi ya Ali Juma kuja juu, ikasimuliwa na kusikika duniani kote.

Masaa 48 baadaye, usiku wa Alhamis kuamkia Ijumaa, Ali Juma alihitajiwa kwa Mola wake akiwa Hospitali Kuu Mnazi Mmoja. Wino ukakauka na daftari la uhai wake likawa limefungwa hapo. Innalillahi wainna ilayhir raajiun!

Hata hivyo, kitabu cha hadithi ya Ali Juma kwetu walimwengu hakikufungwa hadi pale mwenyewe alipopata fursa ya kuandika sehemu ya mwisho ya riwaya yake.

Akiwa kitandani hospitalini siku ya Jumatano, aliweza kuyasimulia masaibu yote yaliyomkumba ndani ya kipindi cha masaa 24 yaliyopita. Neno kwa neno. Tukio kwa tukio. Kama vile mkanda wa sinema, shahidi huyu alipata upumzi wa kuelezea kila kitu. Hadi saa na dakika.

Na yote aliyoyasema yakaja baadaye kuthibitishwa na watu waliomzunguka na walioshuhudia sehemu ya mwanzo na ya mwisho ya jaala yake – yaani pale alipochukuliwa na yaliyojiri wakati huo na baada ya kupatikana na kilichotokea kwenye hatua za awali za matibabu. Ya katikati yake, hapana shaka, wanayo waliomkamata na kumtesa kwenye msitu wa Masingini na Mungu wao.

Hii haikuwa mara ya kwanza kwa Ali Juma kufuatwa nyumbani kwake na watu hawa hawa wanaoaminika kuwa wanatoka vikosi vya SMZ wakisaidiwa na vyombo vyengine vya dola. Ndio maana hata alipowaona waliokuja mara hii wakiwa na mitutu na namna walivyojipanga, aliwaambia mkewe na wanawe: “Buriani. Safari hii sirudi salama!”

Mke wake, Bi Rehema, anasema hii ilikuwa mara ya nne kufuatwa na kupigwa mumewe. Hana imani kabisa na serikali, kwani anaamini ndiyo inayohusika moja kwa moja na mauaji ya mumewe. “Hakuna raia mwenye bunduki, wala bastola, wala pingu. Ni hao hao. Walikuwa wamevaa sare za vikosi vya serikali. Dhuluma kubwa imepita. Mume wangu kadhulumiwa!”

Kauli ya kudhulumiwa inatolewa pia na Seif Ali, mtoto wa Marehemu Ali Juma, ambaye anasema hana shaka na hilo, ingawa haongezi kitu zaidi ya kumuombea mzazi wake asamehewe makosa yake na Mungu amuweke peponi!

Lisilo shaka ni kuwa Ali Juma hakufa kifo cha kawaida. Aliuawa. Na sababu ya kuuawa ni msimamo wake wa kisiasa. Nje ya nyumba yake, huyu alikuwa mwanasiasa wa upinzani, akiwa mwanachama na muanzilishi wa Chama cha Wananchi (CUF) tangu kilipoasisiwa mwaka 1992.

Nusu nzima ya umri wake wa miaka 50, Ali Juma aliitumia akikitumikia chama chake hicho kwenye ngazi mbalimbali, kuanzia za chini kabisa huko matawini hadi juu kabisa kwenye vikao vya kitaifa. Umri wake umekatishwa wakati akiwa mkurugenzi wa habari na uenezi wa chama chake katika Wilaya ya Magharibi ‘A’.

Hadithi ya Ali Juma ni moja tu kati ya hadithi nyingi za aina hii tangu Zanzibar irudi tena kwenye mfumo wa vyama vingi. Bahati mbaya ni kuwa hadithi zote za aina hii zinasimuliwa kutoka upande mmoja wa kisiasa – upinzani.

Kama kuna kitu ambacho uongozi wa CUF ni mahodari kwacho, basi ni uwezo wake wa kuwajengea wanachama wake uvumilivu wa kuachiwa mayatima, vizuka na vilema. Yalianza na Shumba ya Mjini, Micheweni, ambako siku bendera inapandishwa mlingotini kwa mara ya kwanza wilayani humo mwaka 1992, iliondoka na roho ya mwanachama wao, mwenye jina kama hili la Ali Juma.

Kuanzia hapo, ikawa mitutu ya dola ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeshaonja damu ya wana-CUF na haiwezi tena kuiacha. Ndani ya nusu karne hii ya vyama vingi, idadi ya maiti zilizozikwa kwa jina la siasa upande wa CUF zinapindukia 100, waliowekwa vilema ni maelfu na waliowachwa vizuka na mayatima hawana idadi.

Takribani kila familia ya mwana-CUF ina mtu wake ambaye amekuwa muhanga wa vyombo rasmi na visivyo rasmi vya dola. Kama inakosa aliyeuawa moja kwa moja, itakuwa na aliyejeruhiwa. Kama imekosa majeruhi, itakuwa na aliyefukuzwa kazi, kuvunjiwa nyumba au kukoseshwa fursa za kimaisha na kimasomo kwa sababu ya msimamo wao wa kisiasa.

Juu ya yote, kuna malaki ya wengine wanaotembea na majeraha ya rohoni mwao – hayaonekani, lakini yapo ndani kabisa ya miili yao na yanauma kila uchao. Majeraha, majonzi na machozi ndiyo gharama halisi inayolipwa na wale wenye maoni tafauti ya kisiasa na watawala visiwani Zanzibar.

Na katikati ya makovu haya, CUF imejaaliwa kuwa na uongozi ambao unaamini kwenye subira na busara. Unaamini kwenye kuwapa matumaini wanachama na wafuasi wake kuwa haya yote ni mambo ya kupita. Kwamba Zanzibar haitajengwa kwa siasa za kutoana macho na kung’oana meno, bali za Maridhiano na Umoja wa Kitaifa.

Bahati mbaya ni kuwa kadiri uongozi huo unavyojikita kwenye kutaka kuitakasa mikono yao isije ikachirizika damu za Wazanzibari, ndivyo wapinzani wao, ambao ndio watawala, wanavyoona fursa ya kuwasukuma ukutani zaidi na zaidi, hadi sasa wameshawachupisha upande mwengine kabisa, ambako hawawezi kujitetea wala kushambulia.

Swali kubwa ambalo kifo hiki cha karibuni kabisa, miongoni mwa roho nyengine nyingi zilizolazimishwa kuhama kabla ya wakati, kinatuachia ni ikiwa hadi lini Zanzibar itaendelea kuangamiza watu wake na kuwaacha watoto mayatima na wake vizuka? Hadi lini siasa zetu zitaendelea na kusinzwa kwa damu ya watu wetu?

 

 

 

 

 


Filed under: KALAMU YA GHASSANI

Yasemavyo magazeti ya Tanzania leo Oktoba 23, 2017

Hali ya hewa muruwa jijini Dar es Salaam

$
0
0

Baada ya miezi kadhaa ya vumbi na joto kali, hali ya hewa imeimarika suala ambalo limepelekea kiwango cha maradhi kupunguwa. Awali wakaazi wengi waliathiriwa na hali hio likiwemo ibuko la maradhi kama vifuwa, mapunye na ukurutu. wakiongea na Zaima TV, wengi wameonesha kufurahi hali hii.


Filed under: MULTIMEDIA

Balozi Seif kuzindua meli maalum ya utafutaji mafuta na gesi asilia Zanzibar

$
0
0

 

Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi kesho Oktoba 27, 2017 anatarajiwa kuzindua meli maalum kutoka nchini China ambayo itafanya utafiti wa Mafuta na Gesi Asilia katika miamba ya visiwa vya Unguja na Pemba.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Makaazi, Nishati na Mazingira Zanzibar, Ali Halil amesema meli hiyo baada ya kuzinduliwa inatarajiwa kuanza kazi rasmi katika kisiwa cha Pemba eneo la Wete na baadae kuendelea katika maeneo mengine ya Zanzibar.

Amesema meli hiyo inatarajiwa kufanya kazi hiyo kwa kipindi cha mwezi mmoja hadi miwili na itatembea katika maeneo maalum kwa kuangalia miamba ambayo uchunguzi wa rasilimali hizo za mafuta na gesi utakakofanyika kwa kipindi hicho.

Kwa mujibu wa taarifa ya Idara ya habari Maelezo Zanzibar ilitolewa na Naibu Mkurugenzi wa Idara hiyo, Dk Juma Mohamed Juma juu ufafanuzi juu ya zoezi hilo alisema kuwa Meli hiyo ya MV. BGP Explorer yenye urefu wa mita 64 na upana wa mita 13.8 inahusika na zoezi la Mitetemo katika bahari.

Alisema kuwa mbali ya meli hiyo pia kutakuwa na meli nyengine ambazo zitaungana nayo katika zoezi zina la utafutaji wa rasilimali ya mafuta na gesi visiwani humu.

Dk Juma alisema kuwa miongoni mwa meli hizo ni meli ya utafiti ya Fellowship yenye urefu wa mita 39.86 na upana wa mita 9.0 ambayo itakuwa na jukumu la ulinzi wakati wa zoezi la Seismic “Mitetemo” litakapofanyika.

Hiyo ni awamu ya pili ya muendelezo wa kazi ya Utafutaji wa Mafuta na Gesi Asilia baadaya kukamilika zoezi la Utafutaji katika mwezi Februari, 2017 kazi hiyo ya kukagua miamba iliyoko chini ya ardhi ambapo kwa kitaalamu kazi hii inajulikana “Airborne Full Tensor Gravity Gradiometry Survey” (FTG).


Filed under: HABARI

Wizara ya elimu Zanzibar yataja idadi ya wanafunzi waliopata mikopo ya elimu ya juu

$
0
0

Jumla ya Wanafunzi 1,600 wanatarajiwa kupatiwa mikopo  ya masomo kwa ngazi za shahada ya kwanza, shahada ya pili  pamoja na shahada ya tatu kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kupitia Bodi ya Mikopo ya Elimu ya juu Zanzibar.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Riziki Pembe Juma akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo Oktoba 26, 2017 huko ofini kwake Mazizini nje kidogo ya  Mjini wa Zanzibar, alisema kuwa idadi ya wanafunzi hao imepatikana kwa mujibu wa bajeti ya Serikali ya Zanizibar kwa mwaka 2017-2018.

Alisema kuwa katika awamu ya kwanza ya utoaji wa mikopo hiyo   jumla ya waombaji 1,021 kati fomu za maombi 2,675 zilizotolewa katika vituo vya Unguja na Pemba, kwa ngazi mbali mbali za elimu ya juu tayari wameshateuliwa kwa ajili ya kupatiwa mikopo hiyo.

Aidha ameongeza kuwa kati ya wanafunzi hao walioteuliwa awamu ya kwanza kupatiwa mikopo hiyo wanafunzi wa Shahada ya kwanza (Bachelor Degree) wapo 983, Shahada ya Uzamili (Master Degree) 34 pamoja wa Shahada ya Uzamivu (Doctor of Philosophy – PHD) wanafunzi 4 tu.

Alisema kuwa jumla ya shillingi milioni 64,000 zinatarajiwa kutumika kwa ajili ya kulipia gharama za masomo kwa wanafunzi hao waliopata ufadhili kutoka Serikali ya Zanzibar katika masomo yao ndani ya vyuo vikuu vya Tanzania.

Amefafanua kuwa gharama hizo zinajumuisha malipo ya ada ya masomo, mitihani, posho la kujikimu, posho la vitabu, posho la mafunzo ya vitendo pamoja na mahitaji maalum ya vitivo vyao.

Waziri Pembe alisema kuwa kuwa uteuzi huo umefanywa kwa mujibu wa vigezo mbali mbali pamoja na vipaumbele vilivyowekwa na Serikali ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi waliofanya vizuri zaidi kutoka 50 hadi kufiki 88 kwa mwaka 2017.

Hata hivyo metoa wito kwa wale waombaji ambao hawakuteuliwa kwa awamu ya kwanza wawe na subira kwani Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Zanzibar inaendelea na awamu nyengine za uteuzi ambapo teuzi za majina ya waombaji wa mikopo zitafanywa kwa kadiri ambavyo Kamisheni ya Vyuo Vikuu ya SMT (Tanzania Commision for Univversities – TCU) itakapotangaza majina mapya ya wanafunzi watakaopatiwa udahili katika vyuo vikuu na taasisi nyengine za elimu ya juu hapa nchini.


Filed under: HABARI

Zanzibar yakabidhiwa vifaa maalum vya kugundua watumiaji wa dawa za kulevya

$
0
0

Wagonjwa wanaotumia dawa aina ya ‘Methadone’ kama tiba baada ya kuathirika na dawa za kulevya na wanaoutumia aina nyengine ya dawa  kwa njia za siri wamepatiwa muarubaini baada ya kupatikana vifaa maalum vya kumgundua mtumiaji huyo kwa kupimwa mkojo .

Vifaa hivyo vinavyojulikana kwa jina la ‘DOAKIT’ vimetolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa la kupambana na madawa ya kulevya na uhalifu (UNODC).

Mratibu wa Mradi wa Taifa wa kupambana na HIV/AIDS kwa wafungwa, Immaculate Nyoni ambae ni afisa wa UNODC Tanzania amemkabidhi vifaa hivyo Mratibu wa huduma za ukimwi kwa watu wa makundi maalum Zanzibar, Dk Shaaban Hassan katika hafla iliyofanyika Kliniki ya Methadone iliopo Hospitali ya wagonjwa wa akili Kidongo- chekundu Mjini hapa.

Nyoni alisema UNODC itaendelea kuunga mkono juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuwapatia tiba sahihi wagonjwa walioathirika na dawa za kulevya ili kuona kunapatikana wanajamii wazuri.

Alisema katika uungaji mkono wao huo wameanzia kwa kuleta vifaa hivyo vya DOAKIT 1500 ambavyo vinaweza kutumika kwa kipindi cha miezi mitatu kwa mujibu wa idadi ya wagonjwa wanaotumia Methadone waliosajiliwa katika kliniki hiyo.

Daktari dhamana wa Hospitali hiyo ya Kidogochekundu, Dk Khamis Othman alilishukuru shirika la UNODC kwa kuwapatia msaada huo ambao kwa kipindi cha mwaka mmoja walikuwa na upungufu mkubwa na kupelekea baadhi ya wagonjwa kutumia aina nyengine ya dawa bila kujulikana.

Alisema kwa mujibu wa taratibu za kutumia tiba ya Methadone mgonjwa hatakiwi kutumia aina nyengine ya dawa za kulevya na akifanya hivyo hupata madhara makubwa kwa kuongeza kiwango cha dawa mwilini.

Alisema DOAKIT ni vifaa vyenye uwezo wa kugundua aina sita ya dawa za kulevya kwa kuchunguza mkojo wa mtumiaji na vinaweza kutumika katika maeneo mbali mbali kuwachunguza watumiaji wa dawa hizo.

Dk Othman aliesema kuwa Kliniki ya Methadone ya Kidongochekundu ilianzishwa mwaka 2015 na imesajili wagonjwa 434 ambao wanapatiwa  tiba kamili na imekuwa mkombozi wa vijana wengi waliokubali kujiunga.

Alisema kazi ya Methadone ni kusaidia kuondosha hamu ya kutumia Heroine na dawa nyengine za kulevya hatimae mtumiaji huacha kidogo kidogo kutumia dawa hizo.

Hata hivyo amekiri kuwa bado wanakabiliwa na changamoto kubwa akisema kuwa baadhi ya wagonjwa wanaotumia Methadone hukosekana baadhi ya siku kufika kituni kwao kutokana na kufuata dawa  za kulevya kwa siri.

Msaada wa vifaa hivyo uliotolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa la kupambana na madawa ya kulevya na uhalifu (UNODC) vimegharimu shilling milion 17 za kitanzania.


Filed under: HABARI

Kampuni ya Huawei mbioni kuutambulisha mpango wake wa utoaji elimu kwa njia ya Tehama

$
0
0

Kampuni ya Huawei, yenye makao yake makuu mjini Shenzhen nchini China, inatarajia kuutambulisha mpango wake wa utoaji elimu kwa njia ya Tehama, unaojulikana kwa jina la E-education.

Hayo yalibainishwa mapema wiki hii na maofisa kuytoka kampuni hiyo wakati wa ziara ya waandishi wa habari nchini China waliotembelea kujionea namna mradi ‘Smart education’ wanaoutekeleza katika shule ya msingi Baogang nchini China na kuwa wa mafanikio.

Meneja Mahusiano wa kampuni hiyo, Schloss glenn James, alisema kuwa kuanzishwa kwa mradi kama huo wa elimu kwa njia ya teknolojia ya Tehama kwa shule za msingi na sekondari itasaidia kuinua kiwango cha elimu nchini kama ilivyothibitika katika mradi ulioanzishwa katika shule ya msingi Baogang.

James alisema Huawei kwa sasa wamejikita zaidi katika miradi ya mifumo ya elimu kwa mtandao ambapo kupitia mradi huu, matarajio ni kuboresha kiwango cha elimu kwa kiwango cha juu kupitia teknolojia ya Tehama kwa ajili ya kufundishia na kusoma.

Kwa mazingira hayo, Huawei wamekuwa wakihamisha ujuzi wao kwenda kwa watumishi mbalimbali nchini kwa kuwatumia wataalamu waliobebea ndani ya Huawei.

Meneja huyo alisema katika kutekeleza jukumu hilo, Huawei ikiwa na watumishi 120, wamekuwa wakitoa mafunzo na elimu kwa vitendo kwa wanafuzni wa fani ya Tehama.

Sambamba na hayo, mkakati wa kampuni hiyo ya Huawei, ni kupanua wigo wao katika uboreshaji wa miundombinu ya ICT kwa lengo la kuiunganisha nchi ya Tanzania.

Alifafanua kwamba ajenda ya kampuni hiyo ni kuhakikisha wanaendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi wa kiwango cha kimataifa katika kuyafikia mageuzi ya kweli katika nyanja mbalimbali kupitia utaalamu wa teknolojia ya tehama.

Baadhi ya waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari Tanzania, wakiwa katika picha ya pamoja mjini Shenzhen, China, walipokwenda kutembelea makao makuu kampuni ya Huawei na kuijionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na kampuni hiyo ikwemo utekelezaji wa mradi wa elimu wa Smart Education

Kwa mwaka huu, Huawei wamekuwa katika mkakati kamambe wa kutafuta njia mbadala na bora zaidi za kuisaidia Serikali katika malengo yake yake ya kiuchumi ifikapo mwaka 2020/2025.

Huawei wamekuwa wakifanya hivyo kwa maslahi ya nchi katika kutimiza wajibu wao wa kuhakikisha vyanzo na njia mpya za kuharakisha maendeleo zinapatikana.


Filed under: MULTIMEDIA

Namna ya kulitayarisha wa shamba la miti

$
0
0

Kilimo ni sehemu muhimu ya maisha ya mwanaadamu, maana bila ya kula hataweza kuishi na hawezi kula kama hapajalimwa. Lakini ili kilimo kiwe endelevu na kuyafaidisha mwanaadamu, ni lazima pawe na uwiano kati ya shughuli za kilimo na za ulinzi wa mazingira.

Wawakilishi waijia juu serikali kesi ya Kiringo

$
0
0

Wajumbe kadhaa wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar hivi leo wameijia juu serikali, baada ya kupokea taarifa kwamba mshukiwa wa ubakaji watoto wadogo, Hassan Aboud Talib (Kiringo), aliyekamatwa jana kwa tuhuma za kumnajisi mtoto wa kiume wa miaka 13, ameachiwa huru licha ya uzito wa tuhuma dhidi yake.

‘Subalkheri Mpenzi’ yawaweka mashakani akina Aslay

$
0
0

Msanii wa kizazi kipya kutoka Tanzania Bara ambaye ameiimba tena nyimbo mashuhuri ya ‘Sabahalkher Mpenzi’ iliyoimbwa miaka ya zamani na Mwanapombe Hiyari na Marehemu Sami Haji Dau, amewasili Zanzibar kukutana na Bi Mwanapombe kuzungumzia hakimiliki za nyimbo hiyo.

Mbunge wa Malindi amlima barua Infantino wa FIFA

$
0
0

Mbunge wa jimbo la Malindi, mwandishi wa habari na mwanamichezo, Ally Saleh, amemuandikia barua ya wazi Rais wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), Gianni Infantino, siku chache kabla ya kiongozi huyo wa soka ulimwenguni kuwasili kwa ziara maalum nchini Tanzania. Kujuwa yaliyomo kwenye barua hiyo, soma hapa.

OPEN LETTER

Your Excellency Gianni Infantino
President
FIFA
Dar es salaam

Your Excellency Mr. President,

We are happy that you are currently putting your presence in our beautiful country and we would like to wish a FIFA Committee meeting in Zanzibar fruitful deliberations.

Just across Dar es salaam the Tanzania commercial city, there is The Zanzibar Archipelago where football is religion as sports in general is passion. Zanzibar has been making all the efforts to become FIFA member with no success. She has tried three times already.

Last December in high profile performance with special ambition to show the world, and few months after “the in and out” of Confederation of African Football (CAF), Zanzibar against all the odds reached the final of East African Challenge CUP (CECAFA) and smiles are still on our faces for the achievement. With huge potential Zanzibar has been the backbone of the Tanzania National Team without the chances of representing herself in FIFA run competitions but also the CAF competitions.

Zanzibar has been knocking the FIFA door since 2001 for the first time and the second in 2005 and has been rejected for reasons we do not believe warrant that rejection as we are able to demonstrate a lot of instances and situations where other territories have been welcomed into the world body.
Your Excellency Mr. President.

Zanzibar has tried to put her case before your honorable office to explain that sports in Tanzania is not an integral part of the Union arrangement that has been reached over half a century ago under The Articles of |Union, and thus each side of the Union has its own sporting arrangement including own Ministry, own individual sports sport bodies such as chess, basketball etc, as well as own football association.

Tanzania is consisted of two partners -Zanzibar on one side and Tanganyika on the other which took the name of Tanzania 1964 which legally is the UNION ITSELF. It is and has been a contradiction ever since.

We have been explaining that Tanzania Football Association (TFF) is not in actual fact a body fully and legally representing the Tanzania State, but rather TFF by its structure is only a body representing one side of the Union – legally known within our borders as Tanzania Mainland and formerly Tanganyika.

Probably from FIFA eyes and understanding it is not aware of this entity known as Tanzania Mainland, but it takes part in the East African Challenge Cup, a yearly tournament and where Zanzibar takes part on her own status – thus Tanzania sends two teams.

Your Excellency Mr. President

Under Union arrangement the Minister of Sports and Culture Dr. Harison Mwakyembe is not a Union Minister per se, and this because the name and status of Tanzania is invoked to represent the whole territory of Tanzania whilst the truth it only refers to the above term of Tanzania Mainland, probably you know it for the first time and is the gist of the whole problem in the Union. Zanzibar has her own Sports Minister.

Hence this is to say Zanzibar is not at all represented in the TFF. According to TFF Constitution its membership is drawn from regions making the land known as Tanzania Mailnad – only.

Furthermore, no Zanzibari is allowed to vie for any position in the TFF, again a true indication TFF is only for Tanzania Mainland and not the whole of Tanzania which will encompass Zanzibar.

Your Excellency Mr. President

Until today TFF conducts no single football business in Zanzibar. It runs a Tanzania Mainland League, runs no development programs in Zanzibar as well.

Zanzibar runs her own league with clubs representing the Islands in Africa Club competitions where Zanzibar is an invitee. It was accepted as 55th Member last year but the decision was rescinded few months later.

FIFA has refused Zanzibar application for want of statehood for the 1.4m entity whereas British Virgin Island, American Virgin Island, Pueto Rico, Macau, Hong Kong, Liechstein and others are not United Nations Members but are still FIFA Members.

If the condition of becoming a FIFA Member is to be a state and statehood is recognized by being a member of the United Nations, than how comes that United Nations has 193 members whilst FIFA has 213 members?

Zanzibar has a fully grown and blown administrative system including own Legislature, Presidency and Judiciary and not only conducts a full senior league but has youth programs named Juvenile, Junior and Central League as well as beach and women soccer leagues.

We believe we have a good case only that FIFA has not fully heard our case on merit. Under the current Union arrangement Zanzibar will never be represented by Tanzania for us to accept.

Ally Saleh
Member of Parliament
Malindi Constituency
Zanzibar
Email: allysaleh126@gmail.com
+255 777 430022 – + 255 715 430022
Twitter : @allysalehznz


FIFA haina hoja kuinyima Zanzibar uanachama – Alberto

$
0
0

Imeelezwa kuwa hoja ya Shirikisho la Soka la Ulimwengu (FIFA) kuwa haliwezi kuipa uwanachama Zanzibar kwa kuwa si mwanachama wa Umoja wa Mataifa haina mashiko kwa kuwa FIFA ina wanachama wengi zaidi kuliko wajumbe wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na hiyo ikimaanisha kuwa ndani ya FIFA muna nchi wanachama kadhaa ambazo si madola kamili kama ilivyo Zanzibar. Hayo ni kwa mujibu wa Mbunge wa Malindi, Ally Saleh (Alberto), amabye ni mdau mkubwa wa soka visiwani Zanzibar katika mazungumzo yake maalum na Zaima TV. Msikilize hapa.

 

 

 

 

Kubenea azidi kumng’ang’ania Mwigulu mauaji ya Akwilina

$
0
0

Mbunge wa Ubungo kwa tiketi ya CHADEMA, Saeed Kubenea, amemtaka kwa mara nyengine tena Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba (CCM), kujiuzulu nafasi yake akimtuhumu kuwa hawezi tena kuaminika kushikilia wadhifa huo baada ya mkururo wa matukio ya mauaji na uvunjwaji wa haki za binaadamu unaofanywa na vyombo vilivyo chini yake, likiwemo tukio la kuuawa kwa mwanafunzi wa Chuo cha Usafirishaji, Akwilina Akwilini.

 

 

CCM Zanzibar yalia na ‘viringo’

$
0
0

Chama cha Mapinduzi upande wa Zanzibar kimepaza sauti yake dhidi ya tabia inayoendelea kukuwa ya kuwaharibu watoto wadogo kikitaka sheria kali iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi isainiwe haraka na kuanza kufanya kazi.

 

La Prof. Kabudi, Zanzibar na Mtego wa Komba

$
0
0

KOMBA amepewa sifa nyingi za ujanja. Kwa wanaomjua wanampa sifa nyengine, nayo ni ya ujasiri. Anapotafuta anachokitaka, hachelei kuingia katika nyumba ya mtu na hata chumbani.  Pamoja na udogo wake, lakini komba anapokabiliwa na tishio kutoka kwa binadamu, atachukua miguu yake ya mbele na kuiweka kichwani, kisha atatembea kwa miguu miwili ya nyuma akiwa wima; na hapo, kwa asiye mweledi wa kumjua komba anaweza kukimbia akidhani amekutana na jinni au kiumbe wa ajabu. Naam, baba wa miraba minne anaweza kukimbizwa na komba huku akipiga kelele, pengine na suruali ikiwa ameshaiharibu.

PAMOJA na ujanja, mbinu na ujasiri lakini kitu kimoja kimemsaliti. Uchu wake wa kupenda ndizi mbivu. Komba kwa ndizi mbivu ndio maafa na mauti yake.  Binadamu baada ya kujua udhaifu huu wa komba hawapati shida. Ndizi mbivu huwekwa katika mtego wa komba na baadaye huachiwa yeye mwenyewe popote alipo aufuate na kujiangamiza mwenyewe.  Mtego wa komba ni kipakacha chembamba sana kinachotengenezwa kwa kuti la mnazi.

Chembamba kiasi kwamba hata yeye komba huingia kwa shida. Ndizi mbivu huwekwa mwisho kabisa wa kipakacha. Mlango wa kuingilia wa kipakacha huzungushwa kitanzi cha uzi madhubuti usiokatika na baadaye uzi huo hutumika kuifunga ndizi iliyoingizwa ndani ya mtego wa komba.

Nadhani kwa tabia yake, komba anapofika katika mtego, roho humtua akajua binadamu, kama kawaida yake mweledi wa kuficha, kaficha ndizi yake akijua komba haipati. Basi hapo, komba huyu hupenyeza kichwa taratibu akivuta kidogo ndizi akaanza kula. Kila ikipungua, anaivuta zaidi na zaidi na zaidi mpaka tumbo limejaa, mlo wa siku umetimia. Shida inaanza anapotaka kutoka katika kipakacha kile kwenda na safari zake. Anajikuta amekwama. Kuna kitu kimemnasa shingoni. Mwanzo anadhani ni nyuzi tu za kipakacha, lakini baadaye anaanza kutanabahi kuwa ni kitu kibaya zaidi; ni kitanzi na kimeshakaa shingoni kinaanza kumbana.

Na Othman Masoud Othman

Kinachomponza komba ni ukosefu wa nadhari. Badala ya kutulia angalau akabaki hai, anaanza kujinasua kwa pupa. Kila akijivuta, kila akitumia nguvu na kitanzi kinabana. Tahamaki roho imetoka.

Asubuhi, wale waliomtega wanapoenda kuangalia, hujisifu: “Aaah wa jana bwana…komba na ujanja wake, bwana ukimtaka, ndizi mbivu tu umemshika!“ Hawajali kama iliyotoka ni roho, tena wameitoa kwa sababu ya ndizi moja tu. Wanafurahi, wanasherehekea na wanajiandaa kutega komba mwengine…

Bila ya shaka, maafa ya Zanzibar hayafanani kwa asilimia mia moja na komba na mtego wa ndizi moja. Lakini kwa fikra zangu, ipo elimu kubwa katika hili la mtego wa komba kwa Zanzibar, kwa Wazanzibari na hata kwa watawala wa Zanzibar wa sasa hivi, Tanganyika alias Tanzania.

Mjadala na Wasifu wa Profesa Kabudi

Nimefuatilia mjadala juu ya kauli ya Mwalimu wangu, Profesa Palamagamba Kabudi, aliyoitoa Bungeni akiwa Waziri wa Sheria wa Serikali ya Tanzania. Miongoni mwa yanayolalamikiwa sana ni kauli yake juu ya hadhi ya Rais wa Zanzibar, hadhi ya Katiba ya Zanzibar na pia hadhi na mamlaka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Yamesemwa mengi, yamesemwa na wengi, si madhumuni yangu kuanza kuyarejea.

Wakati nasikiliza zile vidio za maelezo ya baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar pamoja na baadhi ya mawaziri walizozitoa katika Baraza la Wawakilishi kumjibu na hata kumlaani Profesa Kabudi, adhana ya laasir ikasomwa. Adhana ilinitanabahisha mambo mawili. Kwanza, kwamba wakati wa sala umefika. Lakini la pili ni ile busara iliyomo ndani ya adhana. Pamoja na kwamba sala ni amri ya Allah kwa waumini wa Kiislamu, lakini pia ni nguzo ya dini ya Kiislamu. Hata hivyo, waumini wanakumbushwa kila inapofika wakati wa sala. Falsafa ya kukumbusha ndiyo iliyonipelekea kuandika makala hii fupi.

Kwanza, napenda kutanabahisha wasifu wa Profesa Kabudi. Kwa kadri ninavyomuelewa ni mtu anayeufahamu vya kutosha mfumo wa sheria na katiba wa Zanzibar, historia yake na maendeleo yake. Anajua vionjo na viroja vya siasa za Zanzibar. Anajua hisia na mtazamo wa umma wa Zanzibar. Lakini anajua pia udhaifu wa waliopo katika nyadhifa mbalimbali Zanzibar kama anavyoujua umakini na umahiri wa baadhi ya watu wa Zanzibar. Ana faida ya kuijua Zanzibar tokea kwa babu zake. Hata jina lake la Palamagamba amelipata Pemba ambako babu yake aliwahi kufanya kazi ya fundi uashi.

Wengi wasiomjua Profesa Kabudi, wanadhani ni mwalimu tu wa Sheria wa Chuo Kikuu ambaye hatimaye ameteuliwa kuwa Waziri. Wanaomjua wanakumbuka kwamba wakati wa vita vya Kagera alikuwa Mwandishi Msaidizi wa Mwalimu Julius Nyerere, kazi yake ikiwa ni kushughulikia utaalamu wa kuandika taarifa za vita. Ni katika waliomshauri Mwalimu Nyerere kuwa taarifa zote za vita ziandikwe katika gazeti la Kiswahili la Serikali na waliobaki wanukuu kutoka katika gazeti hilo.

Weledi wa propaganda za vita na diplomasia wanajua kwamba hiyo sio mbinu ya kitoto bali ni ya weledi wa hali ya juu na inaonesha upeo wa waliotoa uamuzi huo.

Jengine ambalo binafsi nalifahamu kwa Profesa Kabudi ni kwamba msimamo wake binafsi ni kuwa Zanzibar inastahiki kukaliwa na Tanganyika [occupied] kwa maslahi mapana anayoyaita ya kimkakati. Bila ya shaka hiyo ni kasumba ya wengi wasioungalia Muungano kiuchumi na mwenendo wa sasa wa kidunia. Huo ni mtazamo sio wake peke yake, bali wa makada wengi waliopita katika darsa ya MWALIMU yule aliyekuwa akitumia mtaala wa miaka ya 60.

Mbali ya sifa za kitaaluma na kiutumishi, lakini hata kwa upande wa dini amepata fursa ya kulitumikia Kanisa la Anglikana katika nafasi nyeti ya Katibu akiwa na jukumu moja muhimu nalo ni la kuchunga taratibu za kiutawala na uongozi.  Kwa ufupi amekuwa mchungaji wa Katiba, sheria na taratibu za Kanisa hilo.

Uzoefu katika nafasi zote hizo ukichanganya na sifa yake kubwa nyengine ya kuwa mtu mwenye kumbukumbu ya kusifika [photographic memory] haziendani na kile kinachodhaniwa kuwa amesahau alichokisema miaka mitatu tu iliyopita.

Kwa wenye tafakuri na wakawa wanamjua vyema Profesa Kabudi watatanabahi tu kwamba yupo katika mchezo wa kuaminisha lile liliomo katika ajenda ya Tanganyika ambayo baadhi ya viongozi walioiingiza Zanzibar katika mtego wa komba wanajifanya hawaijui.  Wanaotaka tuamini kwamba siasa za Muungano ni siasa za itikadi za vyama na sio siasa za kimkakati wa mtawala na mtawaliwa.

Ni rahisi kuchakata kauli za Profesa Kabudi kuonesha kwamba uwaziri umemfanya kuwa mnafiki na mwenye kigeugeu.  Nadhani ni busara kuangalia kwamba huyu ni mtu ambaye amekuwa katika “establishment” katika takriban uhai wake wote wa kikazi na kitaaluma.  Kubwa zaidi ni kuangalia hatima ya ugeugeu wake au “unafiki” wake. Yote mawili yana faida kubwa kwa mwajiri wake na yanakoleza ajenda tuliyotangulia kuieleza ya mtawala na mtawaliwa.

Katika falsafa ya vita hakuna kigeugeu bali kuna kujipanga upya. Kama kugeuka kauli au mbinu yako ni njia ya kushinda vita itakuwaje kigeugeu hicho kiwe na ila??? Binafsi yangu sioni kama katika aliyoyasema Profesa Kabudi lipo jambo jipya ambalo viongozi wetu hawalifahamu kwamba hiyo ndio dhana ya Muungano waliyonayo wengi wa viongozi wa umma wa Tanganyika.

Itaendelea…

Wavumbuzi wa SUZA wafanya maajabu mengine

$
0
0

Wanafunzi wa Skuli ya Sekondari ya Chuo Kikuu cha Zanzibar (SUZA Secondary) wameibuka tena na ushindi kwenye jukwaa la kimataifa, baada ya kushinda tuzo ya biashara katika mashindano yafahamikayo kama School Enterprise Challenge yaliyozishirikisha nchi zaidi ya 100 ulimwenguni chini ya shirika la British Charity kupitia mradi wa Teach a Man to Fish.

 

 

 

 

Viewing all 854 articles
Browse latest View live