Quantcast
Channel: Zanzibar Daima – Zanzibar Daima
Viewing all 854 articles
Browse latest View live

Trump hudanganya mara 5 kwa siku

$
0
0

Rais Donald Trump wa Marekani ameshatoa madai ya uongo zaidi ya mara 1,000 tangu aingie Ikulu ya White House, linaripoti gazeti la Washington Post.

Madai hayo ni yanajumuisha kauli kadhaa kuwa Sheria ya Huduma Nafuu za Afya – maarufu kama Obamacare – iko kwenye hatua zake za mwisho na ile ambayo amekuwa akiirejea mara kwa mara kwamba alikuwa kiini cha kupuguzwa kwa bei ya ndege za kivita za F-35.

Staili ya uropokaji ya bilionea huyo na mkururo wake wa Twitter umemfanya aingie kwenye dimbwi la kauli zisizo za kweli mara 1,057 tangu aingie madarakani mwezi Januari mwaka huu, kwa mujibu wa timu ya utafiti ya Washington Post.

Hii inamaanisha kwamba anatoa taarifa zisizo sahihi mara tano kwa siku. Ameshayarejea madai zaidi ya 30 uongo angalau mara tatu.

Uongo wa kwanza unaotajwa ni ule maarufu siku ya kuapishwa aliposema umati uliohudhuria ulikuwa mkubwa kuliko ilivyowahi kutokezea kwa wengine akiwemo mtangulizi wake, Barack Obama. Uongo huu ameshaurejelea mara saba. Picha zilizochukuliwa kwenye mikusanyiko yote miwili zinaonesha ukweli tafauti.

Siku mbili tu baada ya kuingia madarakani, utawala wa Trump ukaanza kupata umashuhuri kwa kile ulichokiita “ukweli mbadala” ambao hadi leo inaendelea nao.


Filed under: BURUDANI Tagged: Donald Trump, Marekani

Serikali inapojibu mabomu ya Lissu kwa risasi za maji

$
0
0

Inaonekana mtazamo wa serikali ya Rais John Magufuli kumuelekea mwanasheria wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Tundu Lissu, unaanza kubadilika.

Kutoka kumkamatakamata kila akitoa kauli na kumweka ndani kisha kumfungulia mashitaka yasiyo kichwa wala miguu, sasa serikali imeamua kujibizana naye neno kwa neno, ‘bandika-bandua’ wasemavyo vijana wa mjini.

Sasa leo Lissu akisema jambo kuhusu serikali, ngojea kauli ya msemaji wa serikali hiyo kesho yake. Hii ni hatua nzuri sana, mara nyingi zaidi kuliko ule anaouita mwanamuziki Ibrahim Musa (Roma Mkatoliki) kama ‘uhuni wa kishamba.’

Uhuni wa kishamba ni pamoja na huu wa kukamatamata wanasiasa wa upinzani ovyo, kuwapiga, kuwatesa na kisha kuwafungulia mashitaka yasiyo mashiko alimradi tu kuwasumbua, kuwavunjia heshima na haki zao za kibinaadamu na kuwapotezea muda wao.

Kwa hivyo, ni jambo la kusifiwa kuwa serikali inaamua kuachana na tabia isiyo sahihi, angalau kwa kuanza na huyu mwanasheria anayetambuliwa kwa misimamo ya kimapinduzi, Lissu.

Na Mohammed Ghassani

Huenda tabia hii ikachukuliwa pia dhidi ya wengine wasiokuwa wanasheria, lakini ambao wanaamini kuikosoa serikali iliyopo madarakani kwa mijadala na midahalo ni njia bora zaidi kuliko kugeukia uasi wa silaha na matumizi ya nguvu.

Hata hivyo, inapoamua kutenda hivi, serikali bado inapaswa kujipanga. Isiwe inakurupuka kama kule kwenye huo uitwao ‘uhuni wa kishamba.’ Vyenginevyo, itakuwa inapata matokeo yale yale – ya kubwagwa kwa aibu na fadhaa.

Kwa aliyefuatilia mara mbili tatu ambazo ofisi ya msemaji maalum wa serikali imeamua kumjibu Lissu, atagundua kirahisi namna ofisi hiyo inavyotumia staili ile ile ya kukurupuka hadi sasa, na matokeo yake kuja na majibu mepesi kwa maswali mazito ambayo mnadhimu huyo wa kambi ya upinzani bungeni anayaibua.

Mfano wa karibuni kabisa ni huu wa majuzi, ambapo Lissu aliibua suala la kuzuiliwa kwa ndege aina ya Bombardier Q400-Dash 8 iliyonunuliwa na serikali ya Rais Magufuli nchini Canada kutokana na deni la dola milioni 37.8 (shilingi bilioni 87) ambalo serikali ya Tanzania inadaiwa kwa kuvunja kwake mkataba na kampuni moja ya ujenzi, Stirling Civil Engineering Ltd.

Kwa mujibu wa Lissu, kampuni hiyo ina hati ya mahakama inayoipa haki ya kuzuia mali za Tanzania sio tu nchini Canada, bali pia Uholanzi, Ufaransa, Ubelgiji, Uingereza na hata nchi jirani ya Uganda.

Kwenye mkutano wake na waandishi wa habari, Lissu aligusia pia taarifa ya kampuni ya uchimbaji madini ya Acacia Mining kuifungulia serikali ya Tanzania kesi kwenye mahakama ya usuluhishi ikidai pia mamilioni ya dola kwa kuzuiwa mchanga wake wa dhahabu, maarufu kama makinikia. Acacia wamefungua kesi hiyo hata kama bado mazungumzo baina ya pande hizo mbili yanaendelea.

Hicho ndicho cha msingi alichokibainisha Lissu kwenye mkutano wake na waandishi wa habari, ingawa kiliambatana na makandokando mengine kama vile kusema kuwa ukweli huo ulifichwa na serikali kwa kuwa ni matokeo ya tabia ya serikali hiyo kufanya mambo kwa kuripuaripua bila kufuata taratibu.

Sasa sikiliza majibu ya kaimu msemaji rasmi wa serikali, Zamaradi Kawawa, kwenye hili. Kwanza, kwamba ni kweli Bombardier-4000 imezuiliwa, lakini jitihada zinaendelea kuikwamua na kuifikisha Tanzania muda mfupi ujao.

Pili, kwamba kuzuiwa kwa ndege hiyo kunatokana na kampeni inayoendeshwa na wanasiasa wetu wasioitakia mema Tanzania.

Tatu, kwamba serikali ya Rais Magufuli haibaguwi kwenye maendeleo.

Nne, kwamba serikali hiyo inawafuatilia kwa karibu wanasiasa wanaokwamisha maendeleo kwani pia ni hatari kwa usalama wa taifa.

Wengi walioyasikia majibu haya walivunjwa moyo tangu sentensi ya kwanza kabisa kuanza kusomwa na kaimu msemaji huyo wa serikali. Sababu ni kuwa Lissu kwenye uwasilishaji wa ‘bomu’ lake alikuja na ushahidi mzito na wa moja kwa moja dhidi ya serikali.

Kwamba serikali ilikuwa imevunja mkataba wa ujenzi barabara mwaka 2009 na kampuni hiyo. Kwamba ikashitakiwa. Kwamba ikashindwa kesi. Kwamba ikakataa kulipa fidia. Kwamba ikakata rufaa. Kwamba ikashindwa rufaa. Ikaamuriwa kulipa tena. Ikakataa. Sasa ndege yake imekamatwa. Kwamba ni baada ya ndege kukamatwa kwa deni, ndipo Waziri wa Mambo ya Nje, Balozi Augustine Mahiga, akaenda nchini Canada kusaka njia ya kulimaliza hilo kimya kimya.

Yote haya hayajibiki kwa kusema kuwa ndege italipiwa na itafika nyumbani na Watanzania waendelee kuiamini serikali yao. Waiamini kwa msingi upi kwenye hili, wakati haikuwahi hata siku moja kusema kuwa ndege iliyotakiwa kufika mwezi mmoja nyuma haikufika kwa sababu gani? Na hata alipokuja mtu kutamka hadharani, sababu za kuchelewa kwake kufika, serikali inamrukia mtu huyo kuwa anakwamisha maendeleo?

Mambo matatu yanazuka sasa hapa, sio kwenye suala lenyewe la Bombardier tu, bali kwenye tabia yenyewe ya serikali kuyaendea maswala muhimu ya nchi. Kwanza, serikali hii inayojipambanua kwa kupambana kwake na ufisadi, wizi na ubadhirifu katika sekta ya umma, imeuficha udhaifu wake nyuma ya ukali wa kiongozi mkuu, Rais Magufuli.

Kwamba pale guo la ukali huo wa Rais Magufuli linapovuliwa, basi kinachodhihirika ni serikali isiyo viunganishi na muunganiko. Waliofuatilia suala hili hili, wanajuwa kuwa huko kwenye mitandao ya kijamii, Waziri wa Mawasiliano na Ujenzi Makame Mbarawa alishakanusha siku moja tu nyuma juu ya kushikiliwa kwa Bombardier. Huyu ni mjumbe wa baraza la mawaziri. Lakini siku moja baadaye, msemaji wa serikali anakiri kuwa ni kweli inashikiliwa. Hii inaonesha kuwa huko ndani, nje ya ukali wa Rais Magufuli, kuna vikuku vya mkufu wa mawasiliano ndani ya utawala vimekatika. Na huo ni udhaifu mkubwa.

Pili, miaka miwili baada ya kuingia madarakani, Rais Magufuli ameshindwa kupanga timu yake ya mkakati vyema. Bado utendaji wake na wa timu yake unakwendana na mapigo ya kinachoendelea mitandaoni na kwenye majukwaa ya kisiasa.

Mawasiliano baina ya serikali na umma yanajengwa na kipi kimeibuliwa na ‘waropokaji’ huku nje – mitandaoni, majukwaani, mitaani. Ujanja wa kuziwahi taarifa mapema ili kuchomeka wazo ambalo serikali inataka liwe wazo kuu kwa wananchi haumo ndani ya vichwa vya timu ya mkakati ya Rais Magufuli.

Tatu, na la mwisho, serikali inadanganya kwa jina la uzalendo. Kuanzia Rais Magufuli mwenyewe hadi wanaomfuata chini yake, kauli yao kubwa ya kukumbizia takataka chini ya zulia ni kwamba taifa letu linahitaji uzalendo wa hali ya juu, ambao kwa maoni yao ulikuwa umekosekana siku nyingi huko nyuma.

Wakati hilo ni sahihi kabisa, kisichokubalika ni kwa serikali hiyo hiyo kuficha ukweli au kudanganya kwa wananchi ili kujenga mapenzi yasiyo ya kweli kwa serikali yao.

Ingelikuwa vyema kabisa kile kinachohubiriwa na Rais Magufuli majukwaani, kwamba yeye ni msema kweli, kikawa ndicho kinachoakisika katika mtiririko mzima wa wanaomfuata chini yake. Na inapobainika kwamba kimakosa serikali ilidanganya au ilificha ukweli uliopaswa kufahamika na umma kwa wakati muafaka, basi iwe tayari kuomba radhi haraka na kwa ufanisi.

Mapenzi na uzalendo hujengwa juu ya ukweli na uwazi.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza kwenye gazeti la Mwelekeo la tarehe 22 Agosti 2017.


Filed under: KALAMU YA GHASSANI Tagged: jamhuri ya muungano wa tanzania, John Magufuli, mahakama, Tundu Lissu

Kitendawili cha Angola bila ya dos Santos

$
0
0

Na AHMED RAJAB

KWA muda mrefu tangu miaka ya mwisho ya 1960 nimekuwa nikizururazurura barani Afrrika nikinusanusa siasa au kusaka habari.

Nimezizuru nchi zilizokuwa na amani pamoja na zilizokumbwa na vita au mapigano ya wenyewe kwa wenyewe. Tangu miaka hiyo hadi leo ni mara mbili tu nilipoingia matatani.

Mara ya kwanza ilikuwa ni kwa kujitakia. Nilivunja amri ya Serikali ya Zambia iliyowazuia watu wasionekane barabarani kuanzia saa 12 za Magharibi hadi alfajiri. Kwa kuonekana barabarani saa 12 na sekunde 30 nilikamatwa pamoja na wenzangu watatu.

Wanajeshi waliokuwa na bunduki walituamrisha tuwafuate hadi kituo kikuu cha polisi mjini Lusaka. Huko walitutumbukiza ndani ya chumba cha mahabusu waliokuwa wamewekwa rumande.

Takriban wote wakikabiliwa na mashitaka ya jinai. Chumba kilikuwa cha giza na kilihanikiza harufu ya mchanganyiko wa mikojo, vinyesi, vikwapa na bangi.

Tulipojaribu kugoma kuingia ndani, wanajeshi walitwambia tushike adabu zetu au tutakabiliwa na mashtaka mazito zaidi.

Ilikuwa wakati wa utawala wa Rais Kenneth Kaunda, “KK” kwa umaarufu wake. Wiki kadhaa kabla mnamo Oktoba 1980 palifanywa jaribio la kumpindua. Ndio sababu ya ulinzi kuwa mkali Lusaka.

Mara ya pili kuingia matatani ilikuwa kwa kuonewa. Baada ya kuwasili uwanja wa ndege wa Luanda, Angola, na pasipoti yangu kupigwa muhuri wa kuingia nchini humo ghafla nilishikwa na watu wa usalama.

Waliipekua pasi yangu na wakaniuliza maswali yaliyokuwa na maana na mengine yasiyokuwa na maana.

Baada ya muda walinisukuma kwenye chumba walikokuwa wameshikwa watu walioshutumiwa kuingia nchini kinyume na sheria. Wengi wao walikuwa ni Waislamu kutoka nchi za Afrika ya Magharibi wenye kufanya biashara ndogondogo Angola.

Kama waliachiwa baadaye basi nina hakika wengi wao walifulizia mtaa wa Martires ulio karibu na hapo. Huko ndiko wanakoishi Waislamu wengi wanaotokea Afrika ya Magharibi.

Kireno hakizungumzwi sana mtaani humo. Huzungumzwa zaidi lugha za Afrika ya Magharibi za ki-Bambara, ki-Wolof au ki-Hausa. Kifaransa na Kiarabu pia huzungumzwa kwa sababu miongoni mwa wakazi wa huko ni wahamiaji kutoka Lebanon.

Na mtaani humo ndiko wanakobughudhiwa mara kwa mara wafanyabiashara wa Kiislamu. Wamebandikwa jina la “kinguila” kwa sababu ya kazi yao kubwa ya kuvunja sarafu za kigeni lakini polisi wanawashutumu kujihusisha na biashara za magendo.

Wengine wanasema kuwa wanaonewa tu kwa sababu ni Waislamu. Angola ina ubaguzi mkubwa dhidi ya Waislamu. Ndio maana pale uwanja wa ndege wengi waliokuwa wameshikiliwa walikuwa Waislamu.

Kilichonichongea mimi zaidi nadhani ilikuwa ziara niliyoifanya miaka michache kabla katika maeneo yaliyokuwa yakishikiliwa na waasi wa UNITA, waliokuwa wakiongozwa na Jonas Savimbi.

Bila ya shaka, watu wa usalama wa Angola wakijua kwamba niliwazuru wapiganaji wa UNITAa kutokana na mahojiano na ripoti zangu kwenye kipindi cha BBC cha “Focus on Africa”.

Bahati nzuri mwenyeji wangu alibishana na kuwabembeleza watu wa usalama na baada ya saa kadhaa, kupindukia usiku wa manane, waliniruhusu niingie mjini.

Jijini Luanda nilikutana na wanadamu wa aina mbalimbali. Nilikumbana pia na maneno mawili ya Kireno yaliyokuwa yakiniandama kila niendako.

Maneno yenyewe yalikuwa “confusao” na “situacao”. La mwanzo tunaweza kulitafsiri kama “mchafukoge.”

Wananchi wa Angola, hususan wale waliokuwa hawanufaiki na mfumo wa utawala, wakikielezea kila kitu kwa kusema “confusao”, mambo mkorogo mtupu, mchafukoge. Walikuwa hawajui wafanye nini kuepukana na “confusao” iliyokuwepo.

Mambo yalikuwa msegemnege; yakenda kama hayendi. “Confusao” ilikuwa ikiwakanganya au kuwachanganya. Hiyo ndiyo iliyokuwa “situacao”, hali halisi.

“Situacao” wakiweza kuimudu, kwa kufanya mbarange, mafamba na kila aina ya hila ili waweze kujikimu kimaisha.

Walikwishazoea kuwaona mawaziri na wakuu wa majeshi wakiishi maisha ya raha na anasa. Wao wakiishi maisha ya ufukara.

Fitina iliyoikoroga Angola ni utajiri wake wa mafuta na madini. Mabilioni kwa mabilioni ya dola za Marekani yakiingia katika hazina za Serikali lakini yakitafunwa na viongozi wachache wa chama cha MPLA, kilichoundwa juu ya misingi ya nadharia ya Kimarx na kilichoporomoka kimaadili na kuwa moja ya vyama vya Kiafrika vilivyokumbwa na ufisadi.

Wananchi wa Angola wamezoea kusikia jinsi mawaziri wao wanavyonunua majumba Lisbon, Paris na London huku wengi wao wakiishi katika vibanda.

Hiyo ndiyo hali halisi, “situacao,” ya Angola. Kwenye kilele cha ufisadi huo yuko Rais Jose Eduardo dos Santos “Zedu” na familia yake, hasa binti yake Isabel, anayesemekana kuwa bilionea wa kwanza wa kike katika Afrika, pamoja na wanawe wengine na jamaa zake.

Pia wako mawaziri, majenerali wa kijeshi na vigogo wa MPLA. Hivi karibuni, miezi miwili tu, iliyopita mahakama moja ya Ureno iliamua kwamba Makamu wa Rais wa Angola, Manuel Vincente, apandishwe kizimbani kwa mashitaka ya kumhonga mshitaki wa zamani wa Serikali ya Ureno.

Inasemekana kwamba alimhonga fedha zenye thamani ya dola za Marekani 810,000 ili afifirishe uchunguzi aliokuwa akiufanya juu ya ufisadi wa Vicente alipokuwa akiliongoza shirika la Serikali la mafuta, Sonangol, baina ya 2009 na 2012. Shirika hilo sasa linaongozwa na Isabel dos Santos, binti wa Rais.

Hakuna mwanamke asiyependwa Angola kama yeye. Ingelikuwa Vicente hakugubikwa na mashitaki hayo inaaminika angelikuwa anaongoza orodha ya wagombea wa MPLA katika uchaguzi mkuu wa leo Agosti 23.

Orodha hiyo sasa inaongozwa na Waziri wa Ulinzi, Joao Lourenco, maarufu kwa jina la “JLo”, mtu mpole asiye na kibri, kinyume na viongozi wenzake wa MPLA. Kwa miaka tunaozifuatilia siasa za Angola tumekuwa tukisema kwamba dos Santos, hatobanduka kwenye kiti cha urais.

Tukiamini kuwa ni mauti tu yatayomuondoa, ama kwa kupigwa risasi au kwa kupigwa na maradhi. Tulikosea. Mwaka huu, akiwa na umri wa miaka 74, ametimiza ahadi na anampisha mwengine kwenye kiti cha urais achokikalia tangu afariki Rais wa kwanza Dk. Agostinho Neto miaka 38 iliyopita. Inasemekana kwamba dos Santos akitaka mwanawe, Jose Filomeno, amrithi.

Lakini hilo halikuwezekana kwa sababu vigogo wa MPLA walimtilia guu. Ndipo bahati ilipomwangukia Lourenco, aliyekuwa akiumezea mate urais kwa muda mrefu. Safari moja katika miaka ya 1990, dos Santos aliwatania wenzake alipowaambia kwamba anafikiria kujiuzulu. Lourenço alijitokeza na kusema: “Mimi nipo”.

Maneno hayo mawili yalimponza na kwa miaka dos Santos alimtesa kisiasa. Chama cha MPLA hakitojiachia kishindwe katika uchaguzi wa leo. Lakini kinakabiliwa na changamoto kubwa, hasa za kiuchumi.

Angola inapata takriban asilimia 90 ya sarafu zake za kigeni kwa kuuza mafuta. Juu ya utajiri wake wa mafuta, almasi na madini mingine, wananchi wengi wa Angola wanaishi maisha duni.

Kuanguka kwa bei za mafuta katika masoko ya kimataifa miaka miwili mitatu iliyopita kumezidi kuuathiri uchumi wa nchi. Watu wengi wamevunjwa moyo na MPLA.

Uchaguzi wa leo ni wa mwanzo kwa vijana wengi. Ikiwa chama cha MPLA kitashinda na Lourenco akawa Rais, basi dos Santos anatumai ataendelea kuidhibiti Angola kama alivyoidhibiti kwa miaka 38 iliyopita.

Kwa kuwa anaendelea kuwa rais wa MPLA amejipangia awe na madaraka makubwa yatayomwezesha kuwateua wagombea ubunge wa chama chake na maofisa wakuu wa jeshi na polisi. Hata hivyo, mikono ya dos Santos yatafungika.

Kwanza afya yake si nzuri. Halafu anachukiwa ndani na nje ya chama chake kwa jinsi alivyoukabidhi utajiri wa nchi mikononi mwa wanawe, Isabel na Filomeno, ambaye ni mkuu wa Fundo Soberano de Angola (FSDEA), Mfuko wa Utajiri wa Taifa wa Angola, wenye akiba ya dola za Marekani bilioni 5.

Kuondoka kwa dos Santos kwenye urais huenda kukawa na athari nje ya Angola. Kwa mfano, mkwewe, Sindika Dokolo, mume wa Isabel, anakabiliwa na mashitaka Kinshasa, Kongo, kwa kula njama za kumpindua Rais Joseph Kabila. Mwezi Julai mahakama moja ya Kinshasa ilimhukumu kifungo cha mwaka mmoja jela kwa kosa la ulaghai.

Dokolo, Mkongomani aliyezaliwa na mama kutoka Denmark, amesema amehukumiwa hivyo kwa sababu anamuunga mkono mpinzani wa Kabila, Moise Katumbi. Kwa sasa hayuko jela. Anahifadhiwa na mkwewe Luanda.

Muhimu zaidi ni kwamba Lourenco atataka kuonesha kwamba yeye ndiye mwenye nguvu na atafanya mambo tofauti na dos Santos. Dos Santos aliposhika urais 1974 watu wengi walimdharau.

Wakifikiri atakuwa rais wa mpito kwa vile hakuwahi kuwa jeshini wala hakupigana dhidi ya wakoloni wa Kireno.

Ukikiangalia namna chama cha MPLA kilivyokuwa kimepangika siku hizo, mtu ambaye angepaswa kumrithi Neto alikuwa Lucio Lara, aliyekuwa katibu mkuu wa MPLA.

Lakini Lara alikuwa mwerevu. Alijua kwamba angelikuwa rais, isingefika hata miezi mitatu wenzake wangempindua. Sababu iliyomfanya afikiri hivyo ni siasa za “ugozi” za baadhi ya viongozi wenzake wa MPLA ambao akijua wasingemkubali “mulatto” kama yeye, mtu aliyechanganya damu, awe Rais.

Kwa hivyo, ni Lara aliyesababisha dos Santos awe rais. Na alipokuwa rais aliwashangaza waliokuwa wakimdharau kwa namna alivyojenga mtandao wake na kuihodhi Angola, kisiasa na kiuchumi. Aliwapiga chenga wenzake wote hasa wale waliokuwa na itikadi madhubuti ya Kimarx.

Safari hii yeye ndiye aliyesababisha kuchomoza kwa Lourenco anayeweza akawa Rais mpya wa Angola. Nimeandika kusudi “anayeweza” kwa sababu mchuano ni mkali kati ya MPLA na vyama vya upinzani, hasa cha UNITA kinchoongozwa na Isaias Samakuva, na cha Casa-Ce kinachoongozwa na Abel Chivukuvuku.

Utafiti mmoja uliofanywa karibuni kupima jinsi wananchi wa Angola wanavyoelekea kupiga kura umeonesha kwamba MPLA kitashinda kwa asilimia 38, Unita kwa asilimia 32 na Casa-Ce kwa asilimia 26.

Endapo Chivukuvuku ataamua kuungana na wenzake wa zamani wa UNITA ushindi utakuwa wao. Yakijiri hayo hamna shaka kwamba Angola mpya itazaliwa.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la Raia Mwema la tarehe 23 Agosti 2017. Mwandishi wake, Ahmed Rajab, anapatikana kwa barua-pepe: aamahmedrajab@icloud.com


Filed under: SIASA

UKUTA umefunua siri ya Tanzania – Lissu

$
0
0

Kwa muda mrefu watu wengi wamekuwa wanafikiri kwamba nchi yetu inatawaliwa na chama cha siasa, yaani CCM.

Hata hivyo, wapo wachache ambao walishaanza kuhoji kama CCM ni chama cha siasa hata kabla mfumo wa vyama vingi vya siasa kuruhusiwa miaka 25 iliyopita.

Ukisoma ‘The State and the Working People in Tanzania’, kilichohaririwa na Prof. Issa G. Shivji na kuchapishwa mwaka ’87, utagundua kwamba tayari kuna wasomi ambao walishaanza kuhoji kama kweli CCM ni chama cha siasa.

Chama cha siasa huongoza kwa hoja za kisiasa, sio kwa bunduki, mizinga na mabomu.

Chama cha siasa hushinda mijadala ya kisiasa kwa kutumia ushawishi wa hoja za kisiasa na kiitikadi, sio kwa vitisho vya kuua au kuvunja miguu ya mahasimu wake wa kisiasa.

Chama cha siasa huenda kwa wananchi kuwashawishi wakiunge mkono, hakijifichi nyuma ya vyombo vya ukandamizaji vya dola na kuwatisha wananchi.

Miaka miwili iliyopita Jakaya Kikwete aliwaambia wanaCCM wenzake waende kwa wananchi wakafanye kazi ya siasa, waache kutegemea kubebwa na Jeshi la Polisi.

Hili limewashinda, bila majeshi na bunduki na mabomu, CCM haiwezi kufanya kazi ya siasa. Bila ma-DC na ma-OCD, CCM haiwezi chochote.

Zamani walikuwa wanatuita sisi wapinzani vyama vya msimu vinavyosubiri uchaguzi ndio tufanye kazi ya siasa.

Sasa wanatukataza kufanya kazi ya siasa mpaka tusubiri msimu wa uchaguzi. Sasa sisi ndio chama cha siasa, CCM imegeuka kuwa chama cha msimu.

Wanajifanya walishinda uchaguzi lakini hawadiriki kuturuhusu sisi tulioshindwa kwenda kuongea na wananchi. Wenye hatia huwa na hofu – the guilty are afraid.

Wanatukataza siasa kwa sababu wanajua hawakushinda uchaguzi na wanajua wananchi wengi wanajua hivyo. Na wanajua hawana majibu ya hoja nyingi za kisiasa za utawala huu wa kidikteta.

Kwenye ‘The State and the Working People in Tanzania‘ kuna makala inayoitwa ‘The State and the Party‘ ambayo inazungumzia uhusiano kati ya CCM na vyombo vya dola, hasa majeshi.

Tangu mwaka ’64 lilipoundwa Jeshi la Wananchi wa Tanzania, kumekuwa na mwingiliano mkubwa sana kati ya chama na vyombo vya ukandamizaji vya dola.

Mfano mzuri wa uhusiano huu ni makada wa chama kuingizwa jeshini na kufanywa maafisa wa jeshi, na maafisa wa jeshi kufanywa makada wa chama na kupewa kazi za kisiasa na/au za kiraia.

Wafikirie akina Kikwete, Kinana, Makamba, Nsa Kaisi, Kiwelu, Nnauye, Kafanabo, n.k. Orodha ni ndefu sana.

Wakati wa mfumo wa chama kimoja, majeshi yaligeuzwa kuwa Mkoa wa Chama, sawa na mikoa ya kijiografia kama Dar es Salaam au Singida.

Lengo lilikuwa ni kuwatangamanisha zaidi majeshi katika mfumo wa kisiasa na kiraia ili kuulinda mfumo unaotawala. Katika enzi za vyama vingi, majeshi yameondolewa katika siasa kikatiba na kinadharia tu.

Katika hali halisi, mambo hayajabadilika kwa kiasi chochote cha maana. Angalia wanajeshi walioko katika nyadhifa za kisiasa za kiraia kama wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na sasa hata makatibu wakuu wa wizara. Wote hawa ni wanaCCM kwa Katiba ya sasa ya CCM.

Angalia wanajeshi walioko katika uongozi wa CCM ambao jana tu walikuwa wanakatazwa na Katiba ya nchi kuwa wanachama wa vyama vya siasa.

Kwa hiyo, kinachoonekana sasa kwa majeshi kujitokeza hadharani ili kuzuia UKUTA, ni ushahidi wa wazi kwamba CCM haiwezi tena kujenga hoja ya kisiasa kwa wananchi na ikakubaliwa.

Sasa ni wakati wa mabavu ya kijeshi tu. Na wala sio utii wa sheria bila shuruti tena. Kwa vile sheria ya mikutano ya kisiasa na maandamano iko upande wetu, sasa ni wakati wa shuruti ya kijeshi bila sheria.

Tukishinda vita hii ya sasa, watesi wetu hawatakuwa ni silaha nyingine yoyote itakayobaki. Tutashinda. Wakati ni UKUTA.

Aluta continua!


Filed under: SIASA Tagged: CCM, Tanzania, Tundu Lissu

Wafanyabiashara ‘wampa siku 30’ Magufuli

$
0
0

UONGOZI wa wafanyabiashara wa Tanzania bara na Zanzibar wametoa siku 30 Rais John Magufuli kuhakikisha anatatua changamoto zinazowakabili katika shughuli zao vinginevyo maduka yote hata ya vichochoroni yatafungwa, unaandika mtandao wa MwanaHalisi Online.

Kauli hiyo nzito imetolewa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT), Johnson Minja wakati akihitimisha kikao cha siku mbili cha halmashauri kuu ya jumuiya hiyo.

Minja akisoma maazimio hayo sita yaliyofikiwa katika vikao hicho alisema, lengo kubwa ni kuhakikisha changamoto za wafanyabiashara zinatatuliwa.

Katika maazimio hayo pamoja na kutaka changamoto zitatuliwe wamesema kuwa hawataki kero zao zitatuliwe na kiongozi yoyote isipokuwa rais wa nchi ambaye ni Dk.John Magufuli.

“Halmashauri kuu taifa imeagizwa kumuona mheshimiwa rais kuzungumzia mwenendo mzima wa ufanyaji biashara wa wamachinga kutaka ushuru wa huduma (service levy) iondolewe kwenye maduka badala yake ibakie kwenye makampuni na maduka makubwa,” amesema Minja.

Ametaja maazimio mengine ni pamoja na kuitaka taasisi ya rais, kufuta agizo la waziri wa fedha kwamba mashine ya EFD ikiharibika ndani ya saa 48 na mfanyabiashara akiwa na uthibitisho wa barua kutoka Mamlaka ya Kodi Tanzania (TRA), akamatwe na alipe faini.

Pia imeazimiwa kuwa tangazo la TRA kuhusu kubadili mashine za EFD lirekebishwe, badala ya kutaka wafanyabiashara kununua kwa mara ya pili mashine hizo mawakala ndiyo watakiwe kubadilisha mashine husika.

Aidha, wametaka wafanyabiashara ambao wameishalipa gharama za kupatiwa mashine na hawajapatiw, wapatiwe mashine zao mara moja.

Minja amesema utitiri wa tozo mbalimbali za halmashauri na taasisi nyingine ziainishwe ili ambazo ni kero zifutwe kama rasi alivyoagiza huku zenye mashiko ziunganishwe na kuwekwa kwenye malipo ya leseni.

Amesema wameazimia kukabiliana na kaasumba inayoendelea ya kufunga maduka bila kuwa na uthibitisho wa maamuzi ya kimahakama.

“Kutokana na maazimio haya tunawaagiza wafanyabiashara wote nchini kuendelea kutoa huduma kama kawaida ndani ya mwezi mmoja wakati bodi ya uongozi ikitekeleza maagizo na maazimio ya halmashauri kuu baada ya muda huo bodi itatoa mrejesho juu ya hoja hizi,” ameeleza Minja.

Chanzo: MwanaHalisi Online


Filed under: HABARI Tagged: biashara, Magufuli, Tanzania, Zanzibar

Kikwete si wa kuyasema haya

$
0
0

Katika wiki iliyopita, vyombo vya habari nchini Tanzania vilijawa na habari na tahariri kuhusu marais wawili wastaafu wakiwa kwenye jukwaa la viongozi wastaafu wa Afrika nchini Afrika Kusini.

Katika mkutano huo, ambao marais Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete walialikwa kujumuika na wastaafu wenzao barani Afrika kuzungumzia mambo yanayoliathiri bara la Afrika, waliripotiwa kuisemea vizuri demokrasia, utawala bora na uongozi uliotukuka.

Kwa sababu tatu maalum, nitamuwacha Rais Mkapa kwenye uchambuzi wa leo, na nitajikita kwa Rais Kikwete: moja, ni Kikwete ambaye alichukuwa nafasi zaidi kwenye kurasa za magazeti ya nyumbani, na husemwa kuwa nyongeza huenda kwenye fungu.

Mbili – na pengine ndio iliyosababisha hiyo ya awali – Kikwete si mkuukuu sana kwenye uongozi. Huyu ameondoka majuzi tu madarakani kumpisha Rais John Magufuli, na ndio maana hadi sasa pakifanywa mlinganisho, wachambuzi huwapima wawili kwenye mizani moja wakidadisi nani kamzidi nani kwenye nini.

Kuna hata walioona kuwa kauli ya Kikwete ya Afrika Kusini na ile ya Magufuli akiwa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Kigamboni, zilikuwa majibizano ya moja kwa moja. Mmoja akitumia jukwaa la Gauteng kurusha dongo nyumbani dhidi ya utawala unaowachukulia wapinzani kuwa maadui na unaoliminya bunge, huku mwengine akitumia jukwaa la nyumbani kukumbushia uongozi wa ovyo ulioilitia taifa hasara ya matrilioni ya shilingi kwa mikataba mibovu “ya kijinga na kipumbavu”.

Na sababu ya tatu ni kuwa kuna masuala aliyoyazungumzia Kikwete ambayo yanahusu moja kwa moja kesi ya uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba 2015 uliofanyika wakati yeye akiwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mwenyekiti wa chama tawala cha Mapinduzi (CCM) na pia amiri jeshi mkuu wa majeshi ya ulinzi na usalama. Kwa ufupi, akiwa kwenye kilele cha nguvu, madaraka na maamuzi.

Kwenye jukwaa la viongozi wastaafu, Kikwete alizungumzia mambo matatu muhimu aliyoyaita kuwa ni mihimili muhimu kwa demokrasia na utawala bora barani Afrika: vyama vingi, chaguzi, na mabunge. Kwa sababu ya uchache wa muda, nitaepuka kuyajadili aliyoyasema kwenye vyama vingi na mabunge na nitabakia na moja tu – la chaguzi.

Na kwa maslahi ya uchambuzi, naomba hapa niweke tafsiri ya Kiswahili isiyo rasmi ya kile alichokizungumza yeye kwa Kiingereza kwenye jukwaa hilo:

“La pili (muhimu katika demokrasia na utawala bora barani Afrika), ni chaguzi za kawaida za kidemokrasia. Afrika inafanya chaguzi hizo. Hakuna shaka kwenye hilo. Suala sasa ni namna inavyofanya chaguzi hizo. Je, ni chaguzi za kweli, au za aibu, au za mashaka?

“Hapana shaka, daima kunakuwa na wachunguzi wa chaguzi, na tumeona kwenye ripoti zao… ukiwa unafuatilia ripoti hizo, kuna maendeleo fulani. Kwenye chaguzi za mwanzo kunakuwa na matatizo. Waangalizi wa ndani na wa kimataifa wanatoa mapendekezo, tume za chaguzi zinafanya marekebisho.

“Bila shaka, kuna maeneo ambayo kuna matatizo kwenye chaguzi…Kuna tatizo ambalo naliona, na ambalo hatuwezi kujidai kuwa halipo. Kumekuwa na utamaduni wa kutokukubali kushindwa. Hili ndilo tatizo jengine tulilonalo barani Afrika. Katika migogoro mingi tunayozungumzia barani Afrika, ina chimbuko lake kwenye chaguzi. Ni baada ya uchaguzi, ndipo unapoona kuna matatizo kwenye nchi.

“Moja ya sababu ni ukweli kwamba kunakuwa na matatizo kwenye uandaaji wa uchaguzi kwa upande wa tume za uchaguzi (na) kwa upande wa serikali zenyewe. Lakini sababu nyengine ni pale ambapo hata hakuna tatizo lolote. Ni ile dhana tu kwamba uchaguzi ni wa huru na haki ikiwa tu ninashinda. Ikiwa sikushinda, hauwezi kuwa huru na wa haki, na kinachofuatia hapo ni kuiingiza nchi kwenye migogoro.”

Akiwa mwanajeshi aliyegeuka mwanasiasa, au ukipenda kinyume chake, Kikwete aliingia madarakani mwaka 2005 kupitia uchaguzi ulioandaliwa chini ya utawala wa mtangulizi wake, Mkapa. Huo ulikuwa ni uchaguzi wa tatu wa vyama vingi, tangu mfumo huo urejeshwe nchini mwaka 1992.

Lakini siku chache kabla ya uchaguzi huo, Mkapa alikuwa ameapa kwamba angelitumia kila nguvu aliyonayo, kama kiongozi wa nchi na dola, kuhakikisha kuwa CCM inarudi madarakani kwenye pande zote mbili za Muungano, akimaanisha kwenye Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ). Aliyasema hayo kwenye ukumbi wa hoteli ya Golden Tulip, Dar es Salaam. Na ndivyo alivyofanya.

Kwa hivyo, uchaguzi uliondaliwa kumuingiza yeye Kikwete madarakani, ulikuwa uchaguzi uliokamiwa na Mkapa kwamba iwe iwavyo, lazima mshindi awe wa chama chake. Uchaguzi wa ushindi lazima, litoke jua ama inyeshe mvua!

Yaliyojiri Zanzibar, ni Mkapa kumimina vikosi vya kijeshi kuliko muda wowote kwenye historia ya nchi yetu hadi wakati huo, na hata alipoulizwa kuhusiana na hilo na Jonathan Power wa jarida la Prospect, jibu lake lilikuwa: “Kwa nini huulizi sababu ya Marekani kupeleka vifaru vyake kule Iraq?”

Huo ndio uchaguzi ambao ulimuingiza madarakani mwanajeshi aliyekuwa wakati huo mwanadiplomasia mkuu wa Tanzania, Kikwete.

Lakini hilo tunaweza kulisema pengine si kosa lake, maana yeye hakuwa rais, mwenyekiti wa chama tawala wala amiri jeshi mkuu wa nchi. Alikuwa waziri tu wa kawaida kwenye baraza la mawaziri la Mkapa na, kwa hivyo, kama kuna lolote baya kwenye kutimiza kiapo cha kuzikabidhisha serikali mbili kwa CCM, lilikuwa ni juu ya Mkapa.

Miaka kumi baadaye ulikuwa ni wakati wa Kikwete kuondoka madarakani na kuachia uongozi kwa wanaomfuatia. Kile kile kiapo alichoapa Mkapa, ndicho alichoonekana kukiapa yeye. Kwamba madhali alikabidhiwa serikali mbili – ya Muungano na ya Zanzibar, naye angelizirithisha serikali hizo hizo mbili mikononi mwa CCM, iwe iwavyo. Piga uwa, kwa Kiswahili cha wenzake wa mjini.

Uchaguzi ulioandaliwa wakati yeye akiwa rais wa nchi, amiri jeshi mkuu, na mwenyekiti wa chama tawala, ulishuhudia mchuano mkali usiopata kushuhudiwa kabla, kwa kuwa kwenye upinzani alihamia Edward Lowassa kupeperusha bendera ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).

Naye, Kikwete, katika jitihada za kumzuwia rafikiye wa zamani aliyegeuka hasimu asiwe mrithi wake, akakanyaga kila msingi wa utawala bora, sheria na demokrasia kuhakikisha kuwa Lowassa hawi rais na Magufuli ndiye anachukuwa nafasi hiyo. Aliapa na kujiapiza kuwa hivyo ndivyo itakavyokuwa.

Wengi wanakumbuka kuvamiwa kwa kituo cha kukusanyia matokeo ya kura cha UKAWA kilichokuwepo Mikocheni, ambapo waliokuwapo walipigwa na vifaa kama kompyuta kuchukuliwa. Uvamizi kama huo pia ulikikumba Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, LHRC.

Kabla ya hapo, muda mchache kabla ya bunge kuvunjwa, serikali yake ilipeleka haraka na kuupitisha mswaada wa makosa ya uhalifu mitandaoni, ambayo ilikuwa na imekuwa tangu wakati huo hadi sasa, nyundo ya kuwaangamiza wakosoaji wa watawala kwenye mitandao ya kijamii.

Yote hayo yanaweza kuwa madogo. Tarehe 27 Oktoba 2015, akiwa amiri jeshi mkuu, Kikwete alituma wanajeshi kukiteka kituo cha kutangazia matokeo ya uchaguzi wa urais wa Zanzibar kilichokuwapo Hoteli ya Bwawani mjini Unguja, na siku moja baadaye Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (ZEC), Jecha Salum Jecha, akatangaza kuufuta uchaguzi, ambao waangalizi wa ndani na nje walikuwa wamesema ulikuwa wa haki zaidi na uhuru zaidi kuwahi kufanyika visiwani humo tangu mwaka 1995.

Kwa nini alichukuwa hatua hiyo? Ni kwa sababu ya kile alichokieleza yeye mwenyewe majuzi Afrika Kusini: “Dhana tu kwamba uchaguzi ni wa huru na haki ikiwa tu ninashinda. Ikiwa sikushinda, hauwezi kuwa huru na wa haki, na kinachofuatia hapo ni kuiingiza nchi kwenye migogoro.”

Na, naam, Zanzibar imeingia kwenye mgogoro mwengine mkubwa sana, mgogoro ulioumbwa na mikono ya Kikwete. Sio tu kwamba demokrasia ilizuiwa kuchukuwa mkondo wake kwa maslahi ya kumfanya Kikwete arithishe serikali mbili kwa CCM kama alizoachiwa na Mkapa, bali pia imo kwenye aibu kubwa kwa katiba yake yenyewe, ambayo inaamuru nchi kuongozwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa.

Leo hii serikali iliyopo Zanzibar ni kituko. Ina makamu wa pili wa rais lakini haina makamu wa kwanza. Ina baraza la wawakilishi lisilo na deski la wapinzani. Ina utawala wa chama kimoja ndani ya mfumo wa vyama vingi.

Huo ndio urithi wa Kikwete, kiongozi anayejipa uthubutu leo hii kukaa jukwaani Afrika Kusini kuzungumzia demokrasia na utawala bora barani Afrika. Ndio maana wengine hupatwa na kichefuchefu tunapomsikia kwenye majukwaa ya kimataifa akizungumzia demokrasia, maana tunamjuwa kuwa anadanganya!

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza kwenye gazeti la Mwelekeo la tarehe 29 Agosti 2017.


Filed under: KALAMU YA GHASSANI Tagged: demokrasia, Kikwete, Tanzania, uchaguzi wa Zanzibar, utawala wa sheria, Zanzibar

Tanzania hailiwi na rushwa pekee, bali pia na ufisadi wa kisiasa

$
0
0

Majuzi Rais John Magufuli alimuapisha Brigedia Jenerali John Mbungo kuwa Naibu Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana  na Rushwa (TAKUKURU) akiweka msisitizo kwamba anataka kuona wala rushwa wanafungwa jela haraka iwezekanavyo.

Kwa maneno yake mwenyewe Rais Magufuli, “mambo makubwa ambayo taifa linapambana nayo yanatokana na rushwa…” na kwamba kama Tanzania ikifanikiwa kuipunguza rushwa angalau kwa asilimia 80, basi itakuwa imeyatatua matatizo yake mengi sana.

Hakuna anayepinga kwamba Tanzania, ambayo imeongozwa na Chama cha Mapinduzi (CCM) – chama chake yeye Rais Magufuli – muda wote wa kuwa kwake taifa huru, imeoza kwa rushwa. Inanuka, imeoza, kila mahala, kila sekta!

Lakini katikati ya uoza huo, au pengine kwa sababu ya uoza huo, ndipo unapokuta hii tabia yetu mbovu ya kuuzungumzia uchafu kwa maneno yanayochuja kimaana. Mojawapo likiwa ni hili la kuuita ufisadi kuwa ni rushwa. Rushwa tu!

Ukweli ni kuwa rushwa ni kitu kidogo sana panapohusika uoza wenyewe hasa uliopo. Rushwa ni utowaji na au upokeaji wa kitu (mara nyingi huwa pesa) kwa ajili ya kutoa au kupokea huduma, ambayo kimsingi ingelikuwa haki kutolewa bila ya kitu hicho.

Na Mohammed Ghassani

Wengi wetu tunadhani rushwa ni sawa na ule msamiati wa Kiingereza ‘corruption’, ndiyo maana hata hiyo taasisi inayoshughulika na kadhia hiyo inaitwa TAKUKURU kwa kuwa tunasema inafanya kazi ya kupambana na kuzuia rushwa.

Na kwa kuwa tunakosea kwenye kuipa jina lake halisi hali hii tunayokabiliana nayo, ndio  maana tunazunguka mumo humo, tukiamini kwamba kubadilisha sura kwenye chombo chenye mamlaka ya kupambana na hali hii kunatosha kuimaliza.

Ukweli ni kwamba kuiangalia hali kwa jicho lake halisi kuna nafasi kubwa mno kwenye kuzifikia hizo asilimia 80 anazolenga Rais Magufuli kwenye vita hivi vikubwa na, kwa hakika, vyenye maana kwetu sote.

Tanzania inaliwa na ufisadi na sio rushwa pekee, na tena ufisadi mkubwa zaidi ni ule wa kisiasa, ambao umejengewa mihimili kwa miaka 50 ya utawala wa CCM, kiasi cha kuufanya uonekane hali ya kawaida kwenye maisha ya kila siku.

Ufisadi wa kisiasa unakwenda mbali zaidi ya pale rushwa ya kutoa na kupokea fedha inapoishia. Huu ni utumiaji mbaya wa madaraka unaofanywa na maafisa wa serikali na, au, wa taasisi za kisiasa kwa maslahi binafsi. Aina zake ni za viwango tafauti, na hiyo rushwa moja tu miongoni mwao.

Katika upana wake utakuta pia udugunaizesheni, wizi wa kura, milungula, wizi wa mali ya umma na ubadhirifu, kwa kutaja machache.

Ufisadi huu wa kisiasa, kwa hakika, ndio mama wa maovu mengine yote katika pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Uovu wa madawa ya kulevya, ujambazi, ukahaba na umasikini wa watu wetu, kwa mfano, ni matokeo ya ufisadi wa kisiasa ambao umekuwa ukiila nchi yetu kwa zaidi ya miongo mitano sasa.

Bahati mbaya ni kuwa ufisadi huu una khulka moja ya hatari sana: kuzoeleka. Kila anayechukua nafasi ya uongozi wa umma katika serikali au taasisi ya kisiasa huona sawa kwake kuwa fisadi, na kwa hakika jamii humtarajia awe hivyo. Kwamba atumie fursa ile kujinufaisha binafsi, awatishe wengine, awakomowe, awaangamize ili yeye awe hapo alipo .

Ndio maana maafisa wa tume za uchaguzi huiba kura kwa ajili ya kuwanufaisha wanasiasa wanaowapa vyeo, wagombea hununua wapiga kura, polisi hula mkono kwa mkono na wahalifu, maprofesa hupasisha au kufelisha wanafunzi vyuoni kwa kuzingatia maslahi yao binafsi. Alimradi ni mchafukoge.

Jamii hii ya mchafukoge ni muakisiko wa ufisadi wa kisiasa uliopea na kuzoeleka. Utamaduni wa chukua chako mapema, wa iba ulindwe na kemea udhibitiwe (kama wanavyoonekana kudhibitiwa wapinzani sasa), ndio unaojenga fikra za Watanzania uwaonao mbele yako leo.

Si hasha, kwa hivyo, kusikia hata miongoni mwa kada za hao waitwao wasomi leo hii wakisema: “Naye Tundu Lissu kazidi kidomodomo.” Kwao wao ufisadi ni ada ya maisha ya kila siku.

Kilele cha utamaduni huu huwa ni kile kinachoitwa kleptocracy (rule by thieves), yaani utawala wa wizi – wizi wa kura, wizi wa mali, wizi wa matumaini, wizi wa kesho ya wanyonge walio wengi.

Ufisadi una hatari kubwa na ya pekee katika maendeleo ya taifa. Katika siasa, hufifisha na wakati mwengine kuua kabisa mfumo wa kidemokrasia na utawala wa sheria, maana ufisadi una kiburi cha kuingilia kati chochote ambacho kinaonekana kiko dhidi yake. Ukweli ni kwamba demokrasia na utawala wa sheria ni adui kwa ufisadi; na kilipo kimoja chengine hakikai.

Kwa hivyo, kwa jamii kama yetu, ambayo imejikita katika uoza wa kupindukia wa ufisadi, mafisadi wenyewe hawataki kabisa kuona mfumo wa demokrasia ukistawi ama utawala wa sheria ukisimama. Si ajabu, kwa hivyo, kuona wakiingilia kati taratibu za kawaida za kidemokrasia na za utawala wa sheria kila pale wanapoona zinachukuwa mkondo wake.

Ya kuharibiwa kila mara kwa chaguzi za Zanzibar, kwa mfano, kwa kupelekwa majeshi yenye silaha nzito nzito ni katika hizo jitihada za ufisadi kupingana na demokrasia na utawala wa sheria.

Ufisadi katika chaguzi hupelekea ofisi za umma kukaliwa na watu wasiotokana na ridhaa ya umma na hivyo nao matokeo yake huzikalia ofisi hizo kwa maslahi yao binafsi na sio kwa maslahi ya umma, maana sio uliowaweka ofisini.

Leo hii Rais Magufuli anapolilia ukosefu wa uzalendo miongoni mwa wenzake serikalini – wanaofikia hadi kusaini mikataba ya kuuza madini kiholela – anapaswa kujiuliza namna hao watiaji saini walivyofika hapo madarakani. Je, ni kwa demorasia au kwa ufisadi wa kisiasa?

Ufisadi katika vyombo vya kutunga sheria hupunguza au huondosha kabisa uwajibikaji na uwakilishi wa kweli katika vyombo hivyo; ufisadi kwenye mahakama huiweka rehani haki ya wananchi; na ufisadi kwenye utawala husababisha ukosefu wa uadilifu katika utowaji wa huduma za kijamii.

Kwa jumla, ufisadi hukokozoa kabisa uwezo wa kitaasisi wa serikali, kwani husababisha taratibu kupuuzwa, rasilimali kuporwa, na ofisi za umma kuuzwa na kununuliwa kama bidhaa nyengine yoyote.

Ufisadi wa kisiasa ukipevuka huufanya hata uhalali wa serikali iliyopo madarakani uhojike na vivyo misingi ya demokrasia na kuaminiana itoweke. Ni mapema, pengine, sasa kwa wananchi wa Tanzania kuhoji uhalali wa serikali yao, lakini kwa mwenendo huu tunaokwenda nao, si muda mrefu tena ujao, hilo la kuhoji litakuwa wajibu wetu wa mwanzo!

Lakini wakati tukisubiri wakati huo ufike, sote ni mashahidi wa namna ambavyo ufisadi wa kisiasa unadumaza maendeleo ya kiuchumi kwa kuchochea ubadhirifu na ukosefu wa ufanisi.

Watanzania wameshuhudia mali za nchi zikiibiwa mbele ya macho yao: mchanga wa dhahabu unasafirishwa makontena kwa makontena, meli za kigeni zinavua tani kwa tani za samaki kwenye bahari yao, na wenye vyeo wanajikopesha na kujikatia juu kwa juu kutoka hazina ya taifa.

Na hayo hayajasimama kwa kuwa Rais Magufuli kasema anataka kuwaona wala rushwa wakifungwa jela. Yatasimama kwa kuuita ufisadi kwa jina lake halisi na kuutendea kama ututendeavyo – kuuwa maana nao unatuuwa.

Haitoshi kila siku kulia majukwaani na kwenye vichwa vya habari magazetini. Kuuzungumzia ufisadi kwa jina la rushwa hakutoshi. Kueleza ushahidi wa rushwa hiyo ilivyolimaliza taifa pia hakutoshi.

Hakutoshi, maana baada ya kuwa mashahidi na walalamikaji miaka yote 50 ya taifa huru, kumetusaidia nini? Kwa karibuni miongo mitano yote, hiyo imekuwa hali ambayo taifa hili limeishi nayo.

Leo hii tunajikokota kwenye mstari wa mwisho wa umasikini duniani, watoto wetu wakifa kwa maradhi na njaa, na bado tumeendelea kuwa mashahidi na walalamikaji ambao tunalizunguka tatizo lenyewe, badala ya kutua katikati yake – penye ufisadi wa kisiasa.

Kwa hivyo, si mwanajeshi  John Mbungo anayepaswa kuvaa magwanda yake kupambana na ufisadi huu wa kisiasa, maana si ajabu kuwa hata yeye mwenyewe ni matokeo ya mfumo uliousimamisha ufisadi wa aina hiyo, na ndio maana hata amiri jeshi wake anataka tu akahakikishe anawafunga wala rushwa. Wala rushwa tu!

Ni wananchi wanaopaswa, kwanza, kuufahamu  ufisadi wa kisiasa ambao Tanzania imekulia nao. Kisha, pili, kuuchukia kwelikweli, na mwisho, la tatu, kuchukuwa hatua dhidi ya uoza huu kwa njia halali.

Miongo hiyo mitano ya ufisadi wa kisiasa imewashuhudia watawala wale wale wakiwazoesha kuupenda na kuushabikia ufisadi na kuufanya kuwa utamaduni wao. Wamewapotosha vya kutosha. Wamefanywa waone jambo la kawaida kutoa na kupokea rushwa. Wamewafanya wautarajie ufisadi na wautegemee kama njia ya kupita kufika waendako.

Wanapaswa sasa kukataa na kusema hapana. Hapana kwa ufisadi wa kisiasa. Hapana kwa mafisadi wa kisiasa.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHALISI la tarehe 28 Agosti 2017.

 


Filed under: KALAMU YA GHASSANI Tagged: CCM, John Magufuli, rushwa, TAKUKURU, Tanzania, ufisadi

Uamuzi wa Mahakama ya Juu Kenya ufuatiwe na marekebisho

$
0
0

Mkuu wa Idhaa ya Kiswahili ya DW, Andrea Schmidt, anasema baada ya Mahakama ya Juu ya Kenya kuufuta uchaguzi na kuamuru mwengine, sasa ni wakati wa Kenya kuendelea kuonesha njia kwa kuheshimu maamuzi hayo na kurekebisha.

Huu ni ushindi wa wazi kwa demokrasia barani Afrika. Kwa mara ya kwanza Mahakama ya Juu nchini Kenya imeyatangaza matokeo ya uchaguzi uliokwishamalizika kuwa ni batili, baada ya upinzani ukiongozwa na kinara wao, Raila Odinga, kuyawekea pingamizi mahakamani, na hatimaye kufanikiwa kupata haki.

Baada ya matokeo yaliyotangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kumpa Uhuru Kenyatta ushindi wa asilimia 54.27 na kumuwacha nyuma Odinga kwa asilimia 44,74, kiongozi huyo wa upinzani aliamua kufanya kile ambacho ni mzoefu nacho – kupinga matokeo na kwenda mahakamani.

Hata hivyo, uamuzi wa mara hii wa Mahakama ya Juu chini ya Jaji Mkuu David Maranga haukuwa umefikiriwa na wengi. Kwa kutumia uzoefu wa mwaka 2013, ambapo Odinga aliwasilisha zuio kama hili, wengi walidhani kuwa na mara hii pia angelishindwa.

Na Andrea Schmidt

Lakini tangu Jumatatu ilipoiamuru IEBC kuwapa wapinzani fursa ya kuona mitambo ya kukusanyia matokeo ya tume hiyo, kila mtu alianza kuona kuwa sasa inakusudia kuwa kweli madhubuti. Inaonesha kuwa idara ya mahakama nchini Kenya inaichukulia kazi yake kwa umakini, iko huru na haina khofu mbele ya vyombo vya dola.

Funzo kwa Afrika nzima

Vile vile, maoni kutoka kwa raia wa mataifa jirani kuhusiana na uamuzi huu wa mahakama ya juu yanatia moyo. Hawa ni raia ambao wenyewe ni wahanga wa usaliti unaofanywa na dola dhidi ya kura zao.

Uamuzi huu wa leo, kwa hivyo, unatoa matumaini kwa chaguzi zijazo sio tu nchini Kenya, bali pia katika eneo zima la Afrika Mashariki na Kati na Ukanda wa Maziwa Makuu.

Funzo kubwa ni kuwa si kila mara aliye madarakani ndiye mwenye uamuzi wa mwisho kwa kila jambo.

Uhuru Kenyatta kwa upande wake ameamua kuonesha tafauti. Licha ya kwamba hakupendezwa na maamuzi haya ya Mahakama ya Juu, lakini ametangaza waziwazi kuwa anayakubali.

Sasa marekebisho makubwa yafanyike

Hata hivyo, ishara hizi njema kwa demokrasia ya Kenya hazipaswi kuishia hapo tu. Mahakama ya Juu imeamuru uchaguzi mpya kufanyika ndani ya siku 60 kutoka sasa.

Lakini, kwa vyovyote vile, haielekei kuwa uchaguzi huo uandaliwe na kusimamiwa na chombo kile kile ambacho kimehusika na uchaguzi uliofutwa.

Kwa Wakenya wengi, IEBC haiaminiki tena.

Tayari baadhi ya Wakenya wanashauri kuwa ili uchaguzi mwengine uwe wa kuaminika, basi unapaswa kusimamiwa na Umoja wa Mataifa.

Lakini mimi naona waende mbali zaidi ya hapo. Kwanza, serikali iliyopo sasa madarakani ikae kitako na upinzani kuteua tume mpya ya uchaguzi. Pili, yale mapungufu yote ya uchaguzi uliofutwa yajuilikane na yawekwe wazi kabla ya uchaguzi mpya ndani ya miezi miwili hii.

Pia waangalizi wa kimataifa waliupa sifa uchaguzi wa Agosti 8 kuwa ulikuwa huru na wa haki. Sasa wanapaswa kujifikiria upya.

Jengine kubwa pia kwa muhimu ni kwa wafuasi wa chama tawala Jubilee kufanya kama alivyofanya kiongozi wao, Rais Uhuru Kenyatta, kuyakubali maamuzi ya mahakama.

Wakenya wanastahiki uchaguzi wa kweli.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa na mtandao wa Idhaa ya Kiswahili ya DW. Mwandishi wake, Andrea Schmidt,  ndiye mkuu wa Idhaa hiyo. 
http://www.dw.com/sw/maoni-uamuzi-wa-mahakama-ya-juu-kenya-ufuatiwe-na-marekebisho/a-40331361  


Filed under: SIASA Tagged: andrea schmidt, Idhaa ya Kiswahili ya DW, Kenya, Raila Odinga. Jaji David Maranga, uchaguzi, Uhuru Kenyatta, Ujerumani

Rais Kenyatta ‘aishambulia’ idara ya mahakama

$
0
0

Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya anasema kuwa nchi hiyo ina “tatizo fulani” na idara ya mahakama ambalo lazima lirekebishwe, huku akiinya idara hiyo kutoingilia kati majukumu ya tume ya uchaguzi, linaandika shirika la utangazaji la Ujerumani, DW.

Kauli hiyo ya Kenyatta inakuja siku moja tu baada ya Mahakama ya Juu kufuta uchaguzi wa tarehe 8 Agosti, ambao ulikuwa umempa ushindi Kenyatta dhidi ya mpinzani wake mkuu, Raila Odinga, na kisha mahakama hiyo kuamuru mwengine mpya ndani ya siku 60.

Odinga, ambaye ndiye aliyefungua kesi ya kuweka zuio la ushindi huo wa Kenyatta uliotangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), alikuwa anahoji kwamba kulikuwa na ghiliba nyingi kwenye matokeo ya IEBC.

Baada ya ushindi huo wa Ijumaa, sasa Odinga anataka IEBC nzima ivunjwe, lakini kwenye hotuba yake ya leo, Kenyatta ameionya mahakama dhidi ya kuiingilia kati tume hiyo ya uchaguzi.

“Tutaipitia upya hii kitu. Kwa kweli tuna tatizo fulani,” alisema akimaanisha idara ya mahakama.

“Nani kwani hasa alikuchaguweni? Ni nyinyi? Tuna tatizo la lazima tulirekebishe,” alisema wakati akihutubia moja kwa moja kupitia televisheni akiwa Ikulu ya Nairobi, mara tu baada ya kukutana na magavana na wateule wengine wa chama chake cha Jubilee.

Kenyatta alirejelea pia ujumbe wake wa siku ya Ijumaa (Septemba 1) kwamba angeliuheshimu uamuzi huo wa Mahakama ya Juu, unaochukuliwa kama hatua kubwa kabisa kwenye mahakama barani Afrika, ambako kawaida serikali zilizo madarakani huwadhibiti majaji.

Akiandika kwenye ukurasa wake wa Twitter siku ya Jumamosi (Septemba 2), Kenyatta alisema: “Kwa sasa, tukutane kwenye kisanduku cha kura.”

Aishambulia mahakama mara ya pili mfululizo

Hii ni mara ya pili tangu uamuzi huo wa mahakama, kwa Kenyatta kutoa kauli kali hadharani dhidi ya idara ya mahakama.

Hapo Ijumaa, akizungumza kwenye mkusanyiko wa wafuasi wake jijini Nairobi, Kenyatta aliikosoa mahakama kwa kudharau matakwa ya Wakenya na kuwaita majaji wa Mahakama ya Juu kuwa ni ‘wakora’.

Wachambuzi wanasema kauli hizi za sasa za Kenyatta dhidi ya idara huru ya mahakama zinaogofya sana.

“Ni jambo la bahati mbaya sana kwamba Kenyatta anaonekana kutoa kauli za vitisho dhidi ya idara ya mahakama,” alisema Murithi Mutifa, mchambuzi wa masuala ya Afrika katika Taasisi ya International Crisis ya Nairobi.

“Huu ulikuwa ni muda wa fahari kubwa kwa demokrasia ya Kenya, ambapo mahakama imeusimamisha utawala wa sheria. Wanasiasa wanapaswa kuchukuwa tahadhari ya kutowachochea wananchi dhidi ya idara ya mahakama.”

Katika uamuzi wake wa Ijumaa, Jaji Mkuu David Maranga alisema kuwa uamuzi huo wa Mahakama ya Juu uliungwa mkono na majaji wanne kati ya sita na kuutangaza ushindi wa asilimia 54 wa Kenyatta kuwa batili.

Taarifa za kina juu ya uamuzi huo zitachapishwa hadharani ndani ya siku 21 tangu hukumu kutolewa.

Chanzo: http://www.dw.com/sw/rais-kenyatta-aishambulia-idara-ya-mahakama/a-40339407


Filed under: HABARI Tagged: Kenya, Raila Odinga, Raila Odinga. Jaji David Maranga, uchaguzi wa kenya 2017, Uhuru Kenyatta

Uhuru aiambia mahakama isijaribu kuingilia kati uchaguzi

$
0
0

Siku moja tu baada ya Mahakama ya Juu nchini Kenya kuufutilia mbali uchaguzi wa Agosti 8 uliompa ushindi Rais Uhuru Kenyatta, kiongozi huyo ameitaka mahakama hiyo kutojaribu kuingilia kati majukumu ya Tume ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), katika wakati ambapo mpinzani wake, Raila Odinga, anataka tume hiyo ivunjwe kwa kile alichokiita “kutenda uhalifu”.


Filed under: VIDIO Tagged: Kenya, Raila Odinga, Uhuru Kenyatta
Uhuru Kenyatta na Mahakama

Nguzo ya 7 mitaji ya mafanikio ni muda

$
0
0

Vitu vyote tunavyotaka kufanya iwe ni kupumzika, kulala, kutembea, kwenda kazini au kusafiri popote; tumepewa muda maalum. Lakini, hakuna mtaji au rasilimali muhimu inayopotea bure na kila mara kuliko zote hapa duniani kama muda. Na bahati mbaya wengi tunaupoteza mtaji huu wa muda pasina kujua. Wakati wote muda unakatika na kuisha kabisa pasipo kungojea au kurudi nyuma. Tunaweza tukawa tunangojea tukio fulani lakini kamwe muda haumgojei mtu yeyote yule.

Katika rasilimali zote alizotujaalia Mungu, muda ndio rasilimali pekee aliyotugawia watu wote kwa usawa bila upendeleo. Mtu maskini na mtu tajiri wote wana saa 24 (angalizo: Kiswahili fasaha cha uwingi wa saa ni saa, si masaa!). Nenda kwenye nchi tajiri na nchi maskini zote zina saa 24 kwa siku. Hakuna siku yenye zaidi ya saa 24. Sote tuna siku 7 kwa juma, hakuna nchi yenye siku 10 kwa juma. Tofauti pekee tulizonazo ni mbili tu: jinsi tunavyoitumia rasilimali muda kwa tija na ufanisi, na kiasi cha muda wa kuishi hapa duniani. Baadhi wanaishi muda mrefu na wengine muda mfupi.

Linapokuja suala la kufanya kazi kwa muda tuliopewa, kuna watu hutumia saa 6 kwa siku, saa 18 huishia njiani, kupiga soga na kisha kwenda kulala. Wengine hutumia saa 8 kwa siku, saa 16 hutumika kupumzika, kusafiri, kustarehe na kulala. Ofisi zetu nyingi hufunguliwa saa 2 asubuhi na kufungwa saa 10 jioni. Ina maana theluthi moja tu ya muda tunafanya kazi na theluthi mbili (zaidi ya 66%) tupo njiani, kustarehe na kulala.

Kwa kusema hivyo, mfanyakazi mwenye miaka 60 kazini, anakuwa katumia miaka 20 tu kufanya kazi. Miaka yote 40 ni kwa ajili ya kulala, kustarehe na kusafiri njiani kwenye foleni au msongamano, hasa kwa wanaoishi mijini. Miaka yote 40 hulipwa mshahara wa bure! Hapa tunabaini kirahisi kwanini hatujaendelea inavyopaswa. Upotevu wa mufa ni mojawapo ya sababu kuu za kusuasua kwetu. Watu waliokwisha endelea hawalali! Wanachakarika kucha-kutwa kusaka maendeleo utadhani dunia inaisha kesho. Wengine hukataa kwenda likizo, na wakipata hufanya kazi zingine za kimaendeleo. Wametambua kuwa muda ni mtaji wa kuwaletea maisha yenye mafanikio.

Umuhimu wa muda katika kuleta mafanikio ya kimaisha

Hekima ya Mungu katika misahafu inatuasa tuukomboe wakati na kuutumia vizuri katika kufanya kazi zenye tija katika maisha yetu (Waefeso 5:15). Aidha muda wetu wa kuishi hapa duniani unatofautiana sana baina yetu. Wengine huishi muda mrefu na wengine muda mfupi. Hata hivyo, wanaobahatika kuishi muda mrefu huishi katika mateso ya maradhi ya uzeeni. Tunaambiwa miili yetu ikiwa na afya njema, miaka yake ya kuishi hapa duniani ni 70 au 80 (Zaburi 90:10). Baada ya hapo ni taabu tupu.

Je, tunautumiaje muda tulionao? Ni swali linalotuchenga sana huku tukijisahau mno kutimiza wajibu wetu na ndoto zetu. Watu wachache sana tunauchukulia muda kuwa ni rasilimali muhimu au mtaji adhimu. Tunaupoteza kwa kufanya mambo yasiyo na tija katika maisha yetu.

Mwaka 2002 nilikuwa Ujerumani na timu ya wanaharakati wa Afrika Mashariki kujifunza masuala ya kijamii. Tulitembelea maeneo mengi ya Magharibi na Mashariki. Maeneo ninayoyakumbuka ni Dusseldorf, Cologne, na Bonn katika jimbo tajiri la North-Rhine Westphalia, kisha Hess, Dresden, Saxony (Leipzig) na Berlin. Tulizunguka kwa boti za kifahari katika mto Rhine na Danube na kuishi kwenye hoteli za kifahari na kisasa.

Wakati sisi tukishangaa hatua kubwa ya kiuchumi na kimaendeleo waliopiga Wajerumani, wao walitushangaa jinsi tunavyopoteza rasilimali muda. Kila tulipokuwa tunaingia ukumbini kwenye mafunzo, kuna mtu alikuwa anasimama mlangoni na kuhesabu dakika ambazo kila mmoja kachelewa. Wapo tuliopoteza dakika 2, 10, 20 na wengine nusu saa nzima.

Mwisho wa mafunzo yetu kila mtu alihesabiwa muda alioupoteza kila siku na kwa kipindi chote tulichokaa. Wengine walipoteza jumla ya saa 2, wengine saa 4 hadi 6. Japo hatukukemewa, lakini walitujulisha kazi ambazo tungeweza kufanya kwa mafanikio kwa kutopoteza saa zote hizo bure. Niliumia sana! Lakini nikabaini kwanini wao wameendelea sana Ulaya, huku sisi tukipiga soga vijiweni na kushupalia mizaha, tetesi na umbea.

Inauma zaidi kukuta watu wakipiga soga kwenye ofisi za umma. Wengi hutumia simu zao au kompyuta za serikali kupakua na kupakia udaku mitandaoni. Wengine muda mwingi hukodolea macho tamthiliya kwenye televisheni zilizotundikwa ofisini. Tumegeuza ofisi za umma kuwa vijiwe huku wateja wakisubiri huduma kwa foleni nje. Pongezi nyingi kwa Waziri William Lukuvi aliyekesha akitatua migogoro ya ardhi. Wenzetu Japan wameendelea sana, ni nchi ya pili kwa uchumi mkubwa duniani. Lakini hawaruhusu wafanyakazi wao kuwa na simu ofisini au kutazama runinga.

Aidha kuna haja ya kufanya kazi kwa zamu (shift) kati ya mchana na usiku ili kuondokana na mazoea ya wote kuamka wakati mmoja asubuhi na wote kurudi nyumbani wakati mmoja jioni. Utaratibu huu utapunguza sana foleni. Kwa kuanzia, napendekeza tuwe na zamu mbili za wafanyakazi wanaoanza kazi saa 2 asubuhi na kutoka saa 10 jioni kama ilivyo ada.

Kisha wawepo wanaoanza saa 2 usiku na kutoka saa 10 alfajiri. Tutakuwa tunapishana njiani badala ya sasa ambapo karibu watu wote Dar es Salaam asubuhi huelekea upande mmoja, huku upande mwingine wa barabara ukiwa tupu na mabasi ya abiria matupu. Zamu hizi kwa kiasi kikubwa zitapunguza sana foleni, misongamano na kuukomboa muda tunaoupoteza.

Sambamba na hilo, tutawasaidia sana wazazi wanaotoka asubuhi kwenda kazini watoto wakiwa bado wamelala na kurudi nyumbani watoto wakiwa tayari wamelala. Hawana muda asilani wa kukaa kifamilia. Ikiwezekana, hata masoko makubwa, maduka makubwa (supermarkets and shopping malls), benki, ofisi za mamlaka ya mapato (TRA) ziwe wazi 24/7 – yaani saa 24 kwa juma. Watu watapishana na kujipangia muda wao bila foleni wala msongamano. Kama imewezekana kwenye baadhi ya vituo vya afya, sioni kwanini isiwezekane kwenye ofisi za umma na maeneo mengine.

Muda ni rasilimali muhimu na adhimu, ni mtaji. Ni rasilimali ambayo hupotea na kuisha kila sekunde, dakika, saa, siku, juma, mwezi na mwaka; si rahisi kuirejelea upya. Marafiki zetu wengi wanatupotezea muda au sisi tunapoteza muda wa marafiki zetu na kuleta hasara. Vijana wengi hukaa vijiweni wakipiga soga ambazo haziwasaidii katika maisha yao. Watabishana kucha-kutwa kuhusu wachezaji mpira au timu maarufu za Ulaya wakati wenzao wanacheza na kuingiza kipato kikubwa kwa kila juma.

Wazee watakaa barazani kucheza bao au kweda vilabuni kunywa pombe wakati wenzao wako mashambani au wanajishughulisha na ujasiriamali. Miaka ya hivi karibuni, tumeona watu wengi wakikesha na simu zao wakifuatilia masuala ambayo hayawaingizii kipato chochote au kuwaelimisha. Wako tayari kukosa usingizi wakifuatilia vituko na udaku wa mitandaoni huku wenzao wakikesha kuzalisha mali.

Ukienda nchini China, Wachina na watu wengine wanaoishi huko, muda wote wa mchana na usiku huutumia kuzalisha mali. Kuna baadhi ya watu wameajiriwa sehemu moja kufanya kazi mchana na sehemu nyingine wameajiriwa kufanya kazi usiku. Wanakuwa na ajira mbili tofauti kwa siku moja. Waliojiajiri nao biashara zao ziko wazi saa 24. Hakuna kulala!

Hivi ninavyoandika makala haya, nimeamka saa 10 alfajiri, na najua wengine wameamka kwenda mashambani, kwenda kuvua samaki au kwenda kazini. Lakini kuna wengine pia ambao wanavuta blanketi na huenda wataamka saa 3 au saa 4 asubuhi. Usingizi ni mzuri kwa ajili ya kupumzisha mwili tu, si kwa ajili ya kuulemaza na kupoteza muda wa uzalishaji mali.

Hitimisho

Miaka tulionayo hapa duniani ni michache sana, inatoweka upesi. “However, what significantly matters in life is not the amount of years we put into life, but the quality of life we put into years.” Namaanisha kuwa: “Hata hivyo, thamani ya maisha haiko katika idadi ya miaka tunayoishi, bali iko katika ubora wa maisha katika miaka tunayoishi.”

Kuna watu wanaishi muda mrefu sana hapa duniani lakini hakuna cha maana wanachofanya, wala kumbukumbu zao hatuna. Kuna watu wanaishi muda mfupi lakini hufanya mambo makubwa na yenye faida kwao na jamii. Kila mara tujihoji endapo muda tunaoutumia kufanya jambo fulani unaleta mafanikio katika maisha yetu. Si kila jambo tunalolizingatia lina maana, na si kila jambo lenye maana linapaswa kuzingatiwa. Unaweza ukazingatia sana kuangalia mpira lakini usiwe na maana kwako. Usipate faida yoyote!

Unaweza ukaona kuna maana kupitia kwenye kilabu au baa, lakini ukizingatia sana hilo na kujiwekea ratiba ya kila siku, utapoteza muda muhimu sana kwako na kwa familia yako. Kitu pekee chenye maana na cha kuzingatiwa ni muda tunaoutumia kuzalisha mali au kujenga mahusiano mema ya kifamilia na kijamii.

Nihitimishe kwa kuishauri serikali kuondoa televisheni zote zilizotundikwa kwenye ofisi za umma. Aidha, wafanyakazi wote wa umma wawe wanaacha simu zao nyumbani au mlangoni nje ya ofisi. Zitumike simu za mezani tu.

TANBIHI: Makala hii imeandikwa na Gwandumi Gwappo A. Mwakatobe, mchambuzi huru wa masuala ya kitaifa na kimataifa, anayeishi Mwakaleli, Busokelo, Rungwe, Mbeya. Anapatikana kwa anuani ya baruapepe: gwandumi@hotmail.com au gwappomwakatobe@gmail.com

 


Filed under: JAMII Tagged: mafanikio, mitaji, muda, ujasiri amali

Nguzo ya 8 ya mitaji ya mafanikio ni mahusiano mema

$
0
0

Pamoja na kufahamu mambo kadhaa ya kufanya peke yangu bila msaada, bado kilichoniwezesha kuandika na kutoa makala haya ni mahusiano mema. Tumezaliwa kutokana na mahusiano, tena mazuri sana, baina ya mama na baba. Tumelelewa katika mahusiano, tumesoma kupitia mahusiano na mawasiliano, na tunafanya kazi mbalimbali kutokana na mahusiano na watu wengine waliotuunganisha. Kila mmoja anaye mtu na/au watu waliomfanya awe mahali alipo na kazi anayofanya. Bila hao tusingekuwa hapo tulipo leo.

Hakuna awezaye kufanikiwa katika jambo lolote pasipo kuhusika au kuhusisha watu wengine. Hata biashara unayofanya inastawi kutokana na mahusiano yako mazuri na wafanyabiashara wengine pamoja na wateja wako. Na kwa kubaini hilo, hakuna mtu anapinga kuwa mahusiano mema ni mojawapo ya nguzo za mitaji ya kutufanikisha katika maisha yetu.

Umuhimu wa mahusiano mema kijamii

Mahusiano mema si kufanya kazi pamoja, kuishi pamoja, kuzaliwa pamoja, kusoma shule pamoja, kuwa na imani ya kidini moja, asili moja, kabila moja, rangi moja, kuoana au kuungana pamoja; la hasha. Mahusiano mema ni kumjali mwingine na kumpa nafasi sawa yenye kuleta faida na usawa kwa watu wawili au pande mbili zinazohusiana. Mnaweza mkaishi pamoja, mkasoma shule moja na kulala kitanda kimoja; lakini msiwe na mahusiano mema hata kama ni mapacha. Kila mtu akawa kivyake!

Aidha, mahusiano mema si lazima kuwa na urafiki. Mtu anaweza asiwe rafiki yako lakini pia asiwe adui yako kutokana na kuwepo uhusiano mzuri. Siku hizi tunasema tumeendelea sana na kustaarabika, na wengine kukiri kuwa dunia imekuwa kama kijiji kutokana na maendeleo ya kiteknolojia. Lakini kila mtu anazidi kuishi kibinafsi kivyake, mahusiano yanafifia au kutokweka kabisa. Na wengine wamekuwa wapweke katikati ya umati wa watu kwa kuwa tu hawana mahusiano mema na wengine.

Tumejenga maghorofa makubwa na marefu yakiwa na vyumba vingi vya kuishi pamoja kwa ukaribu, lakini kwa sehemu kubwa kila mtu yuko kivyake kwa kukosa mawasiliano na/au mahusiano na wengine. Hatuko karibu kama kijiji. Mara kadhaa imetokea mtu anakufa peke yake chumbani – mpweke! Watu wa vyumba jirani hawajuani wala hawasalimiani. Tukiri kuwa teknolojia bado haijaweza kutuleta pamoja.

Ukipanda basi, kila abiria yuko na simu yake. Ukirudi nyumbani kila mwanafamilia yuko simu yake. Ukienda mkutanoni kila mtu yuko na simu yake, anaparaza anayoyajua yeye. Wengine hudai simu zimetutenganisha na kutufarakanisha, hakuna mahusiano. Kama tungekuwa tunahusiana vema sisi kwa sisi kwa ukaribu kama tulivyo karibu na simu zetu, naamini magomvi, mitafaruku na hata vita visingekuwepo duniani.

Unyonyaji unaoendelea duniani, unatokana na uchumi kuwa mikononi mwa watu wachache wanaomiliki na kujirundikia utajiri wasiokuwa na haja nao, wakati wengine wanakufa kwa ufukara wa kutisha. Yote haya ni kutokana na kutokuwa na mahusiano mema ya kiuchumi. Tutambue kuwa bila rasilimali asilia za nchi zinazoitwa maskini, leo hii hatuwezi kuwa na nchi tajiri ambazo hutegemea sana rasilimali hizo. Lakini hakuna urari wowote na/au mahusiano mema.

Tukitambua umuhimu wa kila mtu au kila taifa kuhusiana vema pasipo unyonyaji, unyonywaji, ubaguzi, uonevu na ukandamizaji; hatutakuwa na matabaka ya watu au pengo kubwa kiuchumi baina ya watu wenye mali nyingi na wenye ufukara mwingi duniani. Kila mtu anamhitaji mtu mwingine ili aendelee na kustawi na kila taifa linalihitaji taifa lingine ili liendelee na kustawi.

Kila mtu ana thamani katika nafasi yake kwa kiwango chake cha kutumikia wengine na wengine kumtumikia yeye. Tungekuwa tunaelewa umuhimu na mchango wa kila mtu katika jamii na taifa, mahusiano yafuatayo kimaisha yangekuwa dhahiri:

  • Mwenye nyumba asingemwonea mfanyakazi wake wa ndani.
  • Mwenye gari asingemdharau mwenye mkokoteni au mbeba mizigo.
  • Mwenye kazi za ofisini asingemkebehi mkulima.
  • Mwenye elimu asingemdharau mjinga.
  • Mwenye shibe asingemhukumu mwenye njaa.
  • Mwenye afya njema asingemcheka mwenye udhaifu – mgonjwa.
  • Mwenye utajiri asingemdhihaki mwenye umaskini.
  • Mwenye uwezo wa kuajiri asingemnyanyasa mwajiriwa.
  • Mwenye umaarufu asingemdharau mtu wa kawaida (commoner).
  • Mtawala asingemkandamiza mtawaliwa.

Kiongozi angemjali sana anayemwongoza kwa kuwa kiongozi bora pia huongozwa na anaowaongoza. Vivyo hivyo, mataifa nayo endapo yangekuwa yanahusiana vizuri pasipo kunyonyana:

  • Tusingekuwa na nchi za kinyonyaji na za kinyonywaji.
  • Tusingekuwa na dunia ya kwanza, ya pili wala ya tatu.
  • Tusingekuwa na nchi tajiri wala maskini.
  • Tusingekuwa na nchi zinazokopesha na zinazokopeshwa.
  • Tusingekuwa na nchi kubwa wala ndogo kiuchumi.

Tusingekuwa na matabaka ya watu na ubaguzi wa rangi.

Tungejua vema nafasi na mchango wa kila nchi katika ustawi wa dunia yetu, basi tungekuwa na nchi zinazosifika kwa viwanda na nchi zinazothaminiwa na kuheshimika kwa kuzalisha malighafi za viwandani. Hata watumwa waliopelekwa Amerika, Asia na Ulaya kutoka Afrika hadi sasa wangekuwa wanaheshimika na kukumbukwa kwa jinsi walivyojenga miundombinu ya reli na majengo makubwa, na walivyolima mashamba makubwa ya miwa kwa ajili ya kuzalisha sukari. Waafrika na Afrika yetu tungekumbukwa tulivyotoa rasilimali watu na rasilimali vitu kuendeleza mataifa hayo.

Mtu mweusi toka Afrika kamwe asingedhalilishwa na kubaguliwa kwa rangi yake, bali angepewa heshima ya mchango wake na utu wake duniani. Na kwa kusema hivyo, lazima Afrika ijue kuwa bila sisi Waafrika, wazungu na wengineo hawawezi kuendelea pasipo sisi. Tukigoma kuruhusu rasilimali zetu kuvunwa, nchi nyingi za Asia, Ulaya na Marekani zitakwama! Sehemu kubwa ya maendeleo ya Ulaya, Marekani na Asia hutegemea utajiri wa Afrika na nguvukazi ya Waafrika.

Tungeelewa vema na kuthamini umuhimu na mchango wa kila nchi duniani tusingekuwa na nchi zinazojidai kwamba zinajitegemea na nchi zinadaiwa kuwa ni tegemezi. Bali tungekuwa na nchi zinazotambua kutegemeana. Hakuna nchi kubwa au inayojidai kuwa ni tajiri na iliyoendelea bila kutegemea au kushirikiana na nchi zingine zinazodaiwa kuwa ni ndogo na maskini. Tungetambua kuwa mahusiano mema ndio ukweli na uhalisia wa maisha yenye staha, basi tungeelewa kuwa kila nchi, ndogo au kubwa, tajiri au maskini, ina vitu vya kuisaidia nchi nyingine. Bila nchi maskini haiwezi kuwepo nchi tajiri na ndivyo ilivyo kinyume chake.

Na kwahiyo, hakuna nchi ndogo au kubwa kuzidi nyingine, wala hakuna nchi maskini au tajiri kuliko nchi nyingine, bali kila nchi inaihitaji nchi nyingine ili iweze kuendelea. Kama ni utajiri, kila nchi ina utajiri wake, kama ni umaskini kila nchi ina umaskini wake, yaani kile kitu ambacho nchi inakikosa hukipata kutoka nchi zingine. Tunategemeana kwasababu tunatofautiana katika kumiliki rasilimali vitu, rasilimali watu, mazingira, utamaduni, maarifa na teknolojia. Ufahamu huu ndio njia pekee ya kuundoa unyonyaji, ukandamizaji, uonevu na ubaguzi mkubwa ulioshamiri na unaozidi kushamiri duniani.

Migogoro mingi na vita vingi duniani kwa sehemu kubwa havitokani na tofauti zetu za imani za kidini bali hutokana na tofauti zetu kiuchumi, huku kila mmoja akishindana kumnyonya, kumpora na kumzidi mwingine. Kuna watu wachache au nchi chache sana duniani hufaidi rasilimali za dunia kwa mgongo wa watu wengine au nchi nyingine zinazotumika au kutumikishwa kuinua nchi hizo. Ushindani kiuchumi umegeuka kuwa uporaji na kuendeleza umaskini duniani.

Kwa kudhihirsha hoja zangu, mataifa mengi yanayodai yameungana, yamegundua kuwa yananyonyana na kutawalana tu. Mathalani, Uingereza ilijitoa umoja wa Ulaya ikidai haina uhuru wa kuamua mambo yake, eti inanyonywa na kupangiwa kila kitu na watu wa Umoja wa Ulaya walioko Brussels (Ubelgiji). Mwaka jana Waingereza walijitoa kwa kampeni kali iliyoitwa Brexit. Kumbe nchi za Ulaya nazo zimeungana lakini hazina mahusiano mema. Afrika tunao Umoja wetu (AU) lakini hatuko pamoja, hatuna mahusiano mema, kila nchi iko kivyake na utawala wake.

Tanganyika na Zanzibar ziliungana Aprili 26, 1964; lakini kiuhalisia waliungana na hadi sasa wameungana watawala. Muungano haukutokana na ridhaa ya wananchi. Watu wa pande hizi mbili kwa sehemu tunajiona hatuna mahusiano mema na yenye usawa. Wazanzibar wanalalamika miaka nenda rudi, na sasa miaka 53, kuwa wanapunjwa, wanakandamizwa, hawana fursa kitaifa na kimataifa kwasababu ya muungano uliopo.

Kuna watu hubaguliwa kama wabara na wengine wapemba. Mbaya zaidi hata ndani ya Zanzibar yenyewe, kuna watu wanaona mchotara si Wazanzibar, eti Zanzibar ni ya weusi. Bila soni huinua mabango mchana kweupe ya kuwatenga machotara. Ni kisiwa kimoja bila mahusiano mema. Vyama vya siasa navyo vinatufanya tubaguane na hata kuhasimiana vibaya.

Kuungana kwa Tanganyika na Zanzibar kuwe kwa misingi ya mahusiano mema na udugu. Kuwa karibu au jirani si hoja. Leo tuna mahusiano mema na Kuba (Cuba) lakini iko magharibi ya mbali kabisa na Tanzania. Japani iko mashariki ya mbali sana na Tanzania lakini tuna mahusiano mema na ya karibu. Mnaweza mkawa majirani lakini mkawa mbali kabisa kimahusiano na kuwa na utengano badala ya utengamano. La sivyo tusingepigana na Idd Amini Dada maana Uganda ni jirani.

Naamini endapo kweli tunawapenda Wazanzibar hatuwezi kuwazuia kupata mamlaka, hadhi, haki na fursa yao kitaifa na kimataifa kwa kuwa ni ndugu zetu wa asili, wa damu, na zaidi sana ni Waafrika wenzetu. Napenda Zanzibar ipate hadhi ya kidola na kitaifa, na hakika itakuwa faida kwetu sote – Tanganyika na Zanzibar.

Korea ilikuwa nchi moja, watu wa asili moja, rangi moja na lugha moja, lakini waliingia katika mahusiano mabaya na kusababisha vita mbaya kabisa hadi kutengana Kaskazini na Kusini kwa misingi ya tofauti za itikadi za kisiasa. Hadi leo kuna uhasama mkubwa mno huku majeshi ya pande mbili yakiwa mpakani toka mwaka 1953 tayari kwa kushambuliana wakati wowote. Ndugu wa damu na familia moja walitenganishwa na hakuna kuonana hadi kwa ruhusa maalum ambayo haitokei kwa kipindi kirefu. Hata ikitokea wanaonana kwa muda mfupi na kuachanishwa.

Vivyo hivyo, Somalia sehemu kubwa wana imani moja ya kidini, kabila moja, lugha moja, asili na rangi ya aina moja. Lakini wanatwangana kila siku kwa misingi ya tofauti za kiukoo. Hata wangekuwa ukoo mmoja nchi nzima, pasipo mahusiano mema bado wangetwangana. Hakika mahusiano mabaya na yasiyo na urari ni kiini cha migogoro mingi duniani.

Hitimisho

Ili kuwa na mahusiano mema tunapaswa kuziishi sifa zifuatazo: kuwaza mema, kutolaumu sana, kutosengenya, kuwakubali wanaofanya mema na kutowahukumu sana wanapokosea, kuwa wasikivu kabla ya kusema lolote, na kupenda kusaidiana na kufaidiana kwa usawa. Maisha ni mazuri ikiwa hatuchoki kutenda wema, kuhurumiana, kuheshimiana na kujaliana. Ulimwengu huu utakuwa mahali pazuri pa kuishi endapo tutakazana kuwatendea wengine mema kama ambavyo nasi tungependa kutendewa mema. Na hakuna asiyependa kutendewa mema – hakuna, hata dhalimu!

Mahusiano mema hutufundisha kuhusu sisi wenyewe. Kama unamwangalia mtu na kuhisi au kugundua mambo ambayo hayafai kwake, unakuwa umejigundua wewe mwenyewe kwa kuwa tunafanana. Ni sawa na kujiangalia kwenye kioo, unayemwona ni wewe mwenyewe. Makosa tunayoyaona kwa wengine ndiyo tuliyonayo, na mazuri tunayoyaona kwa wengine ndio tupasayo kufanya. Tusimhukumu sana mtu akikosea bali iwe nafasi ya kujiona tulivyo. Na kwahiyo tutatangulia kwanza kujisahihisha wenyewe ndipo tuwasahihishe wengine kwa ustaarabu kwa kuwa ndivyo tulivyo sote.

Mtu anayepigana vita nzuri ni yule anayejishinda mwenyewe kwanza, si anayemshinda mwingine. Ni yule anayeshinda chuki ndani yake, wivu mbaya ndani yake, mawazo mabaya ndani yake, kiburi ndani yake na udhalimu ndani yake. Ndiposa tutaweza kuwasaidia wengine baada ya kujisaidia sisi wenyewe kwanza.

Nihitimishe kusema kuwa kwa usalama wako, waheshimu watu wote ili uwe na mahusiano mema nao, lakini waamini wachache (respect all, trust few).

TANBIHI: Makala hii imeandikwa na Gwandumi Gwappo A. Mwakatobe, mchambuzi  huru wa masuala ya kitaifa na kimataifa, anayeishi Mwakaleli, Busokelo, Rungwe, Mbeya. Anapatikana kwa anuani ya baruapepe: gwandumi@hotmail.com au gwappomwakatobe@gmail.com


Filed under: JAMII Tagged: mahusiano. mafanikio, ujasiriamali

Uhuru Kenyatta: Mtu mzima akivuliwa nguo, huchutama 

$
0
0
 Ni bahati mbaya sana kwa Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya kuwa majaji wa Mahakama ya Juu wameamua kuufuta ushindi wa asilimia 54 aliotangaziwa na Tume ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kwenye uchaguzi wa Agosti 8 wakisema haukuwa halali na kwamba uchaguzi mpya lazima ufanyike ndani ya siku 60 kuanzia tarehe 1 Septemba 2017.

Bahati mbaya zaidi kwake ni kwamba sasa anaanza kuacha njia safi aliyokuwa akitembea na anaingia machakani. Onyo la mapema kwake ni kuwa huko maguguni anakojitia, atakuja kukujutia katika wakati ambao atakuwa ameshachelewa, maana majuto ni mjukuu, daima huja mwishoni.

Awali alikuwa ameanza kubebeshwa sifa za kuwa “Baba wa Demokrasia barani Afrika” kwa kauli zake za awali za kuunga mkono maandamano ya wapinzani waliokuwa hawakuridhishwa na ‘ushindi’ huo na baadaye hata kusema angeliuheshimu uamuzi wa Mahakama ya Juu kuufuta ushindi wake ingawa hakuridhika nao.

Lakini masaa machache baada kuhutubia taifa akiwa Ikulu ya Nairobi akiwa amesisitiza umoja, udugu na amani ya Wakenya, Rais Kenyatta akaelekea mitaani na huko ndiko alikoanza kuonesha rangi tafauti na ile aliyokuwa kajipakaza mwanzo.

Na Mohammed Ghassani

Kwenye mitaa ya Nairobi na Nakuru, Rais Kenyatta alizungumza lugha ya kibabe, lugha ya kupotosha na kupotoka na, baya kuliko yote, lugha ya kutisha na kuchonganisha.

Anawaita majaji wa Mahakama ya Juu kuwa ni “wakora”, neno la Kiswahili cha Kenya linalomaanisha watu wakorofi wasiokuwa na maana.

Anamtisha Jaji Mkuu David Maranga kwamba asijidhani akishavaa joho la ujaji anakuwa na nguvu ya kuogopwa.

Anajilabu kuwa akina Jaji Maranga wanapaswa kujuwa kuwa kwa uamuzi wao huo, sasa yeye, Uhuru Kenyatta, ni rais aliyepo madarakani na si rais anayesubiri kuapishwa tena.

Anauita uamuzi wa Mahakama hiyo ya Juu kuwa ni kauli ya watu wanne watano wasiochaguliwa wanaokiuka matakwa ya Wakenya milioni 15 waliompigia yeye kura.

Zaidi ya yote, anaitishia idara nzima ya mahakama kwamba ina tatizo na ambalo wakimaliza uchaguzi ulioitishwa atalishughulikia. Tatizo ni kutoa uamuzi wa kufuta ushindi wake wa Agosti 8, uliokuwa na utata.

Kwenye hotuba yake mbele ya magavana wa chama chake cha Jubilee, Kenyatta anafikia umbali wa kumtisha Jaji Maranga kwamba asithubutu kuingilia majukumu ya IEBC, licha ya kuwa mahakama ina wajibu wa kusikiliza hoja za wale wanaoamini kuwa Tume hiyo imepoteza uaminifu wake mbele ya umma.

Sasa hapa Kenyatta lazima aambiwe naye aambilike kuwa amefika mbali. Muelekeo aliokuwa amechukuwa mwanzoni ulikuwa sahihi na ulimpatia heshima na sifa kutoka kwa kila mpenda amani, haki na demokrasia.

Ikiwa kweli ni muumini wa demokrasia na utawala wa sheria, kama ambavyo awali alitufanya tumuamini, kauli zake hizi za sasa zinamuweka mbali sana na sifa hizo.

Kwa kauli hizi za kibabe, sasa Kenyatta anajiweka kwenye kundi moja na watawala wenziwe wa Afrika Mashariki na Kati, akina Yoweri Museveni wa Uganda, Paul Kagame wa Rwanda, Pierre Nkurunziza wa Burundi na John Magufuli wa Tanzania, ambao hupenda kujikweza juu ya mihimili yote ya utawala, wakiamini kuwa wao ndio mwanzo na mwisho.

Wengine hata wanahoji kuwa Kenyatta sasa anathibitisha rangi yake halisi – ya mtoto wa kitajiri aliyelelewa na kukulia Ikulu akidekezwa mno na wazazi wake kiasi cha kwamba haujuwi msamiati wa kukosa. Neno “sina” kwake yeye halimo kwenye kamusi. Ni mwana akipataye akitakacho kwa namna yoyote ile.

Gazeti la Daily Nation la tarehe 3 Septemba lilichapisha habari ya uchunguzi inayoonesha kuwa kumbe maafisa wa serikali na chama tawala cha Jubilee walikuwa wamejaribu, bila mafanikio, kuwafanya majaji watowe uamuzi ambao ungeibeba IEBC naye Kenyatta.

Hata kauli yake ya kuwaita majaji wa Mahakama ya Juu “wakora” inaakisi kuwa kiongozi huyo amekasirishwa kupita kiasi na kuona kuwa kanyimwa anachoamini ni chake peke yake, miliki yake.

Kauli hii pia imewakumbusha Wakenya na wanaofuatilia siasa za Kenya ile kauli ya baba yake, Marehemu Mzee Jomo Kenyatta, dhidi ya wapinzani wake, aliyekuwa akiwaita “vinyangarika!”

Hapana shaka, wanaomsema hivyo wanapuuzia ukweli kuwa huyu ni mpambanaji mwenye mbinu na mikakati yake, ambaye kukulia kwake Ikulu kulimpa wasaa wa kujinoa kisiasa.

Lakini, kwa vyovyote viwavyo, Uhuru Kenyatta ameteleza pakubwa na bahati mbaya kwake ni kuwa juu ya kichwa chake panatembea bango la kuwahi kutuhumiwa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) kwa jukumu lake katika machafuko ya mwaka 2007 yaliyoangamiza maisha ya Wakenya zaidi ya 1,000, kuwajeruhi kadhaa na maelfu ya wengine kugeuzwa wakimbizi wa ndani.

Ingawa mashitaka dhidi yake yalilazimika kufutwa na Mahakama hiyo, lakini si kwa kuwa waendesha mashitaka walishawishika kuwa Kenyatta hakuwa na kesi ya kujibu.

Mwezi Aprili mwaka huu wakati nikihudhuria mkutano wa utawala bora barani Afrika uliofanyika mjini Marrakesh, Morocco, nilimuuliza Mwendesha Mashitaka Mkuu wa ICC, Fatou Bensouda, juu ya kushindwa kwake kwenye kesi ya akina Uhuru Kenyatta, na jibu lake lilikuwa moja tu: “Hatukushindwa na kesi haikufungwa. Muda wowote hali ikiruhusu, tutairejesha mahakamani!”

Lau ni kiongozi wa mfano – kama ambavyo alianza kuchukuliwa na wengine, basi Kenyatta ana siku za kuyameza matapishi yake na kuomba radhi kwa Wakenya na Waafrika Mashariki wote waliomchukulia kuwa kigezo chema.

Kenya haimuhitaji Kenyatta asiyeihishimu Mahakama. Afrika Mashariki haina haja ya kuendeleza tawala za viongozi wasiopima athari za kauli na matendo yao.
TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la Mwelekeo la tarehe 5 Septemba 2017

 


Filed under: KALAMU YA GHASSANI Tagged: Jubilee, Kenya, Kenyatta, Mahakama ya Juu, NASA, Raila Odinga

Funzo la uamuzi wa Mahakama ya Juu ya Kenya ni kuwa demokrasia hujengwa kutokea ndani, sio nje

$
0
0

Uamuzi wa tarehe 1 Septemba 2017 wa Mahakama ya Juu ya Kenya kuufuta uchaguzi uliompa ushindi rais aliye madarakani na kuamuru kurejewa upya, umezua maoni mengi na yanayofanana ndani na nje ya taifa hilo la Afrika Mashariki.

Miongoni mwa hayo yanayofanana ni kumwagiwa sifa kwa Jaji Mkuu David Maranga kwa kuamua kwa haki – kuna waliomfananisha na Mfalme Suleiman (amani ya Mungu iwe juu yake), ambaye anasifika kwa kuwa muamuzi muadilifu wa kesi za raia wake.

Mfanano pia ni kwenye hongera kwa kiongozi wa upinzani Raila Odinga na timu ya wanasheria wake kwa kupigania haki yao mahakamani – kuna waliomfananisha na Mtume Daud (amani ya Mungu iwe juu yake), ambaye alisimama imara dhidi ya jitu kubwa, Goliathi, na kuliangusha chini kwa teo.

Na bila kusahau, kuna mfanano wa maneno ya heshima aliyopewa Rais Uhuru Kenyatta kwa kuruhusu demokrasia na utawala wa sheria uchukuwe mkondo wake – kuna waliompachika jina la ‘Baba ya Demokrasia barani Afrika‘.

Sehemu nyengine ya maoni haya yanayofanana ni upande wa lawama na kunyoosheana vidole. Kwanza kwa maafisa wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka ya Kenya (IEBC) waliosababisha uchaguzi huo kuharibika na kufutwa, pili, kwa chama tawala cha Jubilee kwa kushawishi uharibifu huo na, tatu, kwa waangalizi wa ndani na nje walioubariki uharibifu huo, hata kabla ya kufanya utafiti wa kutosha.

Na Mohammed Ghassani

Nitajizuwia kupita humo wanamopita wenzangu, kwenye sifa na lawama, na nitaelekeza mchango wangu kwenye funzo moja tu miongoni mwa mafunzo mengi muhimu ambayo mataifa ya Afrika Mashariki na Kati yanaweza kuchota kutokana na hatua hii yenye maana kubwa kwa eneo hili zima.

Kama kuna jambo moja muhimu kabisa la kukopa kutoka kwa Wakenya kwenye hili, basi ni la kutufanya tukubali kivitendo kwamba demokrasia na utawala wa sheria hujengwa kutokea ndani ya taifa husika, na wala sio kutokea nje yake.

Kilichomfanya Odinga na wenzake kutoka muungano wa upinzani (NASA) kukimbilia mitaani na mahakamani, si kigeni ndani ya eneo zima la mashariki, kati na kusini mwa Afrika.

Ni kile kile kilichojiri Burundi mwezi Julai 2015, Tanzania na Zanzibar mwezi Oktoba 2015, Uganda mwezi Februari 2016, Zambia mwezi Agosti 2016, Rwanda mwezi Agosti 2017, na ambacho kimekuwa hivyo hivyo kwa muda mrefu.

Ni ile hali ya watawala wameziteka nyara chaguzi zilizotakiwa ziwe za kidemokrasia na kuzitumilia kuwa kichaka cha kujitawalisha milele madarakani, hata pale ambapo wananchi wanawakataa.

Safari hii, Odinga aliamini ametendewa hayo hayo na wale aliowaita watotoaji wa “vifaranga vya kompyuta“. Mfumo wa matokeo ya uchaguzi wa Agosti 8, alihoji, ulikuwa umechezewa tangu mapema kumnufaisha mpinzani wake mkuu, Rais Kenyatta.

Wakati anatoa madai hayo, tayari waangalizi wa uchaguzi huo kutoka taasisi zinazoheshimika duniani, kama ile ya Jimmy Carter ya Marekani, walishaupa sifa uchaguzi huo kuwa huru na wa haki.

Baya zaidi, waangalizi wengi sana wakaenda mbali zaidi kumtolea wito Odinga ayatambuwe matokeo hayo na kama ana la ziada basi aende mahakamani, ingawa wenyewe wakijiaminisha kuwa Odinga hakuwa na kesi madhubuti ya kuwakilisha, maana uchunguzi wao ulikuwa unaonesha kila jambo liko sawa.

Kama Odinga angewasikiliza akina John Kerry wa Carter Center, basi leo hii Waafrika Mashariki wanaofurahikia uamuzi huu wa Mahakama ya Juu ya Kenya, wasingelikuwa na cha kufurahia, na badala yake msiba ule ule kwa demokrasia ya eneo hili ungelikuwa umejirejea.

Na haikuwa mara ya kwanza kwa Odinga kuamini uchaguzi ‘umechakachukuliwa‘ kwa maslahi ya watawala, na angalau ilikuwa mara ya pili kuamini kwenda mahakamani kupeleka malalamiko yake.

Mara ya kwanza ilikuwa ni mwaka 2013, ambapo baada ya kile kilichoonekana kama “mahakama kwa ajili ya amani“ (peace judiciary), Odinga akabwagwa chini.

Wakati huo ilikuwa ni miaka mitano tu baada ya mauaji ya 2007 na nchi ikawa kwenye mazingira ya kuhofia kujirejea kilichotokea hapo awali.

Wenyewe, Wakenya, wanasema sio tu majaji, bali hata waandishi wa habari, wote, walikuwa kwenye ‘peace journalism‘ – uandishi wa habari kwa ajili ya amani.

Kwa maslahi ya amani, kwa hivyo, kila mtu akawa anaona bora tu mambo yaende kama yaendavyo lakini pasiwe na damu itakayomwagika.

Hata Odinga, licha ya kutokuridhika na uamuzi huo wa mahakama, akakubali kurejea kwenye kitu cha upinzani, kutoka nafasi ya uwaziri mkuu wa nchi aliyokuwa nayo kabla ya hapo.

Hiyo haimaanishi kwamba hakuwa na njia nyengine ya kufanya. Alikuwa nayo. Siasa za ndani kupitia umma.

Miaka miwili baada ya Odinga kushindwa kesi ya 2013, nilikutana na mmoja wa majaji waliokuwemo kwenye kesi hiyo jijini Nairobi. Nilitambulishwa kwake na rafiki yake mkubwa ambaye nami ni rafiki yangu.

Nikatumia fursa hiyo kumuuliza la kesi ile, naye akanijibu kwa kutumia mkasa tafauti wa walimu waliokuwa wakigoma na wakawa wameshinda kiwango fulani cha madai yao mahakamani, lakini yeye mwenyewe jaji huyo, akamuambia mmoja wa viongozi wa mgomo huo kuwa: „“Sasa mshahinda mahakamani, kauendelezeni ushindi wenu mitaani kuhakikisha kuwa kilichoamuliwa mahakamani kwa manufaa yenu, kinatimizwa. Mkilala, hapana kitakachotekelezwa!“

Lakini hadi kufikia mahala pa kwenda mahakamani, Wakenya wamepitia mengi kuijenga hiyo mahakama yenyewe. Yakiwemo mapambano ya kuipata katiba mpya mwaka 2010.

Ukimsikia leo Rais Kenyatta akiwaambia wapinzani: “Andamaneni mtakavyo, muhimu tu msiharibu mali na kuumiza wengine!“ si kwa kuwa Kenyatta ni mwanademokrasia sana, bali ni kwa kuwa Wakenya walipigania na kujenga taasisi imara za kusimamia demokrasia na utawala wa sheria, ambazo lazima yeye aziheshimu akataka asitake.

Huwezi kuwa na wapinzani ambao wanapangiwa na mtawala namna ya kumpinga nao wakawa wanamfuata mtawala huyo atakavyo, kisha ukatarajia kusimama kwa taasisi imara za kidemokrasia na utawala wa kisheria.

Huwezi kuwa na upinzani ambao unashiriki uchaguzi, unashinda kura lakini unaamini kuwa baada ya kuibiwa kura zao, haki hiyo itarejeshwa na waangalizi wa kimataifa, bila ya wenyewe kuendeleza shinikizo hilo, na bado ukatazamia kuna siku kura itakuwa na maana kwenye maisha ya watu.

Odinga aliwakaidi waangalizi wa kimataifa, wakiwemo wa mataifa makubwa ya Marekani  na Uingereza, na akawaambia mbele ya macho yao: “Shame on you!“ – Nyie musiokuwa na haya!

Wakati wao wakisisitiza kuwa uchaguzi ulikuwa huru na wa haki, Odinga alishikilia kuwa matokeo yaliyotangazwa na IEBC yalikuwa “vifaranga vya kompyuta“ na kwamba angeliwathibitishia hivyo.

Hii ni kwa kuwa, mbali ya ushahidi madhubuti aliokuwa nao, Odinga alikuwa pia na uhakika wa nguvu ya ndani aliyonayo – umma. Aliapa kuwa angeliisaka haki mahakamani na mitaani, kama vile yule jaji wa mahakama ya juu alivyowahi kuniambia aliwashauri walimu waliogoma nchini Kenya.

Kwa hivyo, mafanikio makubwa ambayo Kenya imeyapata kupitia uamuzi huu wa Mahakama ya Juu hayatokani na nia njema tu ya majaji kwenye mahakama hiyo, wala huruma ya Rais Kenyatta kuwaruhusu kufikia hatua ya kwenda mahakamani au kuandamana mitaani, bali unatokana na mapambano ambayo upinzani na asasi za kijamii nchini Kenya zimeyapigana kwa zaidi ya miongo miwili sasa.

Haya ni mapambano ya ndani, ya watu wenyewe, ambayo yana gharama kubwa lakini ambayo matunda yake pia ni makubwa.

Ikiwa wanademokrasia wa mataifa mengine ya Afrika Mashariki na Kati wanayatamani  yanayojiri Kenya, basi watende kama walivyotenda wenzao huko.

Wajipange na wajijenge ndani yao, na wapambane kwa imani kuwa wao peke yao ndio wa kubadilisha hali iliyopo.

Si Muingereza wala si Mmarekani!

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHalisi la tarehe 4 Septemba 2017.

 


Filed under: KALAMU YA GHASSANI Tagged: Kenya, Kenyatta, Odinga

Uhuru Kenyatta na maafisa wa IEBC waondolewe

$
0
0

Siwezi kuacha asilani masuala ya uchaguzi wa Kenya yanipite bila kutoa maoni yoyote yale. Chaguzi zote za nyuma pia nilitoa maoni na ushauri kupitia vyombo vya habari. Tunakumbuka kuwa siku ya Ijumaa Septemba 1, 2017 ilikuwa ni shangwe Afrika nzima. Ni siku ambayo Kenya na Afrika iliishtua dunia ya wastaarabu na wapenda haki, amani na demokrasia.

Vyombo vya habari vikubwa duniani vilirusha habari ya dharura au habari ya hivi punde (breaking news) kutoka Kenya. Ilikuwa siku ya ushindi mkubwa na wa kihistoria kwa Kenya na Afrika. Hata Uhuru Kenyatta ambaye ushindi wake ulibatilishwa aliheshimu maamuzi ya mahakama japo hakukubaliana nayo. Na akaahidi yuko tayari kwenda kupiga debe upya.

Sambamba na hilo, dunia nzima iliwapongeza majaji wa Kenya wakiongozwa na Jaji Mkuu David Maraga kwa kuonesha ukomavu na ujasiri wa kutenda na kutoa haki. Binafsi nilifurahi mno kwa maamuzi ya majaji. Si kwamba napendelea yeyote kati ya wagombea wanane waliojitokeza, kama ambavyo akina Edward Lowassa walivyofanya. Na naelewa hakuna tatizo kumpenda mgombea yeyote, lakini utashi wangu unapenda ushindi wa kidemokrasia na wa haki kwa yeyote, awe Mohammed Abduba Dida au Dkt Ekuru Aukot.

Ilipofika Jumamosi ya Septemba 2, 2017, kwa kutumia ulimi uleule na kinywa kilekile, Uhuru Kenyatta aliporomosha matusi mazito kwa majaji na kuahidi kuifumua upya na kuirekebisha mahakama endapo atashinda uchaguzi wa marudio; tofauti kabisa na aliposema anaheshimu maamuzi ya majaji. Akawaita majaji wakora! Akaapa, ninanukuu “…watano au wasita…” eti hawezi kuamua nani awe rais kwa niaba ya Wakenya milioni 40.

Hata hivyo, ukweli ni kwamba majaji hawakuamua nani awe rais. Na wala hawakusema Uhuru alichakachua matokeo. Ni tume (IEBC) iliyochakachua matokeo ya urais. Kwahiyo majaji wakaamua uchaguzi urudiwe kwa kuwa haipendezi hata kwa Uhuru mwenyewe kupata kura haramu kwa mitambo ya kompyuta. Inabidi apate kura halali miongoni mwa Wakenya milioni 40.

Dosari za Wazi za IEBC na Makosa ya Uhuru Kenyatta

Kuna watu wanauliza kwanini uchaguzi wa urais umepatikana na dosari wakati waangalizi wa kitaifa na kimataifa walisema ulikuwa huru, wa haki na wa uwazi? Nifafanue kwa ufupi kuwa kazi ya waangalizi ni kufuatilia uhalali wa mchakato wa uchaguzi kabla na wakati wa kupiga kura. Hawahusiki kabisa kuhesabu kura. Wapiga kura wakimaliza zoezi la kupiga kura unakuwa ndio mwisho wa kazi ya waangalizi. Kuhesabu kura ni kazi ya maafisa wa tume, mawakala wa vyama vya siasa na/au wagombea binafsi.

Badala ya kuhesabu kura kwa kutumia kompyuta na fomu 34a na 34b kwa pamoja, IEBC ikaamua kupeperusha tu matokeo kwa kompyuta pasipo kuambatisha fomu husika. Haikuzingatia matakwa ya kikatiba, kisheria na kikanuni. Lakini kumbe baadhi ya maafisa wa IEBC walianza kuchakachua hesabu. Kisheria mshindi wa uchaguzi hana budi kutokana na utashi na uwingi wa wapiga kura, na si kutokana na utashi wa  wanaohesabu kura.

Katika anga za kimataifa nimewahi kusema, najinukuu: “What counts in authoritarian regimes is not who cast votes, but who count votes.” Nikimaanisha kuwa kinachojalisha katika tawala za kiimla si wanaopiga kura, bali wanaozihesabu. Hao ndio humweka mshindi wamtakaye wao!

Nchi nyingi (si zote) za kidikteta Afrika, na hata nje ya Afrika, watawala dhalimu hujigamba eti mshindi hapatikani kwa vijikaratasi vya kura. Labda niweke wazi hapa, kura si karatasi tu, bali ni sauti ya maamuzi ya mpiga kura. Kuidharau sauti hii kupitia karatasi ya kura ni kuinajisi demokrasia na ni kuyanajisi maamuzi ya kidemokrasia. Ndicho walichokifanya IEBC.

Kabla hata kampeni za uchaguzi wa marudio hazijaanza rasmi, tayari IEBC imeanza kwa dosari kubwa. Kimakosa imetangaza marudio ya uchaguzi yawe Oktoba 17, 2017 kwa wagombea wawili tu, Raila Amalo Odinga na Uhuru Muigai Kenyatta, badala ya wagombea wote wanane. Baada ya kugundua dosari kadhaa (irregularities and illegalities), majaji waliamua uchaguzi wa urais urudiwe kwa kuwa ulikuwa batili (null and void).

Majaji hawakusema wagombea wawili warudie uchaguzi, la hasha! Walisema utaratibu wa kuhesabu kura za urais ulikiukwa kinyume na katiba na kwahiyo ni batili na usiofaa. Wagombea urais walikuwa wanane, IEBC wanapaswa wasikilize tena na tena hukumu ndiposa watangaze tarehe mpya ya uchaguzi kwa wagombea wote. Mimi si Mkenya, ni Mtanzania, lakini ninayewapenda jirani zetu na kuwakumbusha sheria, kanuni na taratibu walizojiwekea wenyewe. Ninawaombea Mungu awaongoze na kuwalinda!

Kama nilivyotangulia kusema hapo juu, Uhuru Muigai Kenyatta kaichukia vibaya sana mahakama ya juu kufuta upuuzi wa tume, anaitetea tume iliyochakachua matokeo ya urais. Naelewa kuchanganyikiwa kwake, lakini mwenye hekima na ambaye ni rais angependekeza, japo kwa kuzuga, irekebishwe tume, si mahakama. Je, mbona 2013 hakuirekebisha mahakama iliyomthibitisha? Je, anadhihirisha aliungana na tume kuvuruga hesabu?

Kwa elimu yao majaji, hadhi yao, umri wao (na kuwa na familia), na uaminifu wao katika kutenda na kutoa haki, ni kuwadhalilisha na kuwafedhehesha kwa kuwaita wakora (crooks). Wakora ni majambazi, wahuni, walaghai na vibaka wa mitaani. Ni wahalifu! Kama anaona wanasheria ni vibaka, je atairekebisha mahakama kwa kuwaweka nani mbadala? Wafanyabiashara? Munguki? Kabila lake? Mbona si fani yao?!

Ikumbukwe kuwa tangu uhuru, Kenya imetawaliwa na marais wanne toka makabila mawili tu, watatu wakikuyu na mmoja mkalenjin. Muungano wa Jubilee sehemu kubwa ni wakikuyu na wakalenjin. Labda Kenyatta anataka hata mahakama iwe makabila mawili tu: Kikuyu na Kalenjin. Ubaguzi wa kikabila unawatesa sana Wakenya, hatutaki mahakama iwe ya kikabila.

Aidha, nisisitize kuwa mahakama ndio itakuwa mshindi katika uchaguzi wa marudio, si mgombea mmoja. Nasema hivyo kwa kuwa mahakama imeushinda udhalimu. Mgombea atakayepata kura nyingi auweke wakfu (dedicate) ushindi wake kwa mahakama na majaji waliotenda na kutoa haki.

Naam, safari hii hatutaki tena tume itutoneshe kidonda na machungu ya mauaji ya kikatili ya Chris Musando aliyesimama kidete kuhakikisha kuwa hakuna mtu yeyote atakayedukua (hack) utaratibu wa kuhesabu kura kwa kuwa ana nywila (password) kwenye kiganja chake. Kama vile kumkomoa kwa usemi wake huo, wauaji walikikata kiganja chake na kuitupa maiti yake vichakani! Mpaka sasa kuko kimya, hatujui kama upelelezi unaendelea au kama kuna yeyote aliyakamatwa kuhusiana na mauaji hayo.

Uhuru Kenyatta kajikosesha sifa

Kwa kuwatukana majaji na kuahidi kuivunjilia mbali mahakama, Uhuru Kenyatta amejifutia sifa ya kugombea uchaguzi wa marudio. Aidha, kwa tume kufanya makosa mengine kabla hata uchaguzi haujarudiwa, imejiondolea uhalali wa kusimamia uchaguzi wa marudio. Kwahiyo, natoa wito wa kumfuta Uhuru Kenyatta katika uchaguzi wa marudio kwa kukosa sifa za kuwa mgombea, hususan kwa kutishia kuuvunja mhimili wa dola wa kutoa haki uliopo kikatiba na wenye nguvu sawa na serikali na bunge.

Mtu aliyeitukana mahakama, aliyeitukana haki, aliyeutukana utawala na uongozi bora, hapaswi kugombea nafasi yoyote. Mtu aliyewafananisha wanasheria na wakora hafai kuwa rais wa Kenya na nchi yoyote ile ya kidemokrasia. Hawafai Wakenya na Waafrika wote. Amejitia aibu, amewatia aibu Wakenya, amewadhalilisha wanasheria wa Kenya na nje ya Kenya, na katutia aibu sisi Waafrika na Afrika yote.

Matusi kwa mhimili wa mahakama kutoka kwa mtu mwenye hadhi ya rais hakuwezi kuvumilika. Aende kuiendeleza ardhi ya maelfu ya hekta ambayo Baba yake Jomo Kenyatta aliichukua kwa uroho na ubinafsi na kuwaacha Wakenya wengi wakiwa hawana pa kuchungia ng’ombe, kulima na kuishi. La sivyo asubiri rungu la kufutiwa vibali vya kumiliki ardhi toka kwa mtu kama John Pombe Magufuli, endapo atokea Kenya.

Natoa wito kwa majaji wote 7 waliohusika kutoa maamuzi, wamshitaki Uhuru Kenyatta kwa kuwadhalilisha na kuidhalilisha mahakama. Aidha achakuliwe hatua kali za kutishia kuifumua na kuivunjilia mbali mahakama, mhimili unaojitgemea kama ilivyo serikali na bunge. Amevunja katiba aliyoapa kuilinda. Kama ana japo chembe ndogo tu ya uungwana, ajiuzulu urais na ukaimiwe na mwingine hadi rais mwingine apatikane.

Natoa wito kwa wajumbe na maafisa wote wa tume na Mwenyekiti wao Wafula Chebukati wajiuzulu mara moja, au la wafukuzwe kazi endapo hawatajiuzulu wenyewe kwa hiari. Hawafai kuendesha uchaguzi kwa kuanza kuwabagua wagombea kinyume na katiba ya Kenya na tume yenyewe iliyowapitisha. Wasipewe nafasi nyingine ya uharibifu.

Nihitimishe kwa kutoa wito kwa wagombea wote wanane, viongozi wa asasi za kijamii (pamoja na dini), wanasheria (hususan LSK), na viongozi wa vyama vya siasa; wakae kujadili dosari zilizojitokeza na namna bora ya kuziondoa. Wapate mwafaka na maridhiano ya kuendesha uchaguzi wa marudio unaokubalika pande zote kikatiba, kisheria na kikanuni. Kisha wateue wajumbe na maafisa wapya wa tume mpya wanaoaminiwa na wote.

TANBIHI: Makala hii imeandikwa na Gwandumi Gwappo A. Mwakatobe, mchambuzi huru wa masuala ya kitaifa na kimataifa, anayeishi Mwakaleli, Busokelo, Rungwe, Mbeya. Anapatikana kwa anuani ya baruapepe: gwandumi@hotmail.com au gwappomwakatobe@gmail.com

 


Filed under: SIASA Tagged: IEBC, Kenya, Uhuru Kenyatta

Profesa atatulia akitimiza anachotakiwa

$
0
0

MSOMAJI wa MwanaHALISI, na hasa safu hii, amenijia. Kupitia ujumbe mfupi wa simu ya mkononi, akitumia Na. +255623248721, anasema, “… kwa kuwa CUF walitoa mwanya, yeye ameutumia kujirudisha kwenye kiti… sasa wamsikilize tu maana ameshika mpini.”

Huyu msomaji anajibu nilichokiandika katika toleo la gazeti hili, Na. 404, nilipojadili kinachoendelea ndani ya Chama cha Wananchi (CUF), na hasa mgogoro aliousababisha Profesa Ibrahim Lipumba, aliyejirudisha uongozini na kushikilia kiti cha mwenyekiti ilhali alijiuzulu mwenyewe kwa tamko la hadharani.

Msomaji hakufafanua mwanya ambao CUF waliuacha ambao Profesa Lipumba aliutumia kutaka kurudi kwenye kiti miezi kumi baada ya kujiuzulu kwa hiari yake akisema nafsi yake inamsuta kuendelea kukiongoza chama hicho.

Hata hivyo, namsoma msomaji kuwa anazungumzia kile kinachotajwa na wengi kuwa eti chama, baada ya tamko la profesa kujiuzulu ambalo alilitoa tarehe 5 Agosti 2015, kwenye mkutano na waandishi wa habari katika Hoteli ya Peacock, Mnazimmoja, Dar es Salaam, hakikuitisha mkutano ili kujadili uamuzi huo.

Tangu awali, mtizamo wangu uliniaminisha kusema kwa akili ya kawaida, kilichopaswa kufanywa wala sio kujadili kujiuzulu kwa mwenyekiti. Msingi ni kuwa hakuomba kujiuzulu, alijiuzulu. Alijiuzulu kwa tamko la maneno, na akafanya hivyo kwa barua rasmi aliyokiandikia chama kupitia Katibu Mkuu.

Tena kwa kweli, Profesa Lipumba alijiuzulu huku akipuuza mashauri na nasaha za watu mbalimbali katika chama – makundi ya wanawake, wazee na vijana – waliomfikia na kumsihi aahirishe uamuzi wake angalau kwa wakati ule.

Katika pitapita zangu hivi karibuni, nilikutana na mmoja wa viongozi wa Kiislam inayomiliki shule ya msingi na sekondari, akinieleza kuwa alikuwa mmoja wa viongozi wa kidini “waliomsihi sana” profesa asijiuzulu.

Alinambia aliongoza kundi la maulamaa wenzake na vijana wa Kiislam wanaokiamini chama hicho, na kumsihi kuakhirisha kujiuzulu ili angalau asubiri uchaguzi wa rais, wabunge, wawakilishi na madiwani upite. Huko mbele angefikiriwa kuchukua hatua hiyo.

“Niliongoza wenzangu tukaenda Buguruni. Tulipokutana naye, nikamweleza tumefika kumuomba asijiuzulu kwa sasa… baada ya muda kidogo wa kuanza kutoa maelezo, nilijikuta nalia machozi kwa huzuni. Fikiria mtu mzima na familia yangu ninalia hadharani nikimsihi.

“Nilipopata nguvu nikamwambia, Profesa, hivi unavoniona ndivyo walivyo wenzangu hawa niliofuatana nao kuja kukuona hapa, na hata jamii kwa upana wake kabisa imeguswa na kushtushwa na habari hizi. Sasa tunakunasihi sana subiri kwanza uchaguzi upite.”

Hii ni ile siku ambayo profesa alihanikiza uwanja mzima kwenye ofisi kuu za CUF Buguruni, baada ya kusikika taarifa za nia yake hiyo. Siku hiyo ya tarehe 4 Agosti 2015, gazeti la Uhuru linalomilikiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), hasimu mkubwa wa kisiasa wa CUF, lilikuwa limechapisha habari iliyopewa uzito mkubwa kuwa Lipumba amejiuzulu uenyekiti CUF.

Katika habari hiyo, kulikuwa na kauli ya Katibu Mkuu Maalim Seif Shariff Hamad kuwa hakuwa na taarifa hizo, na kwamba kwa nafasi yake ya kuwa dhamana wa mbele wa chama hicho, anahisabu Profesa angali mwenyekiti CUF.

Profesa Lipumba akionesha kusikia kilio cha viongozi wenzake, ambao pia walimsihi asitishe nia yake hiyo mpaka chama kimalize shughuli za uchaguzi mkuu, wanachama wenzake na wapenzi wa chama, aliondoka Buguruni na kurejea nyumbani kwake.

Kumbe aliwaridhia wote wale kwa shingo upande. Moyoni mwake na kama alivyosema hadharani, dhamira yake inamsuta kubakia kiongozi, alipoamka tu siku iliyofuata, tarehe 5 Agosti, alifukuzia hotelini Peacock, na kutangaza kuwa amejiuzulu.

Ni muhimu ieleweke hapa, profesa huyu wa uchumi, hakutangaza nia. Hakusema anaomba chama kimruhusu ajiuzulu. Alisema “nimeamua kujiuzulu nafasi ya mwenyekiti wa CUF na nitabakia mwanachama ambaye nimelipia kadi yangu….”

Hivi baada ya hapo, uongozi ufanye nini? Ndipo ukaitisha haraka kikao cha Baraza Kuu la Uongozi la Taifa (BKUT). Baraza likateua wanachama watatu wa kushika majukumu ya mwenyekiti aliyekiacha kiti.

Baraza hilo ambalo ilielezwa kuwa lilikasimiwa mamlaka ya Mkutano Mkuu wa Chama, lilimteua wakili maarufu nchini, Twaha Taslima, kuongoza iliyoitwa Kamati ya Uongozi ya Taifa. Wajumbe wenzake ni Aboubakar Khamis Bakary, mwakilishi wa Mgogoni, Pemba, na Severine Mwijage, mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa wa Kagera.

Hapana shaka, uongozi uliona hiyo ndiyo hatua muafaka inayozingatia katiba ya chama. Haionekani hii inayosemwa na wanaomtii profesa kuwa kulipaswa kuitishwa mkutano mkuu ili kuridhia. Kwa CUF, katika kipindi kile, dharura ilikuwa kushughulikia mipango ya uchaguzi mkuu wa taifa, na wala sio kushughulika na mtu aliyejiuzulu mwenyewe.

Hata akili ya kawaida, inakubali kuwa kwa vile alichokifanya profesa ni kujiuzulu, na sio kuomba kujiuzulu, la muhimu ni kujaza nafasi yake. Si tumeona namna alivyoshawishiwa asijiuzulu akapuuza; anayesema ilikuwa kushughulikia uamuzi wake kwa maana ya kuitisha mkutano mkuu wa kuridhia, anataka kuonesha anavyodharau akili za viongozi wote aliowaacha profesa.

Baraza Kuu lina nguvu za kutosha kufanya maamuzi. Na kwa kuwa ndio chombo cha kuweza kukutana kwa dharura kuliko mkutano mkuu unaohitaji maandalizi na raslimali fedha, na kwa wakati ule chama kikikabiliwa na kibarua cha kushiriki uchaguzi wa taifa, uamuzi wa kuteua kamati ya kushika majukumu ya mwenyekiti, ni muafaka.

Si kweli kuwa palikuwa na mwanya wa profesa kurudi kitini. Ni aibu na fedheha kujirudisha uongozini baada ya kukaa nje kwa miezi kumi. Uamuzi aliouchukua haujapata kutokea penginepo popote.

Katika kuonesha msimamo imara kuhusu uamuzi wa chama kuteua kamati ya uongozi, tarehe 17 Juni 2016, mwenyekiti wa kamati, wakili Taslima, alitoa tamko kuhusu hatua ya profesa kulazimisha kurudi kwenye kiti kwa kuwa eti “hakujibiwa barua yake ya kufuta au kutengua uamuzi wake wa kujiuzulu.”

Kwamba kulikuwa na sharti la kikatiba kuwa ajibiwe barua ya kujiuzulu, halipo kwenye katiba ya chama. Alijiuzulu anajibiwa nini hapo? Kuwa Mheshimiwa Profesa Lipumba umekubaliwa kujiuzulu?” Hilo halipo kwenye chama hicho, ndivyo uongozi unavyoshikilia.

Wakili Taslima alihoji: “Hivi madai ya kutojibiwa barua yake ya tarehe 5 Agosti aliyompelekea Katibu Mkuu, ndiyo msingi wa hoja yake ya kurudi katika nafasi ya uwenyekiti, hajui kwamba Mkutano Mkuu wa Taifa haukuhitajika kufanyika kwa ajili ya jambo hili?

Hivi wale wajumbe walioteuliwa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kuunda Kamati ya Uongozi wanaenda wapi sasa baada ya yeye kuamua kujirudishia uongozi?

Hivi yeye Lipumba na Baraza Kuu nani mkubwa kimamlaka mpaka afikie hatua ya kutoheshimu uamuzi wa Baraza Kuu?

Profesa Lipumba hasa kwa uamuzi wake wa kujirudishia uenyekiti ametumia kipengele kipi cha Katiba ya chama hasa baada ya kuvitaja vipengele kadhaa vya Katiba katika Ibara ya 117?

Maswali haya tumeshindwa kuyajibu kwa ufasaha. Chama kinamuomba asijaribu kukiyumbisha chama kipindi hiki; Watanzania wanahitaji kuwekwa pamoja na kupewa matumaini ya namna gani matatizo yao yanaweza kutatuliwa.”

Ni kwa sababu hiyo, hata profesa Lipumba anapohangaika kutafuta suluhu haeleweki. Na sababu kubwa ni kwamba ameendelea kuchukua hatua za kukidhoofisha kuliko kukiimarisha chama. Ni tofauti na madai yake “ninakipenda chama hiki na tungemaliza mgogoro nje ya mahakama.”

Ukweli profesa anaogopa kesi mahakamani, zikiwemo zile alizotuma mawakili wazifungue. Anajua ataanguka. Si hivyo, angetulia akisubiri maamuzi. Hatulii maana anachotakiwa kukikamilisha kwa maslahi binafsi – kumtokomeza Maalim Seif – hajakifikia.

TANBIHI: Makala hii imeandikwa na Jabir Idrissa na ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHALISI la tarehe 28 Agosti 2017.


Filed under: SIASA

Ukorofi wa CCM unazuia demokrasia

$
0
0

TONY Mwangi hakumchagua Raila Odinga anayewakilisha muungano wa National Super Alliance (NASA). Na wala hakumpendelea Uhuru Kenyatta wa Jubilee. Isitoshe hajachukia wala kujuta.

Mpigakura huyu katika uchaguzi mkuu wa Kenya, si kwamba amekosa tabasamu kwa uamuzi wa mahakama ya juu – Supreme Court of Kenya – kubatilisha uchaguzi wa rais wa taifa lenye uchumi mkubwa zaidi kwa kanda hii ya Afrika Mashariki.

Kwa hakika ni kinyume chake. Mwangi anaringa na kujivuna kwa hatua hiyo. Anafurahia kile anachokiita “tukio muhimu” la ustawishaji wa demokrasia na utawala wa sheria nchini kwake.

Hana wasiwasi kwa kuwa ana imani kubwa Kenya itampata rais katika muda uliopangwa ili aongoze jahazi la kusukuma mbele maendeleo yao.

Mahakama ya Juu ya Kenya imebatilisha matokeo ya uchaguzi wa rais uliofanyika tarehe 8 Agosti 2017 baada ya kuthibitisha malalamiko ya ukiukwaji mkubwa wa utaratibu yaliyowasilishwa na Odinga.

Odinga wa NASA aliyapinga matokeo tangu hatua ya kwanza yalipokuwa yakitangazwa hatua kwa hatua kupitia kituo cha kurushia matangazo ya matokeo kilichokuwa ukumbi wa Bomas, jijini Nairobi.

Taarifa yake ya awali ilisema kuwa matokeo yaliyokuwa yakitangazwa yalikuwa tofauti na yale yaliyokuwa yamerikodiwa kwenye fomu ya matokeo iliyosainiwa na watendaji wa Tume ya Uchaguzi na Mipaka ya Kenya (IEBC).

Upinzani wa matokeo aliouonesha Odinga uliendana na madai kuwa mfumo wa kuhakiki na kurusha matokeo uliingiliwa. Zikaja sauti kutoka kwa watu mbalimbali hasa makundi ya watazamaji wa uchaguzi kumtaka asubiri matokeo ya mwisho ndipo atangaze msimamo wake.

Matokeo yakatangazwa. Uhuru aliyegombea akitaka kuongoza kwa muhula wa pili mfululizo, baada ya kushinda awali mwaka 2013, akatangazwa ameshinda tena.

Tume, sasa ikiwa imekana madai ya upinzani kuwa mfumo wake wa kiteknolojia wa kuhifadhi matokeo uliingiliwa katikati, ilisema Uhuru alishinda urais kwa tofauti ya zaidi ya kura milioni mbili.

Ni hapo watazamaji wakainua sauti kwa msisitizo kumtaka Odinga na NASA yake kutochochea vurugu, badala yake, apeleke malalamiko yake mahakamani.

Shinikizo kwa Odinga lilikuwa na mantiki. Katiba ya Kenya na Sheria ya Uchaguzi vinaruhusu mgombea urais ambaye ametangazwa kushindwa kura, kufungua shauri mahakamani.

Kwa lugha nyingine, Katiba ya Kenya inatoa haki ya matokeo ya uchaguzi wa rais kuhojiwa. Hoja za kuyapinga matokeo zinawasilishwa kwenye mahakama ya juu inayoundwa na jopo la majaji saba.

Odinga kwa kuamini hajatendewa haki katika hatua ya Tume ya Uchaguzi kumtangaza mpinzani wake, Uhuru Kenyatta, kuwa ndo mshindi, ametumia fursa ya kikatiba na haki yake kufungua shauri.

Katiba inatoa fursa na kupanga muda wa kuitumia fursa hiyo. Odinga akatimiza masharti ya kuhoji utaratibu wa kupatikana kwa mshindi.

Tume ikasikiliza kwa kupokea vielelezo vilivyoendana na malalamiko ya Odinga; na yenyewe ikiwa na muda maalum wa kisheria kufanya uamuzi wa malalamiko iliyoyapokea.

Ijumaa ya tarehe 1 Septemba 2017 ikawa siku ya Mahakama ya Juu chini ya rais wake David Maraga, kutoa uamuzi wa malalamiko ya Odinga.

Uamuzi ukathibitisha madai ya kukiukwa kwa utaratibu wa kisheria wa kuendesha uchaguzi. Majaji watano wakaridhika uchaguzi ulikuwa huru lakini haukuwa wa haki.

Vipi sasa kuhusu fidia ya ukiukwaji huo wa utaratibu wa kuendesha uchaguzi ulio huru, wa haki na kwa njia ya uwazi? Mahakama imeamua uchaguzi mpya ufanyike ndani ya siku 60 kutoka siku imetoka uamuzi wake.

Malalamiko yalitolewa ya kupinga matokeo. Walioona wameonewa wakatumia fursa ya kikatiba kudai haki itendeke. Upande wa Odinga umeridhika haki imetendeka.

Uhuru na kundi lake hawakuridhika na uamuzi wa Mahakama ya Juu na huku wakimuita Jaji Maraga na wenzake kuwa ni wakora au wezi, wameheshimu uamuzi japo hawauamini.

Mpigakura Mwangi anajivunia hatua hii. Inaendelea kuthibitisha kuwa nchi yake inazidi kuwa mfano wa baba wa demokrasia katika Bara la Afrika.

Mafanikio haya niliyaeleza bayana katika makala yangu wiki mbili zilizopita. Nikasema Kenya imepiga hatua nyingi mbele katika dhana ya demokrasia na utawala wa sheria. Nikasema na bado ninamaanisha, Tanzania na Zanzibar zinalo funzo kwa Kenya.

Ndipo ilipo tofauti ya hisia kati ya Mwangi wa Kenya na Mtanzania awe Mtanganyika au Mzanzibari. Mtanzania hana utulivu wala furaha kama alivyo Mwangi wa Kenya.

Tume ya Uchaguzi sio tu hazikuridhisha wagombea na wananchi kwa ujumla, bali kwa hakika zimeacha vinyongo ndani ya nyoyo za watu. Malalamiko yalikuwepo yalipuuzwa.

Mgombea urais upande wa Jamhuri ya Muungano kutoka upinzani uliounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa mpaka leo anaamini alishinda.

Kwa Zanzibar, hali ndio mbaya zaidi kwa sababu hivi ninavyojadili hapa, wananchi wanaamini mgombea wao kipenzi, Maalim Seif Shariff Hamad angetangazwa mshindi.

Watu wanasema wazi walisubiri Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) itangaze matokeo ya uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba 2015 kwa kuwa ndio kisheria uliostahili kuwapatia kiongozi wao.

Wanaamini Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 pamoja na marekebisho yake makubwa ya 2010, haitambui kilichoitwa “uchaguzi wa marudio” ambao Tume iliutumia kumtangaza Dk. Ali Mohamed Shein kuwa rais.

Katiba hiyo haisemi popote kuwa tume au ofisa wake yeyote, kwa jina lolote lile, anaweza kufuta uchaguzi uliokwishafanyika. Hayapo mamlaka ya kumwezesha hata mwenyekiti wake kufanya hivyo.

Wazanzibari walipigakura kwa amani. Kura zikahisabiwa kwa amani. Matokeo ya viti vya uwakilishi na udiwani yalihisabiwa sambamba na yale ya urais. Washindi wa uwakilishi na udiwani walitangazwa na kukabidhiwa hati za ushindi.

Kura za urais zilihisabiwa kwa mfumo huohuo. Kazi ya kuzihakiki ilifanywa vizuri ndio maana matokeo yalianza kutangazwa kwenye kituo cha kurushia matokeo kilichowekwa ukumbi wa Salama wa Hoteli ya Bwawani.

Ni nini kilichosababisha Mwenyekiti wa Tume, Jecha Salim Jecha kutangaza kuyafuta matokeo ya uchaguzi wote? Jecha katika tangazo lake la tarehe 28 Oktoba 2015 alifuta hata uchaguzi wa uwakilishi na udiwani ambao washindi walishakabidhiwa hati za ushindi.

Alifanya hivyo akijua fika hana mamlaka ya kisheria ya kufanya hivyo. Alijua na mpaka sasa anajua hana utetezi wowote wenye nguvu ya kisheria wa kumvua na kosa la kuhatarisha usalama wa nchi ikitokea ameshitakiwa mahakamani.

Ni kwa sababu alijua kwa kuwa watakaonufaika na hujuma yake ndio walioshika serikali, hataguswa na mkono wa sheria. Lakini ninaamini hajaukwepa mkono wa sheria. Unachelewa tu kumfikia.

Jecha alijua hakuna mahakama inayoweza kusikiliza malalamiko ya swahiba zake Chama Cha Mapinduzi (CCM) iwapo angewatangaza kuwa washindwa katika uchaguzi.

Kwa upande mwingine, alijua pia hakuna mahakama itakayofanya kazi ya kusikiliza malalamiko ya Chama cha Wananchi (CUF) katika kunyimwa haki yao ya ushindi katika uchaguzi huo.

Na hiyo ndiyo kasoro ya waziwazi na kikwazo cha kuisogeza Zanzibar kwenye demokrasia ya kweli, utawala wa sheria na utengamano wa kijamii kupitia uchaguzi mkuu ulio huru, wa haki na uliofanywa katika mifumo iliyo wazi.

Upinzani kupitia CUF na mwamvuli wa Ukawa upo tayari kama walivyo tayari wananchi wa Unguja na Pemba.

Shida kubwa iliyopo ni ukorofi wa viongozi wa CCM kwa kudhani wamehulukiwa haki ya kuiongoza serikali milele.

TANBIHI: Makala hii imeandikwa na Jabir Idrissa na ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHALISI la tarehe 11 Septemba 2017.


Filed under: SAUTI

Miezi 10 bila Ben Saanane

$
0
0

Miezi 10 sasa tangu Ben Saanane apotee. Umoja wa Kizazi cha Kuhoji Tanzania (UTG) tumeshirikiana na vyombo vya dola, taasisi na mashirika ya kiraia katika juhudi za kumtafuta. Tumetoa ushirikiano wote kwa jeshi la polisi na mamlaka zingine za nchi. Katika vikao vyetu na vyombo vya dola, tulieleza mashaka yetu na tukahitaji wayafanyie kazi ili kuyasahihisha.

Walituhakikishia kuwa wangeshughulika na kila njia ambayo ingeweza kuleta taarifa ya Ben alipo. Lakini miezi 10 sasa, mashaka yapo pale pale. Vyombo vya dola vimeshindwa kusahihisha hata mashaka madogo tu, kwa mfano mtu aliyempigia simu ya vitisho Ben.

Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TRA) walitoa mawasiliano ya Ben ikiwa ni pamoja na watu waliokua wakimtisha. Polisi wakaahidi kufuatilia na kubaini watu hao. Sasa ni miezi 10 polisi WAMESHINDWA kuwakamata watu hao. Wameshindwa hata kuwabaini tu kwamba ni akina nani wakati wamepewa mawasiliano yote na TCRA.

Hiki ni kielelezo kwamba vyombo vyetu vya ndani vimeshindwa kumtafuta Ben. Mara ya mwisho tumeenda makao makuu ya polisi, taarifa tuliyopewa ni kwamba bado wanaendelea na uchunguzi. Miezi 10 ya uchunguzi wameshindwa hata kujua waliokua wanamtisha Ben wakati namba wamepewa na TCRA? Uchunguzi gani huu?

Siingilii kazi za polisi, lakini inawezekanaje uchunguzi wa mtu anayekashifu serikali unatumia siku moja ameshakamatwa, lakini mtu aliyemtishia Ben maisha unatumia miezi 10 na bado wameshindwa kumpata?

Na hili ni moja dogo. Yapo mengi makubwa kuhusu Ben ambayo polisi waliahidi kuyachunguza. Lakini kama hili dogo limewashinda, hayo mengine itakuaje?

Tunalipenda jeshi letu la polisi, tunaliheshimu, lakini tunadhani wamefikia kiwango chao cha mwisho cha uchunguzi. Hawawezi tena. Tunawasiliana na wenzetu wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) ili kuomba serikali iruhusu wachunguzi wa kimataifa.

Tuliomba waangalizi kutoka Umoja wa Mataifa ataifa na wakaonesha hamu ya kusaidia, lakini serikali ikatuambia tusubiri kwanza polisi wamalize uchunguzi wao, kama wakishindwa ndipo tufikirie wachunguzi kutoka nje. Serikali ilituhakikishia tuendelee kuwa na IMANI na jeshi la polisi.

Ni kweli tuna imani na polisi lakini tunadhani uwezo wao ni mdogo kuchunguza suala la Ben. Tutawaomba waweze kutangaza kwamba wameshindwa, ili tupate uhalali wa kuomba wachunguzi wa kimataifa. #BringBackBenAlive!


Imeandikwa na Malisa Godlisten katika mtandao wa Facebook tarehe 12 Septemba 2017.


Filed under: JAMII

Taifa lisilowaomboleza wahanga wake, haliwezi kuwaadhimisha mashujaa wake

$
0
0

Usiku wa kuamkia tarehe 10 Septemba 2011, meli ya Mv Spice Islander iliondoka kisiwani Unguja kuelekea Pemba ikiwa imejaza kupita uwezo wake halisi.

Inasemekana kuwa ndani yake mulikuwa na abiria zaidi ya 3,000 badala ya 645 iliotakiwa kisheria. Ilikuwa pia na shehena kubwa ya mizigo.

Majira ya saa saba za usiku ikazama kwenye Mkondo wa Nungwi na hadi sasa, miaka saba baadaye, watu waliopatikana wakiwa hai ni 620 tu, hiyo ikimaanisha kuwa ndani ya usiku huo mmoja tu, Zanzibar ilipoteza roho takribani 2,500.

Kwa taifa lenye raia milioni 1.3, hii ni idadi kubwa kabisa kupotea kwa wakati mmoja, tangu wale waliopotea wakati wa mavamizi ya Januari 1964. Takribani kila familia, hasa kisiwani Pemba, ilikumbwa na msiba huo. Aliyekuwa hakupoteza jamaa yake wa moja kwa moja wa damu, basi alipoteza jamaa wa jamaa yake, na kwa mjengeko wa kijamii na kitamaduni wa Zanzibar ulivyo, kwa hakika huu ulikuwa msiba wa taifa zima.

Ripoti iliyotolewa baadaye na Tume ya Uchunguzi wa ajali hiyo ilithibitisha kuwa hasara hiyo kubwa kwa roho na mali ilisababishwa na uzembe na ukosefu wa uwajibikaji. Hapana shaka, palikuwa na mkufu mrefu wa waliopaswa kuwajibishwa kwa uzembe huu – kuanzia maafisa wa bandari, wamiliki wa meli yenyewe hadi maafisa wa usalama.

Bahati mbaya, hivyo sivyo ilivyokuwa hadi sasa, miaka saba baada ya mkasa wenyewe. Lakini hilo huenda likawa ni dogo sana kuliko upande mwengine wa suala hili. Nalo ni ukweli ni kuwa taifa la Zanzibar limeamua kuzidharau kabisa hisia kali zinazoambatana na msiba huu mkubwa.

Mwaka 2012, mwaka mmoja baada ya tukio lenyewe, nilizungumza na waziri aliyekuwa na dhamana ya usafiri wa baharini kwenye Serikali ya Umoja wa Kitaifa ya Zanzibar, Rashid Seif, na nilipomuuliza serikali ilikuwa na mpango gani wa kuwawekea kumbukumbu wahanga wa ajali ile, jawabu yake ilikuwa: “Zanzibar ni nchi ya Waislamu na Waislamu huwa hawana kawaida ya kuikuza misiba yao.”

Nilimkumbusha ukweli kuwa Zanzibar ina sanamu ya kumbukumbu ya Abeid Karume na hadi leo sanamu hilo na kaburi lake ni miongoni mwa alama za historia ya nchi, pamoja na pia kuifanya siku yake aliyouawa, tarehe 7 Aprili, kuwa siku ya mapumziko kitaifa.

Msimamo wake, ambao ndio uliokuwa msimamo wa serikali, ulikuwa kwamba hitima zilizosomwa na matanga yaliyowekwa na familia pamoja na siku tatu za maombolezo ya kitaifa zilikidhi haja yote. Hapakuwa na chengine cha kufanya.

Wakati huo nilidhani kuwa jawabu hiyo ingelikuwa ya muda tu, na baadaye hali ingelibadilika. Moyoni mwangu mulikuwa na imani kwamba hatuwezi kupoteza watu wengi kwa wakati mmoja kama wale, kisha tukawasahau milele kama kwamba hakuna kilichotokezea ndani ya nchi.

Huu ni mwaka wa sita sasa na alichokisema Waziri Rashid wakati ule ndicho ambacho kimesimama hadi leo, na imani yangu imeanguka na kuzikwa mchangani. Hii haimaanishi kuwa msimamo huo wa serikali ulikuwa sahihi, wala kwamba wangu ulikuwa sio. Hapana. Bali tuliyaangalia mambo kutoka vipembe tafauti.

Wakati huo, na hadi leo, mimi nilitaka Zanzibar iuchukulie msiba huu kwa uzito mkubwa zaidi, maana haikuwahi kutokezea kabla ya hapo, ajali ya baharini, angani na wala ardhini kuondoka na watu wetu wengi kwa wakati mmoja kama ajali hii.

Ni kweli ajali si jambo la fahari hata kidogo. Lakini kuwakumbuka wahanga wa ajali yenyewe hakuna maana ya kuionea fahari ajali hiyo. Kulikuwa, na bado, kuna maana ya kuwajali wenzetu waliotangulia mbele ya haki na kujifunza kwa mkasa wenyewe uliosababisha ajali hiyo.

Hadi leo, waliohusika na ajali yenyewe hawakubebeshwa dhanama yao wanayostahiki kuibeba, badala yake suala lenyewe limebambanywabambanywa na kuvungwavungwa hadi limefutika kwenye vitabu vya kumbukumbu kama kwamba roho zilizopotezwa hazikuwa za binaadamu.

Kulikuwa, na bado, kuna maana ya kuliwekea taifa letu kumbukumbu ya mazuri na mabaya yetu, ili vizazi vijavyo viige mazuri tuliyofanya sisi watangulizi wetu na vijifunze kwa mabaya yaliyotutokezea.

Ni kwa kuwa hatukuonesha tangu awali uzito unaostahiki kwenye jambo hili, ndio maana si ajabu kuwa miezi minane tu baadaye, meli nyengine iitwayo MV Skargit nayo ikazama mkondoni ikielekea Dar es Salaam, ikiondoka na roho nyengine za maelfu ya watu wetu. Chanzo kikiwa ni kile kile – uzembe wa wenye dhamana.

Kulikuwa, na bado, kuna maana ya kuwaenzi waliobakia hai baada ya mkasa wenyewe. Kwanza wale 620 walioripotiwa kuokolewa, kwa kuwapatia msaada wa kisaikolojia, kisheria na kiuchumi ili kuyaanza tena maisha baada ya kupitia njia ya mauti na kunusurika. Pili kwa wanafamilia ambao waliwapoteza ndugu na jamaa zao.

Kuna ambao ajali hii iliondoka na takribani familia nzima, mfano wa yule bwana wa Gando, ambaye alibakiwa na paka wake tu nyumbani, lakini mke na wanawe wanne wote walikwenda.

Hadi leo, hakuna taasisi wala mfuko ulioanzishwa kwa ajili ya wahanga hawa. Wenye misongo ya mawazo wameendelea kuwa nayo. Na si hasha kuwa wengine wamewafuata wapendwa wao makaburini, maana majonzi waliyoyabeba bila msaada wa kitaalamu kufarijiwa, yaliwafanya nao kufa vifo vya mapema.

Namjuwa rafiki yangu mkubwa ambaye alipoteza mke wake aliyekuwa ndio kwanza wameoana mwaka mmoja kabla ya ajali hiyo. Mwaka wa sita sasa huu amekataa kuoa tena, na bado hadi leo anaomboleza kama ndio kwanza mkewe amekufa jana jioni.

Namkumbuka mama ambaye aliwapoteza watoto wake watatu na wajukuu wanne, akibakiwa nyumbani na mtoto mmoja tu sasa, na hadi leo akimuita yule mmoja, kwanza hutaja majina ya wote waliotangulia mbele ya haki. Wala hakusudii. Lakini akili yake imetikisika, moyo wake umeganda.

Hawa wote walistahili jawabu nzuri zaidi kuliko ile ya kuambiwa tu kuwa Zanzibar ni nchi ya Waislamu na Waislamu hawana kawaida ya kuitukuza misiba yao. Jawabu ambayo sio tu ni kinyume na Uislamu wenyewe, maana vyenginevyo Qur’an isingejaa visa vya majanga yaliyowapata waliotangulia, bali pia haitatuwi ukubwa wa tatizo lililosababishwa na ajali hii.

Lakini kama kweli sisi ni taifa la watu wenye fikira, bado hatujachelewa kupatengeneza pale tulipoharibu. Ni miaka sita tu sasa imepita tangu ajali hizi mbili – ya MV Spice Islander na MV Skagit. Hata miaka kumi haijafika.

Yako matukio makubwa duniani ambayo kuanza kwake kukumbukwa na kupewa nafasi inayostahiki, kulianza miongo kadhaa baadaye, baada ya jamii kutulia na kutazama zilikopita ili kujenga mbele ziendako. Nasi tunaweza kufanya hivyo.

Kuelekea kuwapa hishima yao wahanga hawa, hata hivyo, tunapaswa kujipanga kwa tafiti, kwa maandishi, kwa rikodi za picha, vidio na sauti. Tunapaswa kuanzisha sasa vuguvugu maalum kwa ajili ya wahanga wa ajali hizo na kulipa sura na nguvu ya kuhifadhi tareikh yetu.

Tufanyeni hivyo kama jamii, kama nchi na kama taifa, maana taifa lisilowaomboleza wahanga wake, halina uthubutu wa kuwatukuza mashujaa wake.


Filed under: KALAMU YA GHASSANI Tagged: ajali, msiba, Mv Spice Islander, Zanzibar

Maisha yasiyotathminiwa hayana maana huyaishi

$
0
0

Ulimwenguni kote na katika zama zote jamii inapokuwa chini ya utawala ulioziba masikio na macho na nyoyo, watawala hupenda waachiwe wafanye watakavyo.

Huwa wamejirithisha wenyewe nchi na raia wake. Na kwa hili hawataki muhali, masahihisho, wala mabadiliko.

Anapotokea mtu kuwasahihisha, badala ya kumchukulia kuwa msaidizi, wao humchukulia adui wao nambari moja, na hivyo hujihalalishia kumuadhibu kwa namna yoyote waionayo inafaa.

Si jibu la haki, ingawa ndiyo kawaida ya watawala kumgeuza mkosoaji wao kuwa muhanga wa utamaduni huo mviya wa kutokutaka mawazo tafauti.

Na hiyo ndiyo dhambi ya asili ya watawala wote wa mkono wa chuma – kule kuamini kwao kuwa msaidizi wao ni yule tu anayewaitikia: “Ndiyo Mzee”, na kwamba kila anayewaambia: “ Hapana” ni adui wao.

Dhambi hii ni kubwa na gharama zake ni ghali mno kulipika.

Kuwatawala watu kwa mkono wa chuma kuna matokeo mabaya, lakini hakuvizi khulka ya wanaadamu kupinga walionalo silo.

Na ndio maana, kote ulimwenguni ambako tawala za aina hii zimepata kuweko, upinzani dhidi yake huzidi kukuwa na kukuwa kila kukicha, hata kama kila mbinu ya kuudidimiza hutumika kila saa na kila dakika.

Wakosoaji wa watawala wakizuiliwa njia hii ya kuwakosowa, huzumbuwa njia nyengine. Alimradi kila watawala wakaapo, hawawezi kustaaladhi nafsi zao, maana macho yote ya umma huwakodolea wao na vinywa vyao huhanikiza sauti: “Hivi sivyo, hilo silo!”

Mwangwi wa sauti hizi ni vitu vinavyoudhi sana mbele ya hadhara ya mtawala, lakini si vitu vinavyoweza kuepukika ikiwa mtawala huyo hakubali mwito wa mabadiliko.

Kila mtawala akizidi kuwa muimla, ndipo anapozidi kuzalisha sauti zinazomsuta na macho yanayomkodolea.

Hizi ni sauti na macho ya watu waliojitolea kumuambia mtawala wao makosefu yake na kumuonesha njia.

Lakini, utawala wa mkono wa chuma huambatana na ujigambi na majivuno.

Mtawala hupandwa na kichaa anapoambiwa kuwa ana makosefu fulani na fulani.

Maana, kwa kila hali, huwa kilevi cha madaraka kimeshamlevya na zile andasa zake humdanganya kwamba yeye yu Mr. Perfect – hawezi kuwa na mapungufu yoyote yale.

Basi hapo hucharukwa na kuanza kumuadhibu kila amuhojiye, haidhuru hoja hiyo iwe makini kiasi gani.

Na kila anavyoadhibu, huona bado – na huwa bado kweli! Huadhibu kwa ulimi wake, kwa mikono yake, kwa virungu, kwa jela, hata kwa risasi na kitanzi. Kwa kwa kila kitu.

Na bado wanaompinga huendelea tu. Angalia msuguano baina ya Bi Kirembwe na Mtolewa katika tamthilia ya Kivuli Kinaishi iliyoandikwa na Dk. Said Ahmed Mohammed uone anguko la kishindo la utawala ulioziba milango yake yote ya fahamu.

Dunia imejaa mifano ya visa na mikasa kama hii. Ni juu yetu kufundishika, ikiwa kweli tu watu wa kuzingatia kutokana na maandiko.

Twapaswa kufundishika, maana vyenginevyo tutakuwa miongoni mwa wale waliotajwa “kuwa na macho lakini hawaoni, masikio lakini hawasikii na nyoyo lakini hawafahamu.”

Ubaya ulioje kuwa miongoni mwao!

Mfano mmoja maarufu ulimwenguni ni ule wa Socrates, mmoja kati ya wanaharakati wa kale.

Tunasoma katika vitabu kwamba Socrates aliwaandama watawala wa Athens kwa kutumia mbinu ya udadisi na uchambuzi wa mambo yaliyoonekana ya kawaida tu, lakini muhimu sana kwa maisha ya watu.

Hayo ni kama vile imani juu ya Mungu, uzuri wa matendo, uadilifu, ilimu, maumbile na kadhalika. Mbinu hii iliuvuta umma wa watu, wengi wao wakiwa vijana, ambao walimchukulia kuwa kigezo chao.

Katika Phaedo, kitabu kilichoandikwa na Plato, aliyekuwa mwanafunzi wa Socrates, tunamsikia mwenyewe akijitetea mahkamani: “Wao (watawala) hukereka mno na hili, na si kuwa wanakerwa na udhaifu wao walionao, bali kwa kuwa udhaifu wao umedhihirishwa na kubainika, na basi huishia kunilaumu na kunichukia mimi.”

Khatima ya kukereka huku kwa wakubwa ikawa ni kumtoa muhanga Socrates, ambaye tunaweza kumuita kuwa ni aalimu mkubwa wa wakati wake na mwanaharakati jasiri.

Alishitakiwa kwa makosa mawili. Kwanza ni kusambaza mafundisho ya kumkana Mungu. La pili ni kuwachochea vijana kuipinga serikali yao. Makosa haya mawili yalimuhalalishia adhabu ya kifo.

Naye, licha ya kupewa fursa ya kujitetea ili aisalimishe roho yake na mauti, kwa kuahidi kuwa angeliiwacha kabisa kazi hii, mwanafalsafa huyu alikataa kwa kusema: “Waheshimiwa waungwana, licha ya kuwa mimi ni mtumishi niliyejitolea kwenu, lakini nina jukumu la kuonesha utiifu wa kiwango cha juu zaidi kwa Mungu wangu na sio kwenu nyinyi; na madhali ninaendelea kuvuta upumzi huu na kuendelea kubarikiwa vipawa hivi nilivyonavyo, basi kamwe sitaacha kuifanya kazi hii ya kuufunua ukweli kwa kila mtu nimkutaye…. Na sitaliacha hili, hata kama itabidi nife mara mia moja!”
Maskini, Socrates akafa akiamini kuwa ni bora kuishi siku moja kama mwanaadamu, kuliko kuishi miaka alfu kama dude, maana ‘the unexamined life is not worth living’ – maisha yasiyotathminiwa, hayana thamani kuyaishi.

Maisha yake yalizimwa pale, lakini ukweli ni kuwa ameendelea kutukuzwa hadi leo hii ulimwenguni.

Hiyo ndiyo gharama ya kuwa mwanaharakati, na ndilo lipo la kuwaambia ‘hapana’ watawala wasiopenda kubadilika.

Wala watawala wa aina hii hawahitaji sababu kubwa ili wapate kumvamia raia wake wanayemuhisi kuwa ni hatari kwao.

Vile kuwa tafauti na wao tu, ni sababu inayotosha kabisa kukupambanisha na ghadhabu ya dola.

Kwamba kama unahitaji kuishi salama usalimini chini ya tawala kama hizi, basi ni kukubali kuwa kama vile wakutakavyo wao uwe.

Wanakutaka uitikie wimbo wauimbao, na ucheze ngoma waipigayo. Na katika kufanya hivyo, usioneshe tafauti yoyote ile – hata ile ya kuuimba wimbo huo huo kwa ghuna nzuri zaidi au kunengua kwa minenguo mororo zaidi kuliko wao. Kwao, hilo litahesabika kuwa ni tendo la kiadui.

Dunia imejaa mifano mingi zaidi ya wanaharakati wanaolipia gharama kubwa kwa uwanaharakati wao.

Kuna waolipotea kiajabuajabu. Kuna waliopaswa kuzihama nchi zao. Kuna waliodhalilishwa na kuteswa kwa mateso mabaya mabaya.

Na wote hawa waliteseka kwa kusema kwao: “Hivi sivyo, hili silo!” – kwa kuhojihoji kwao kusikokwisha.

Lakini dunia shimo la sahau. Leo hii, wa wapi wateswa na watesaji? ‘In’da Rabbihim yansiluun! Wameshawasili mbele ya Mola wao, naye ndiye Mbora wa walipaji na Mkali wa kuadhibu!
Basi kupatwa na mazito ni katika kawaida za harakati. Na nadhani wengi wetu, katika sisi watawaliwa, tunalijuwa hilo.

Sote tunajuwa kuwa kuwakosoa wakubwa kuna khatari zake nyingi sana. Tunajuwa kuwa watawala wana nguvu za kila aina na wanaweza kuzitumia nguvu hizo dhidi yetu, pindi wakitaka.

Tunajuwa kuwa wanaweza kutumia nguvu zao kutubambikia mashtaka ya uhalifu au hata uhaini. Wanaweza kuyafanya maisha yetu yawe kitendawili.

Bali wanaweza hata kuwageuza wake zetu kuwa vizuka na wenetu kuwa mayatima. Wanaweza hawa, hakuna linalowashinda, pindi wakiamua.

Lakini kadiri tunavyoyajuwa hayo, ndivyo tunavyozidi kupata ujasiri wa kuzikosoa serikali kandamizi. Kwa maana nyengine ni kuwa kujuwa kwetu huko, hakupunguzi chochote katika dhamira yetu ya kurekebisha hali mbovu iliyopo.

Sisi raia tumeshajifunza na tumeshaielewa. Zilizokuwa hazijajifunza wala kuelewa ni serikali zetu.

Bado hazijajifunza kuwa hakuna utawala wowote ulimwenguni uliodumu katika madaraka yake kwa kutumia mbinu hizi chafu.

Pengine inaziwia vigumu kuamini, lakini ni historia hii hii ndiyo inayotudihirishia kuwa kuinamako ndiko kuinukako, na kuinukako kukainama.

Lini watawala wetu watakuwa tayari kukabiliana na ukweli huu?


Filed under: KALAMU YA GHASSANI
Viewing all 854 articles
Browse latest View live