Quantcast
Channel: Zanzibar Daima – Zanzibar Daima
Viewing all articles
Browse latest Browse all 854

Kinachowafanya Uamsho waendelee kusota rumande

$
0
0

Serikali zote duniani zinakuwa na nguvu nyingi, ukiacha vyombo vya dola ambavyo siku zote husimama imara vikiwa upande wao, hata ikitokea serekali inaboronga basi wao huendelea tu kusimama nayo.

Ni mara chache sana vyombo vya dola kuwa kinyume na serekali, inatokea lakini ni baada ya mure mrefu wa kuwa bega kwa bega na serekali, hata ikitokea wakiasi basi ni kutokana na maslahi yao zaidi na wala si maslahi ya raia.

Nguvu nyegine kubwa ambayo serekali nyingi wanakuwa nazo, ambayo ndio mzizi wa makala hii, ni hili suala la matumizi ya sheria, wakati mwengine sheria hutoa nguvu kwa serekali.

Ndio maana hutungwa baadhi ya sheria zikitoa nguvu nyingi kwao, hili tumelishudia tangu enzi za ukoloni, pale wakoloni walipokuwa wanatunga sheria zilizowapa wao nguvu.

Sheria ambazo hutungwa makusudi kutoa nguvu kwa serekali na sheria ambazo hazijatungwa makusudi hivyo, kuna wakati hizi zote hutumika kwa ajili ya maslahi ya kiserekali, inapobidi kufanya hiyo. Wakati huo zaidi inakuwa ni maslahi wala sio upatikanaji wa haki.

Na Rashid Abdallah

Wakati vuguvugu la Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu (JUMIKI), almaarufu Uamsho, linaanza takriban miaka mitano au sita iliyopita, lilianza kidogo kidogo kisha likakuwa kwa nguvu zilizochangiwa na wafuasi wao kuwaelewa vizuri mno, nguvu zikaanza kuhofiwa na watawala wetu.

Sio kitisho tu cha uimara wa Muungano walichokiweka, pia uimara wa kukubalika serekali zetu hasa upande wa Zanzibar nao ukaanza kutikisika, Uamsho sasa wakaonekana ni watoto wanaochezea ndevu za mzee.

Nguvu za kukusanya watu kutoka pembe zote za visiwa na kujaza wafuasi katika mikutano yao, wakieleza kinaga ubaga hatima ya Zanzibar hasa katika muktadha wa muungano, zilizidi kuihenyesha Serekali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) na hasa Chama cha Mapinduzi (CCM).

Nitakueleza sababu. CCM na viongozi wa kiserekali ndio ambao walikuwa wanapingana na Uamsho wazi wazi, hadi hapo Chama cha Wanachi (CUF) kilikuwa hakijawah kutoa tamko rasmi ikiwa wanapingana na Umasho au wanawaunga mkono, kwahiyo kwao haikuwa tatizo.

Tatizo likawa kwa CCM/SMZ ambao walikuwa wanapingana na watu ambao wameshabeba rundo la wafuasi. Na kuifanya CCM hadi kuanza kupoteza wafuasi. Ndipo hapa sasa ilipotafutwa mbinu ya kuwanyamazisha Uamsho.

Kwa vifungu vyao walivyovitumia, wakaamua kuwapachika kesi ya Ugaidi na kesi nyengine kadhaa, kisha bado wakaona kuwaacha Unguja wataendelea kuleta hatari, ndipo walipowahamishia Dar es Salaam kwa siri na ulinzi usio wa kitoto. Kwa sasa wamekuwa na kesi isiyokwisha, nenda rudi na ushahidi uliokosa kukamilika hadi sasa.

Hofu zote watawala wa CCM waliokuwa nazo, zaidi ilikuwa ni ule uchaguzi ambao tuliuwelekea, waliamini kuwaacha Uamsho nje wakati nchi inaelekea kwenye uchaguzi, wangekuwa ni kikwazo kibuwa kwa mafaniko yao.

Na huo ndio ukweli, Uamsho walikuwa tayari wameshaingia katika damu za Wazanizibar, wengi wa Wazanzibar wanamini Uamsho ndio waliowafumbua macho na kuona upi hasa ni muelekeo wa nchi yao.

Kufunguka macho huku kwa raia kukawa ni tatizo kwa uongozi wa muda mrefu wa CCM, sheria ndio zikatumika kama silaha kuwafumba midomo nyuma ya nondo za vyuma katika magereza ya Tanzania bara.

Uamsho hawakuwa wanavunja sheria, walikuwa wanatumia haki yao kikatiba kukusanyika na kujadili masuala ya nchi yao na kutoa maoni yao juu ya Muuungano.

Uchaguzi ulipoisha mategemeo makubwa Uamsho wangetoka na kuwa huru, kwa sababu lile daraja la hofu CCM walilokuwa wanaliogopa tayari liikuwa tumeshavuuka.

Swali ni kwanini bado Umsho wanasota ndani wakati uchaguzi umeisha? Jawabu ni moja kubwa, siasa za Zanzibar ambazo bado hazijatulizana zinaendelea kuwapa hofu watawala na hivyo azimio lao la kuwaacha Uamsho baada ya uchaguzi linaendelea kukwama.

Ukweli ulio wazi, ingekuwa hali ya kisiasa Zanzibar imeshatulizana hakuna tena mikwaruzano, ni wazi wangeachiwa huru, kwa sababu kilichowafanya wawekwe ndani tayari kilishapita.

Hizi ndio zile nguvu za kisheria serekali nyingi duniani wanakuwa nazo, huzitumia sheria kwa maslahi yao ya kisiasa, kwa sababu kuwakamata watu na kuwaweka tu ndani duinia isingewaelewa hata kidogo.

Lakini ili dunia iwaelewe ni lazima utafute kesi ya kuwapachika, iliyo nzito inayotishia amani kisha ndio sasa uwashike mmoja mmoja uwanyime dhamana kwa kutumia hiyo hiyo sheria, halafu uwatoe kila mwezi mara moja au mbili kwenda mahakamani.

Wakifika huko, ushahidi wa kesi unaendelea kutokukamilika, hii huchukua muda hadi pale lengo lao la kuwaweka ndani litapo malizika, dunia haitopiga kelele kwa hali kama hii.

Kwa sababu inaona kuwa wanayo kesi ya kujibu, wamekamatwana kuwekwa dani na mahakamani wanapelekwa kila siku, hata watetezi wetu wa haki za binaadamu ndio unawakuta wamekaa kimya.

Kwa sababu wamefungwa midomo kikanuni, kila kitu kinakwenda kikiwa juu ya mstari, kimefunikwa makoti ya tuhuma na fulana za sheria lakini kumbe uongo mtupu na usanii usiokwisha.

Hatujui hali ya Zanzibar itatengemaa lini, ikiwa Zanzibar itaendela kutikisika kisiasa watu hawa nao wataendelea kubaki tu ndani, maana kule kwao wanaogopwa wakirudi wataenda kuitikisa hali zadi, na nguvu zao ni kubwa mno.

Miaka minne mumeshika dazeni ya watu mmeshindwa hata mmoja kuthibitisha uhusika wake juu ya mnachokidai! Si usanii ni kitu gani hicho, ni kufanya uhuni tu kwa kutumia sheria.

Kinachobaki sasa anayezungmzia sakata hili, anaanza kutengenezewa mazingira ya kupachikwa kesi ya uhaini. Hakuna upelelezi wowote ila ni maigizo ili kuiridhisha dunia kuwa hawajawashikilia kinyume na sheria.

Lazima niweke wazi jambo moja hapa, mimi sipo kutetea uhalifu wa aina yoyote,hata Uamsho ikiwa kweli wanahusika na hicho serekali wanachokidai, wakiwapata  na hatia bila kuwasingizia wala sina shida.

Lakni kinachoonekana sio hicho, siasa ndio inagubika kwa kiasi kikubwa uhalisia wa kesi hii, masheikh wenywe wanaamini maoni yao juu ya Muungano ndio yamewafikisha pale.

Pia usisahau kuwa viongozi wetu wote hadi huyu wa sasa hula viapo majukwani kuulinda muungano kwa gharama zote, hata kwa wale wanaotoa maoni kisha maoni yao yakaonekana kuwa na nguvu kwa kundi kubwa la watu, hutafsiriwa wanahatarisha muungano.

Ikiwa serekali inataka unyamaze, kukuweka gerezani ndio njia nyepesi na kiungwana kwao, kwani wengine hufutwa na hawaonekani tena, kwasababu baadhi ya serekali  huamini mchakato wa mahakama utakuwa mrefu sana.

TANBIHI: Mwandishi anapatikana kwa simu nambari +255 657 414 889


Filed under: JAMII Tagged: jamhuri ya muungano wa tanzania, Magufuli, Segerea, Tanzania, Uamsho, Zanzibar

Viewing all articles
Browse latest Browse all 854

Trending Articles