Quantcast
Channel: Zanzibar Daima – Zanzibar Daima
Viewing all articles
Browse latest Browse all 854

Ngeleja, shujaa au fisadi aliyeogopa?

$
0
0

Makala hii imeandikwa na Julius Mtatiro, mchambuzi wa masuala ya kisiasa na Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya Chama cha Wananchi (CUF) kwenye ukurasa wake wa Facebook ikiwa na kichwa cha habari “William Ngeleja, shujaa wangu!” Zanzibar Daima inaichapisha tena hapa ikiwa na kichwa cha habari kipya, kwani mhariri ameona kuwa ndani ya makala yenyewe ushujaa wa mtajwa unaning’inizwa baina ya uhalisia, mashaka na matazamio. Sasa endelea… MHARIRI

Kaka yangu mpendwa, William Ngeleja amefanya uamuzi wa kishujaa sana. Ameamua kujitakasa kwa kurejesha fedha za wizi ambazo aliyempa alituibia huko nyuma na jambo hili lilishafanyiwa maamuzi na bunge lakini hayakutelezwa.

Hata hivyo, namkumbusha Ngeleja kwamba makosa ya jinai hayafi milele. Ukiuwa mwaka 1970 halafu ukaombwa ujitokeze, ukakataa, halafu mwaka 2017 (miaka 47 baadaye) ukajitokeza na maburungutu ya pesa au roho na mwili wa mtu mwingine ili uwakabidhi ndugu wa mtu uliyemuua kwa maana ya kuwalipa fidia, vitu vyako vitapokelewa lakini havifuti jinai.

Ukiiba hela za walalahoi mwaka 1950, halafu miaka 67 baadaye ukajitokeza na hela mara milioni elfu moja ya zile ulizoiba, zinaweza kupokelewa kwa mbwembwe kubwa, lakini hiyo haifuti jinai. Hata kama leo ungelikuja na viwanda vyote vya Mo na Bakhressa na vya Dangote uwakabidhi uliowahi kuwaibia senti tano huko nyuma, hiyo haifuti jinai!

Ukishatenda jinai, makosa ambayo humaanisha umeshindwa kuwa mwaminifu kama hili la kina Ngeleja, wewe ni mtenda jinai na dunia yote sheria ziko wazi kabisa. Jinai haijadiliwi, haitafutiwi ufumbuzi, haifanyiwi maridhiano. Jinai ni makosa yenye adhabu kwa mujibu wa sheria na adhabu hizo hazina mjadala.

Na Julius Mtatiro

Kama tungelikuwa na serikali iliyo makini na inayokata kotekote, baada ya mkutano na waandishi wa habari wa kaka yangu Ngeleja, ilipasa maafisa wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) wamsubirie geti la HABARI MAELEZO na asionekane hadharani hadi awe mahakamani, kama akina James Rugemarila!

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Happi, ni juzi tu hapa alitumia ile sheria ya kikoloni, kibaguzi na ya kitumwa, akaamuru Halima Mdee akamatwe mara moja na kusota rumande, kwa sababu tu Halima alizungumza na vyombo vya habari na akaonya juu ya mienendo ya Rais John Magufuli.

Ni juzi pia wale viongozi karibu 50 wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) waliokuwa kwenye kikao halali cha ndani huko Geita, walizingirwa na polisi na kukamatwa kwa nguvu kubwa sana. Kisa walikuwa wanatimiza haki yao ya kikatiba kama chama cha siasa.

Undumilakuwili kwenye uchukuwaji hatua

Huwa najiuliza, hivi tuna dola ngapi Tanzania? Hivi tuna serikali zinazofanya kazi kwa kutumia sheria zipi kuhusu wale wa Geita au zipi kwa mbunge wa Kawe inapolinganishwa na hii ya Ngeleja?

Godbless Lema alipotangaza ile ndoto yake. Aliishia gerezani miezi minne, lakini Ngeleja ametangaza hadharani kuwa amerudisha fedha za wizi, hadi sasa yuko kwake! Tunataniana?

Unawezaje kumshughulikia mtu aliyetabiri mambo ya kufikirika tu ambayo umeamua kuigiza kuwa mambo hayo ni kinyume na sheria, na wakati huo huo ukamuacha huru mtu ambaye ameeleza mambo halisi ambayo ni makosa ya jinai yasiyo na mjadala?

Rugemarila pia ni binadamu jamani, kama yeye yuko gerezani kwa sababu ya fedha alizoiba, vipi kuhusu wale waliopokea fedha hizo za wizi na tena wengine wakasema ni hela za mboga?

 

James Rugemarila (kushoto) akiwa mahakamani anakoshitakiwa kwa makosa kadhaa likiwemo la kuiibia serikali.

Kama Rugemarila yuko gerezani kwa kukwapua fedha za umma, vipi wale watendaji na viongozi wa serikali na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) walioidhinisha fedha zile zitoroshwe wako huru mitaani? Yaani unamkamataje mwizi aliyeiba fedha halafu wale waliomfungulia geti na kumhesabia fedha kwa hiyari na wale waliowatuma wakiwemo hadi watendaji wa ikulu, wako mitaani salama?

Kama kweli taifa langu lingekuwa na sheria zinazokata kotekote, unamshughulikiaje Rugemarila na kuwaacha watendaji wa Benki ya Stanbic na Benki ya Mkombozi ambao walizitumia benki zao kutakatishia fedha hizo bila kujali kuwa kufanya hivyo ni kinyume na taratibu za fedha na sheria za nchi?

Tunakumbuka kuwa bunge liliazimia fedha zile zirejeshwe kwa kulipiwa kodi. Ilikuwa mwaka 2014, lakini akina Ngeleja hawakurudisha fedha hizo, akina Chenge, Askofu Methodius Kilaini na wenzao waliendelea kuwa na misimamo kuwa zile ni fedha halali. Nini kinachotokea hii leo? Wanawezaje tu kuzirudisha kienyeji namna hii?

Askofu Kilaini ni askofu wangu, maana mimi ni Mkatoliki. Huku Marekani, wapo wachungaji, maaskofu, mapasta, mapadre wako gerezani, walishtakiwa na kufungwa, kama watu wengine. Siwezi kuwatetea watu walioshiriki kuliibia taifa, hata kama angelikuwa Papa wa Kanisa!

Unamshughulikiaje Rugemarila kwa wizi wa fedha zile kama mwizi mkuu, halafu ukamuacha jaji wa mahakama kuu ambaye alipokea fedha za umma kama rushwa au fedha haramu? Jaji unamstaafisha kwa maslahi ya umma, yeye hawezi kukaa jela! Kwamba Jaji ana mke mzuri na muhimu kwake kuliko Ruge? Undumilakuwili!

Chenge naye, pamoja na kushiriki kwenye masakata yote makubwa ya wizi kuanzia ule wa rada na bado kupokea shilingi bilioni 1.6 za rushwa kutoka kwa Rugemarila, bado ameendelea kuwa mtu muhimu ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na nchi, na leo hii Chenge ni Mwenyekiti wa Bunge. Hivi tuko makini kweli? Yaani Rugemarila yuko gerezani kwa makosa makubwa, lakini walionufaishwa na fedha zinazomponza Rugemarila wanapeperusha bendera za serikali mitaani?

Yaani inaingiaje akilini kuwa umuweke Mdee ndani kwa masaa 120, umuweke Lema gerezani miezi minne, lakini Chenge yeye yuko mtaani tu! Hakika tunadanganyana sana! Hivi kati ya Chenge na Lema, nani ameihasidi nchi hii? Hivi kati ya Chenge na Mdee nani ameichafua nchi hii? Yaani hawa wanaotoa maoni yao, na kushauri na kuonya serikali, wao wanaishia jela. Yale majizi makubwa yanadunda mtaani na bado kuna watu wanakwambia nchi imebadilika kwelikweli. JPM ameinyoosha!

Wote wanawania kumridhisha Mtukufu Rais 

Na kichekesho kikuu kinaweza kuwa kwamba hata hao wanaochukuliwa hatua na kufikishwa mahakamani, TAKUKURU haifanyi hivyo kwa weledi wao, bali wanamtumia ishara Rais Magufuli na kuona kama angelipenda mtu fulani afikishwe mahakamani. Sote tunajua kuwa kwa utawala wa sasa hakuna anayefanya maamuzi. Kila kitu watu wanasubiria kupima upepo, ikiwa kina madhara kwao (kitamfurahisha Rais au la!) Maana kwa sasa unaweza kufanya maamuzi mazuri, lakini Rais asiyapende, utatumbuliwa, na ukifanya maamuzi mabaya akayapenda unaweza kubaki (na kinyume cha kila moja), kwa hiyo ponapona yako ni kutokufanya lolote hadi uwe na uhakika kuwa litamfurahisha Rais.

Andrew Chenge, mmoja wa viongozi waliotuhumiwa takribani katika kila kashfa kubwa ya hivi karibuni ya ufisadi serikalini.

Unaweza kukuta TAKUKURU wana ushahidi dhidi ya Askofu Kilaini, kwamba anastahili kushtakiwa, lakini unaweza ukashangaa wakubwa wanawaambia, “huyo mwacheni, huyo ni Askofu!” Kwa kweli hili ndilo taifa tunalojenga, taifa linaloongozwa na utashi wa mtu mmoja mmoja katika uongozi kuliko kuongozwa na taasisi ambazo zinafuata viwango.

Nchi zinazofuata viwango, askofu akibaka na mvuta bangi akibaka, wote watashtakiwa na wote watafungwa ikiwa wana hatia. Lakini kwa Tanzania, Ruge na Chenge wataiba pesa na kugawana, kisha Ruge atakwenda gerezani na Chenge atabaki mtaani, na bado Watanzania wanapiga makofi kuwa hatua zinachukuliwa! Tutasubiri milele, kama hakuna viwango katika hatua zetu hatutapiga hatua. Kama tukisubiri kuongozwa na sauti ya mtu mmoja hatutakwenda mbele.

Tunaendelea kujenga taifa lenye ubaguzi mkuu na lenye aibu. Ndiyo maana leo Rais anakwenda Sengerema anahutubia mkutano wa chama chake kwa kigezo cha urais wake lakini vyama vingine vimezuiliwa kufanya mikutano, hata ya ndani, na wapo watu wanashangilia kuwa “ngoja awakomeshe wapinzani, 2020 wawe wamemalizika” na anayesema hayo ni Mtanzania masikini ambaye hata bima ya afya ya uhakika hana.

Nani amesema kuwa kwa hatua hizi za undumilakuwili za sasa eti Freeman Mbowe anakomeshwa? Eti Maalim Seif Sharif anakomeshwa? Eti James Mbatia anakomeswa? Eti Zitto Kabwe anakomeshwa? Hivi hata hiyo 2020 ikiwa Watanzania wataichagua CCM kwa asilimia 100, Zitto ataathirikaje? Mbatia ataathirikaje? Maalim ataathirikaje? Mbowe ataathirikaje?

Yaani tunakisia kuwa wote siyo wabunge na wako mitaani tu, wataathirikaje kukushinda wewe ambaye hadi leo hujui utaajiriwa lini na nani? Au wewe ambaye umeajiriwa na mshahara wote unatumika kupandia daladala na kula mlo wa mchana?

Bila viwango, mbele kuna giza

Nchi yetu inapoendeshwa kwa undumilakuwili wa kuchukua hatua dhidi ya watu fulani na siyo wengine kwenye jambo lile lile, nchi hiyo haiwezi kupiga hatua, itakuwa inarudi nyuma kweli kweli.

Inaonekana kila afisa serikalini na kwenye chama tawala anataka kutenda jambo la kumridhisha Rais John Magufuli na sio kujenga taasisi imara za nchi.

Kwenye masuala ya viwango masuala ya msingi yanayohusu nchi na sheria zake, askofu ana wajibu ule ule alionao mwanafunzi wa Chuo Kikuu, Rais ana wajibu ule ule alionao mama kule kijijini Kiabakari, mwenyekiti wa chama cha siasa kinachoongoza dola ana haki na wajibu ule ule wa yule mwenyekiti wa chama ambacho hakina dola, sheikh ana wajibu ule ule ambao anao mfanyakazi au mkulima. Sote tuna wajibu katika viwango vyetu.

Tukiendelea kwenda mbele bila viwango, tutaona baadhi ya watu wanakomeshwa na wengine wakila bata! Kwangu mimi, Rugemarila ana haki sawa sawa na Chenge, na Ngeleja, na Anna Tibaijuka na kadhalika, maana naye ni binadamu pia. Ana watoto, mke, na ndugu na wana uchungu naye.

Hakuna namna yoyote kwamba kwamba eti askofu, waziri, au mbunge fulani ni muhimu katika nchi kuliko na ana utaratibu tofauti mbele ya sheria na haki tofauti na mtu wa kawaida. Ndiyo maana kila siku nasema na nakumbusha maneno ya Barack Obama alipokuwa Ghana: “Afrika haihitaji watu imara, inahitaji taasisi imara!”

Mfano huu wa Obama kwa baadhi ya watu wanaofikiri kinyume chake, nawapa changamoto. Wale wanaoamini kuwa JPM ni Rais bora sana, anapambana na rushwa na ufisadi, nataka niwaambie kuwa kama huo uimara wa JPM hatautumia kujenga taasisi imara, na akaendelea kujilimbikizia madaraka na amri na kila kitu, baada ya miaka yake mitano au kumi kuisha, Tanzania itabakia na bunge dhaifu, mahakama dhaifu, serikali dhaifu, TAKUKURU dhaifu na kila kitu dhaifu. Na hapo ndipo wale watetezi wa hoja kuwa ujenzi wa taasisi imara unahitaji watu imara, wataelimika kwamba kiongozi imara asiyejenga taasisi imara ni sawa na mtu anayechota maji kwa kutumia tenga.

Kitendo cha kaka yangu Ngeleja nakiita cha kishujaa kwa sababu kimeivua nguo serikali nzima, kwamba mwizi anaweza kusimama hadharani na kutamba kuwa anarudisha fedha za wizi na baada ya tambo zake akarejea hadi kwake na kulala huku wezi wenzie waliomuibia fedha hizo wako gerezani. Yaani ni sawa na mmeibiwa ng’ombe, kisha mwizi halisi mkamkamata na huku mkiwajua wale ambao mwizi alikwenda kuficha ng’ombe huyo kwao na wao wakijua ng’ombe ni wa wizi na wakakaa na ng’ombe kwa miaka kadhaa, kisha siku moja wanamrudisha bila hofu na mnampokea na mnawaacha watunza ng’ombe wa wizi wakirejea makwao huku mwizi mkuu yuko gerezani!

Nakushukuru sana kaka Ngeleja, shujaa wangu wa leo!


Filed under: SIASA Tagged: Escrow Tegeta, Tanzania, ufisadi, william ngeleja

Viewing all articles
Browse latest Browse all 854

Trending Articles