Quantcast
Channel: Zanzibar Daima – Zanzibar Daima
Viewing all articles
Browse latest Browse all 854

SMZ iondowe utata kima cha mishahara sekta binafsi

$
0
0

Nimelichukuwa tena na kulisoma kwa makini zaidi agizo la serikali lililochapishwa katika Waraka wa Sheria Nambari 68 (The Legal Notice No.68) kuhusu ongezeko la mshahara wa kima cha chini kwa sekta binafsi, zikiwemo taasisi zote ambazo zinamilikiwa na watu binafsi wa nchini na wageni, wawe wakubwa au wadogo, likitokana na Sheria Nambari 11 ya mwaka 2005, Kifungu Nambari 97 (1) lililosomwa na waziri mwenye dhamana ya kazi katika serikali ya Zanzibar, Maudline Castico, mbele ya waandishi wa habari mnamo tarehe 2 Julai 2017, aliagiza kwamba utaratibu huo wa mishahara ulitakiwa kuanza tarehe 1 Julai, yaani siku moja nyuma.

Katika waraka huu wa kisheria nimegundua kwamba kuna baadhi ya changamoto katika agizo lile, lakini nilikuwa na imani ya hali ya juu kwamba wengi wa waajiri wetu si wapingaji wa sheria mpya na hata zile kongwe ambazo zinaongoza makampuni yao.

Hapa nimeonelea ni vyema nizieleze changamoto hizi ili kama wahusika wataafikiana na mimi zitatuliwe na mapema. Kwa mfano, katika agizo hilo, Kipengele Nambari 1 kinawataja: “employees with written contracts – 300,000/-“, yaani waajiriwa wenye mkataba – bila ya kuianisha mkataba wa muda gani wala kwa taasisi zipi, kubwa, ndogo au ya kati – wote walipwe mshahara wa shilingi 300,000/-.

Na Ali Mohammed

Ni wazi kuwa baadhi ya waajiri wataingia makosani kwa kutotekeleza agizo hili kwa sababu tuchukulie mfano muajiri ana kioski pale Kwa Mchina kilicho rasmi na ameajiri wafanyakazi wawili na wote wana mikataba, lakini mtaji wake ni shilingi 2,000,000/-, sasa atawezaje kulipa 300,000/- na bado juu ya kima hicho pia aongeze na asilimi nyengine 13 kumlipia kila mwajiriwa wake mafao ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (ZSSF)? Je, akifanya hivyo si atakuwa ameshaiuwa biashara yake?

Katika Kifungu Nambari 2 cha agizo hilo imeandikwa: “Emplyees with with written contracts for small institutions established under regulations – 180,000/-“. Labda ungelifikiria kuwa hofu na utata uliopo katika Kifungu Nambari 1 unaweza kupatiwa mwarobaini wake katika kifungu hichi, lakini bado kifungu hichi nacho kinazidi kukipinza Kifungu Nambari 1 na kisha kujipinza chenyewe, kwa sababu kifungu kinasema, “waajiriwa wenye mikataba ambao wanafanyakazi katika taaasisi ndogo zilizoainishwa katika kanuni watalipwa 180,000/-”.

Lakini hadi naandika makala hii, ikiwa ni tarehe 15 Julai 2017, hiyo kanuni iliyotajwa inayoainisha ni ipi taasisi ndogo, haipo hewani na haijawahi kuwepo na kama ipo basi waajiri haijawahi kuwafikia.

Kwa upande wa vifungu nambari 3,4 na 5 vinavyoelezea ajira za vibarua, hakuna tatizo katika utekelezaji, bali lipo kwenye zile fursa za ndugu zetu ambao wao hawapendi kuajiriwa moja kwa moja, ambao daima wanapenda kuwa vibarua, yaani ajira za kutwa. Kwa ungezeko hili la malipo ya kibarua la asilimia 200, wasitegemee kwamba fursa hiyo itakuwepo. Hata ikitokea, basi haitakuwa ya muda mrefu, mana ikiwa muajiri atakuajiri kama kibaruwa, kwa muda wa siku 26, atatakiwa kukulipa 780,000/-, wakati akikupa mkataba, atakulipa 300,000/- pekee. Hivyo muajiri atakhiyari akuajiri ili mshahara wako wa siku 26 alipe watu wawili na chenji ibakie.

Wakati naandika makala hii, mmoja miongoni mwa wadau wa ajira amenipasha habari kwamba Jumiya ya Waekezaji katika Sekta ya Utalii (Zanzibar Association of Tourism Investors – ZATI), wamemuandikia waziri husika juu ya changamoto mbalimbali zilizomo katika waraka huo na hata kulalamikia wizara kwamba wamekwenda mbali sana kwa ongezeko hilo la mshahara kwa zaidi ya asilimia 100% kwa waajiriwa wenye mikataba na kwa asilimia mia 200% kwa waajiriwa wa vibarua.

Kabla ya kutangazwa kwa kima kipya cha mshahara, mwaka jana Jumuiya ya Waajiri Zanzibar (ZANEMA) ilifanya mkutano katika ukumbi wa Kiwanja cha Kufurahishia Watoto cha Kariako, ambapo mkurugenzi wa jumuiya hiyo, Bwana Salah Salim Salah, aliwaelezea wajumbe lengo hilo la serikali kupandisha mshahara na waajiri wakasema bayana kwamba hawana uwezo wa kulipa kima hicho cha mshara na wakaitahadharisha wizara kwamba endapo ingesimamia maamuzi hayo, basi kwa kuwa wataathirika kimapato kutokana na kwamba bili ya mshahara itapanda na faida yao kushuka, basi wao waajiri watatekeleza kifungu cha sheria ya kupunguza wafanyakazi.

Makala hii haina lengo la kuwatetea waajiri wasilipe kima kilichowekwa na serikali, lakini lengo ni kuzishauri pande zote hizi kukaa tena pamoja kwa maridhiano na kutoka na kitu kitakachoondowa hali hizi za utata, hofu na mifarakano inayotarajiwa kutokea kuanzia tarehe 1 Agosti 2017, ambapo waajiri watakuwa wameshafanya maamuzi aidha kutekeleza agizo hilo au kulitupilia mbali na kujifichia kwenye utata nilioueleza hapo awali.

Tukizidharau changamoto hizi na tuking’angang’aniza bila ya kulipitia upya agizo lenyewe la serikali na endapo waajiri watatumia haki yao ya kupunguza wafanyakazi iwe kwa kutowapa mikataba mipya wale wanaomaliza mikataba yao au kwa kutumia sheria ya punguzo la wafanyakazi, tutakuwa hatukuwatendea haki wafanyakazi ambao ni ndugu na jamaa zetu, na zaidi tutakuwa tumekwenda kinyume na agizo la Mkataba wa Kimataifa Namba 131 wa (ILO Minimum Wage Fixing Convention, 1970 No. 131), ambapo Zanzibar na Tanzania kwa ujumla tumetia saini kuuridhia kikamilifu.

Mkataba huo wa kimataifa unasema katika Kifungu Nambari 3 kuwa ongezeko la mshahara wa kima cha chini lizingatie mambo yafuatayo:

  • Ukuaji wa kiuchumi
  • Engezeko la ajira
  • Kuangalia uwezo wa Muajiri

Sasa kwa mambo hayo matatu yafaa tujiulize:

a) Je, uchumi umekuwa kwa kiwango gani kumuezesha muekezaji kumudu kulipa kima hicho?
b) Endapo waajiri wakiamuwa kupunguza wafanyakazi, je ajira itaengezeka au itapunguwa?
c) Je, waajiri wote wanalingana kiuwezo kuweza kumudu kima hicho?


Filed under: JAMII Tagged: ajira, kima cha chini, mishahara, uwekezaji, Zanzibar

Viewing all articles
Browse latest Browse all 854

Trending Articles